MWANANCHI
Utata umeibuka kuhusu bastola waliyodaiwa kukamatwa nayo wafuasi
wa Kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Askofu Josephat Gwajima baada ya kiongozi huyo kusema
anaimiliki kihalali kinyume na maelezo ya polisi.
Gwajima aliyetolewa kwenye chumba cha uangalizi maalumu cha
Hospitali ya TMJ jana, amelitaka Jeshi la Polisi kurudisha bastola hiyo,
akisema ni mali na aliiagiza ipelekwe hospitalini kwa sababu ya kujilinda.
Akizungumza na waandishi wa habari hospitalini hapo alipolazwa
baada ya kuishiwa nguvu na kupoteza fahamu akiwa katika mahojiano na polisi,
Gwajima alisema anashangaa kukamatwa kwa wachungaji wake waliokuwapo kwa ajili
ya kumlinda.
Hata hivyo, katika kwa upande mwingine, Kamanda wa Polisi Kanda
Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema bunduki hiyo haina umiliki
halali wa Gwajima wala wa wachungaji 15 waliokamatwa lakini baadaye jioni baada
ya maelezo ya Gwajima, alitoa taarifa akisema bastola hiyo ni mali halali ya
askofu huyo.
Pia alisema kuhusu risasi 17 za bunduki aina ya Shortgun, Gwajima
anamiliki bunduki ya aina hiyo lakini akasema uchunguzi kuhusu watu hao 15
unaendelea.
Akizungumza kwa shida akiwa amejishika tumbo, Gwajima alisema
alipopata taarifa za uvumi kwenye mitandao ya kijamii kuwa amefariki dunia,
aliagiza wachungaji waende hospitalini kwa ajili ya kumlinda, lakini wakaishia
mikononi mwa polisi wakidaiwa kutaka kumtorosha.
Alisema alihofia kuwapo kwa watu wabaya ambao wangeweza kumdhuru
halafu wakasingizia kitendo hicho kufanywa na polisi kwa kuwa alipata tatizo
akiwa mikononi mwao.
“Usiku wasiwasi ulizidi, huku
kila mmoja akiwa hafahamu kwa nini ujumbe wa namna ile unasambazwa kwenye
mitandao, msambazaji ni nani, ana nia gani, nikaamua kuwaagiza waniletee silaha
yangu iliyokuwa kwenye begi ili likitokea lolote niweze kujilinda,”Gwajima.
Alisema alishangaa kukamatwa wachungaji wake na kuchukua silaha
iliyokuwa ndani ya begi na hadi jana hakuwa ameulizwa chochote kuhusu umiliki
wa silaha hiyo.
“Kabla sijazungumza na waandishi
kueleza ukweli wa kinachodaiwa kuwa nilitaka kutoroshwa na wachungaji wangu,
nilitaka kuzungumza na ZCO (Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu), lakini hajaja,
kadi ya ile silaha ninayo,” alisema Gwajima.
Alisema madai kuwa alitaka kutoroka ilihali polisi alikwenda
mwenyewe akitokea Arusha baada ya kusoma katika vyombo vya habari kuwa
anatafutwa.
Alifafanua kuwa hata alipofika polisi kwa ajili ya mahojiano
hakuwa na shaka hata kidogo, lakini alishangaa kuona anaishiwa nguvu kila baada
ya muda na alipoona kichwa kinamuuma, akawaomba wampeleke hospitali ili mambo
mengine yafuate baadaye, kitu ambacho hakikufanyika kwa wakati.
MWANANCHI
Vyombo vya usalama nchini Kenya, vinawashikilia wasichana watatu
akiwamo Mtanzania, kwa kile kunachodaiwa kutaka kujiunga na kundi la kigaidi la
al-Shabaab huko Somalia.
Taarifa kutoka kwa Kamishna wa Polisi Jimbo la El -Wak, mpakani mwa Kenya na Somalia, Nelson Marwa amesema Mtanzania aliyekamatwa,
alijieleza kuwa ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Afrika, Sudan.
Mtanzania huyo, Ummul-Khayr
Sadir Abdul (19),
mwenyeji wa Zanzibar, anatajwa kuwa kiongozi wa kundi hilo lililopanga kujiunga
na al-Shabaab.
Wasichana wengine waliokamatwa pamoja na Ummul-Khayr, ni Maryam
Said Aboud na Khadija Abubakar Abdulkadir wote raia wa Kenya.
“Hawa wasichana watatu,
inaaminika kuwa walikuwa wanakwenda Somalia kupata mafunzo ya kigaidi na
baadaye kufanya mashambulizi ya kujitoa mhanga,” Kamishna
Marwa.
Akizungumzia suala hilo, Kaimu Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai, DCI
Diwani Athumani alisema: “Tunafuatilia hatujapokea
taarifa zaidi ya hizo.”
Kamishna Marwa alisema raia hao wawili wa Kenya, mmoja
ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mount Kenya kilichopo Thika, Jimbo Kiambu na
mwingine ni mwanafunzi wa Sekondari ya Burhania, iliyopo Malindi, Kilifi.
“Serikali imepata taarifa
kuhusu watu wanaokusanya watu kutoka Afrika Mashariki ili wakajiunge na makundi
ya ugaidi nchini Somalia, wakala wetu wa usalama wamepata taarifa hizo na
kufanikisha kukamatwa kwa wasichana hao,” alisema Kamishana Marwa.
Hivi karibuni, tovuti ya al-Jazeera ilitoa taarifa za kukamatwa kwa mkanda
wa video ulioonyesha mwakilishi wa kundi la kigaidi la Dola ya Kiislamu ya Iraq
na Levant (ISIL)akimtaka
kiongozi wa kundi la al-Shabaab kuliimarisha kwa kufanya mashambulizi ya
kigaidi katika miji ya Mwanza na Dar es Salaam.
Kamishna Marwa alisema ingawa nyaraka za wasichana hao zote
zinaonyesha kuwa ni wanafunzi, lakini bado walibanwa kwa maswali kuhusu
sababu inayowapeleka nchini Somalia.
Aliongeza zaidi kuwa chanzo cha habari cha kiusalama kilieleza
kuwa nyaraka za wasichana hao zilionyesha kuwa walikuwa wakienda kuolewa na
wanajeshi wa kundi la al-Shabaab.
MWANANCHI
Wachambuzi wa soka wamesema timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa
Stars’ haina kiwango cha kuvutia uwanjani na imepoteza mvuto.
Wakizungumza baada ya kuishuhudia Taifa Stars ikilazimishwa sare
ya bao 1-1 na Malawi katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa uliofanyika Mwanza
juzi, walisema wanauona mwisho mbaya wa kocha Mholanzi, Mart Nooij.
Kocha Joseph
Kanakamfumu aliliambia
gazeti hili kuwa Nooij hajaibadilisha Stars na inacheza ili mradi tu tofauti na
mtangulizi wake, Kim Poulsen.
Kanakamfumu alisema jambo kubwa analokosea Mholanzi huyo ni uteuzi
wa kikosi chake, hasa aina ya wachezaji anaowaita kwani wengi wao hawako fiti.
“Nikiangalia hajaibadilisha timu
tofauti na wakati wa Kim kwani timu ilikuwa unaona kabisa inacheza mpira mzuri,
lakini kwa huyu timu haichezi kwa mpangilio, hatuoni mtiririko mzuri uwanjani,
kila mchezaji anajichezea anavyojua yeye,” alisema
Kanakamfumu.
Aliongeza: “Tatizo kubwa anapokosea ni
kwenye uteuzi wa timu yake, inatakiwa aangalie wachezaji anaowaita wapo vizuri
namna gani kulingana na mfumo anaoutumia, kwani wachezaji wengi aliowaita
hawaendani na mfumo wake wa kujilinda.”
Naye Eugine
Mwasamaki alisema
tatizo liko kwa kocha na hata wachezaji wake kwani kiwango cha timu hiyo si
kizuri na kinasikitisha.
Mwasamaki alisema anachoshangaa ni Nooij kuwaita kikosini
wachezaji ambao hata kwenye klabu zao hawachezi na kuwacha wengi wanaoonyesha
viwango vizuri kwenye mechi Ligi Kuu Bara.
Wachezaji ambao hawana namba ya kudumu katika klabu zao kwa sasa,
lakini wapo Stars ni pamoja na Mwadin Ally, Amri
Kiemba, Deo
Munishi na John Bocco.
MWANANCHI
Unakumbuka
masaibu ya mtoto, hayati Nasra
Mvungi aliyeishi
kwenye boksi miaka mitatu? Mkazi wa Mbondole, Wilaya ya Ilala, Uwesu Mansuri (28) naye ameishi kwa kufungwa
mnyororo mguuni na wazazi wake kwa miaka mitatu kwa madai ya kulinda usalama
wake.
Kijana
huyo ambaye anapata huduma zote za kibinadamu chini ya kibanda kidogo kilichopo
chini ya mwembe nyumbani kwao, ameonekana kudhoofika na kutoa harufu mbaya
kutokana na kutoogeshwa kwa muda mrefu.
Taarifa za
kufungwa kwa kijana huyo zilisikika kutoka kwa wakazi wa eneo hilo na mwandishi
wetu alifika eneo hilo na kushuhudia jinsi alivyofungwa na kuishi katika
mazingira machafu.
Kijana
huyo anakula na kujisaidia hapohapo, jambo ambalo limeelezwa na baadhi ya
wakazi wa eneo hilo kuwa ni la unyanyasaji na hatari kwa afya yake.
Wakizungumza
jana, wakazi wa eneo hilo walisema kijana huyo alifungwa mnyororo huo kwa zaidi
ya miaka mitatu huku akiwa analala kwenye kibanda kidogo ambacho si salama
kwake.
Mmoja wa
wakazi hao, Imelda
Saburi alisema
wanaona uchungu kwa kitendo cha wazazi hao kumfunga mnyororo kijana huyo
huku akipata maumivu makali yanayomfanya awe analia kwa sauti kila siku usiku.
Alisema
walijaribu kuwashauri wazazi hao wamfungue mnyororo huo na wampeleke
hospitalini kupata huduma za afya lakini walikataa. “Tulimfuata baba wa mtoto huyo
na kumshauri amfungue hiyo minyororo lakini alikataa ushauri wetu,” alisema Saburi.
Mkazi
mwingine, Hassan
Abdul alisema,
wanashangazwa na wazazi hao kutojali huku wakimtenga na kumlaza nje akinyeshewa
na mvua na kupigwa na jua.
Mama mzazi
wa kijana huyo, Zuena Ngarima alisema walilazimika kumfunga mnyororo
mguuni kwa kuwa amekuwa akifanya fujo na kuharibu vitu mbalimbali vya wakazi wa
eneo hilo.
Alisema
mwaka 2009, kijana huyo alianza kuchanganyikiwa na walimpeleka katika Hospitali
ya Taifa Muhimbili (MHN) na alilazwa kwa siku 19, alipopata
nafuu aliruhusiwa kurudi nyumbani.
Ngarima
alisema wakati kijana huyo akipata ugonjwa huo, baba yake mzazi alikataa
kumpeleka hospitalini akidai atapona, ndipo alipoamua kuwafuata ndugu zake na
kumlazimisha amchukue ili akapatiwe matibabu.
“Mwanangu amelazwa Muhimbili
mara tatu lakini baba yake haonekani na huwa hachangii na kuniachia peke yangu
nikimuuguza.”
Alisema
kutokana na kukosa mtu wa kumsaidia kumhudumia kijana huyo, analazimika
kutombadilisha nguo zilizochafuka kwa haja ndogo na kubwa jambo ambalo
limemfanya awe anatoa harufu kali.
NIPASHE
Wafuasi 11 wa Chama cha Wananchi (CUF) wamevamiwa na kujeruhiwa na watu wasiojulikana
wakati wakitokea katika mkutano wa hadhara wa chama hicho.
Tukio hilo lilitokea juzi jioni eneo la Fuoni Jitimai, wakati wakirudi nyumbani baada ya
mkutano huo, uliofanyika Makunduchi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kusini Unguja, Juma Sadi, alisema watu
wasiojulikana waliwajeruhi wafuasi hao, ambao walikuwa katika gari na majeruhi
hao kukimbizwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na baadhi yao wamepewa ruhusa na
wengine wamelazwa.
Kamanda Sadi alisema Jeshi la Polisi linaendelea kufanya uchunguzi
ili kuwatia mbaroni waliohusika.
Wakati huo huo, Mbunge wa Mtambile (CUF), Masoud Abdallah Salim, jana alilitaka Bunge lijadili kwa
dharura hali ya amani visiwani Zanzibar kwa maelezo kuwa wanachama wa CUF,
wamepigwa na kujeruhiwa.
Alisema kupigwa kwa wafuasi na wanachama wa CUF kunahatarisha
amani visiwani humo na Tanzania kwa ujumla hivyo, akaliomba Bunge lijadili hali
hiyo.
Akijibu mwongozo huo, Spika wa Bunge, Anne
Makinda, alimtaka aandike hoja yake na aiwasilishe kwa Katibu
wa Bunge kwa njia ya maandishi.
NIPASHE
Mke wa Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, Josephine Mushumbusi, jana alitoa ushahidi katika Kituo
Kikuu cha Polisi jijini Dar es Salaam, kuhusiana na tuhuma zinazomkabili Khalid
Kagenzi, za kutaka kumdhuru mumewe.
Kutokana na hatua hiyo ya Mushumbusi, Dk. Slaa alisema tayari
wamefunga ushahidi kwa upande wake. Mushumbusi ambaye aliongozana na mumewe,
Dk. Slaa walifika katika kituo hicho saa 4:00 asubuhi na kutoka saa 7:25
mchana.
Akizungumza na waandishi wa habari baadaye, Dk. Slaa alisema
alimsindikiza mkewe kituoni hapo kutoa maelezo akiwa shahidi yake.
“Leo mke wangu alikuja kutoa ushahidi. Na maelezo yote aliyoyatoa
yameandikwa. Ameyapitia na mimi nimeyapitia.
Hivyo, kwa upande wangu ushahidi
nimekamilisha. Imebaki kwao tu kwa hatua zaidi pamoja na faili letu kupelekwa
kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP),” alisema Dk. Slaa.
Aliongeza: “Ninaomba ieleweke kwamba mke
wangu ni shahidi na siyo mtuhumiwa kama ambavyo nimekwisha kueleza. Naomba
msipotoshe kama ilivyotokea awali.”
Kwa upande wake, Mushumbuzi alisema wakati tukio linatokea,
alishindwa kutoa ushahidi alipoitwa na Jeshi la Polisi kwa sababu alikuwa
safarini, lakini baada ya kurudi alitoa taarifa kwa jeshi hilo.
“Wakati tukio linatokea,
niliitwa kutoa ushahidi wangu, lakini sikufanya hivyo kwa sababu nilikuwa
safari. Niliporudi niliwaambia, kwa hiyo wakaniambia nije leo,” Mushumbusi.
Aliongeza: “Maelezo ambayo nimeyatoa ni yale yale niliyosema
kwenye vyombo vya habari. Kwa hiyo yameandikwa na nimeyapitia nikajiridhisha.”
Awali, akizungumza na waandishi wa habari juu ya wito wa mke wa
Dk. Slaa, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova,
alisema hakuwa na taarifa na jambo hilo na kwamba suala hilo linawezekana
kwa kuwa ni utaratibu wa kawaida wa utendaji kazi kwa jeshi hilo.
“Sina taarifa juu ya jambo hilo.
Lakini hilo ni jambo la kawaida. Siyo jambo kubwa sana na ni utaratibu wa
kawaida wa utendaji kazi wa polisi. Na kama amekuja kuhojiwa ni wito, ambao
anaweza kuitwa mtu mwingine yeyote,” Kova.
Katika maelezo yake kwa vyombo vya habari, Mushumbusi alidai
alibaini njama za Kagenzi ambaye alikuwa mlinzi wa Dk. Slaa, kutaka kumuua
mumewe baada kukutwa na msaidizi wake wa ndani akiwa katika meza ya chakula,
ambayo hutumika kwa ajili ya kuandalia chai ya mumewe japokuwa haikuwa kawaida
yake kunywa chai katika meza hiyo.
Alisema hata hivyo, baada ya kukutwa na msaidizi wake wa kazi za
ndani, Kagenzi alishtuka na kumwaga chai na hata alipoulizwa sababu za kufanya
hivyo, hakutoa sababu za msingi.
Taarifa za awali za Kagenzi kutaka kumdhuru Dk. Slaa
zilitolewa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Mabere Marando, mbele ya
waandishi wa habari, ambaye alieleza kuwa amekuwa akitumiwa na maofisa 22
wa vyombo vya usalama katika miaka miwili iliyopita kufanya mipango hiyo dhidi
ya chama hicho.
Alidai Kagenzi amekuwa akitumiwa na maofisa usalama wa vyombo
hivyo kupata taarifa nyingi za Chadema na kuziwasilisha kwa Chama Cha Mapinduzi
(CCM).
NIPASHE
Rais Jakaya Kikwete ametunukiwa tuzo kubwa zaidi zinazotolewa na
Umoja wa Vijana wa Afrika, kwa kutambua uongozi bora na mchango wake katika
kuendeleza vijana.
Tuzo hiyo iitwayo “The African Youth Peace Award”, hutolewa
na umoja huo kwa wakuu wa nchi na viongozi wa Afrika, ambao wamethibitika
kuchangia kwa kiasi kikubwa ustawi wa Waafrika.
Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, ilisema jana kuwa ,
Rais Kikwete alikabidhiwa tuzo hiyo na Rais wa Umoja huo, Francine Muyumba, wa
Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC).
Alikabidhiwa tuzo hiyo aliposimama kwa dakika chache kuwasalimia
vijana wanaohudhuria mkutano wa tatu wa viongozi vijana wa Afrika na China,
mkoani Arusha.
Muyumba alimweleza Rais Kikwete kama kiongozi mfano wa kuigwa kwa
mchango wake katika kuwatambua na kuwaendeleza vijana katika nafasi za uongozi.
Rais Kikwete alikutana kwa mazungumzo na Mwenyekiti wa Umoja wa
Afrika (AU), ambaye pia ni Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe, aliyekuwa jijini
Arusha kufungua mkutano huo.
Alimshukuru Rais Mugabe kwa kukubali mwaliko wake wa kutembelea
Tanzania ili kufungua mkutano huo.
Rais Kikwete pia alikutana kwa mazungumzo na Makamu Mwenyekiti wa
Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China, Wang Jiariu, ambaye ndiye
kiongozi wa msafara wa vijana kutoka China kwa ajili ya mkutano huo.
HABARI LEO
Wizara ya Nishati na Madini iko kwenye mchakato wa kukamilisha
uandaaji wa sheria tatu, zitakazowasilishwa bungeni wakati wowote, zenye lengo
la kuweka uwazi katika maeneo yote yanayohusu mikataba ya uchimbaji wa madini
na gesi.
Aidha, wizara hiyo imetangaza kugunduliwa kwa gesi asilia ya futi
za ujazo trilioni 1.0 hadi 1.8 katika kisima cha Mdalasini 1 mkoani Mtwara.
Ugunduzi huo unaongeza kiwango cha gesi asilia iliyopatikana kwenye kitalu
namba mbili na kufikia futi za ujazo trilioni 22.
Unafanya gesi asilia iliyopatikana nchini hadi sasa kufikia futi
za ujazo trilioni 55.08.
Akizungumza mjini hapa, Waziri wa Nishati na Madini,
George Simbachawene alitaja sheria zinazofanyiwa kazi kwa sasa ni ya uchimbaji,
usambazaji na utafutaji.
Sheria nyingine ni ya Uwazi na Uwajibikaji katika
masuala ya madini na inayofanyiwa marekebisho ni Sheria ya Petroli ya mwaka
1984.
Alisema sheria hizo zote zina lengo la kuhakikisha kila kitu
kuhusu madini kuanzia uchimbaji, utafutaji wake na mikataba kinakuwa wazi,
tofauti na ilivyo sasa ambapo kwa mujibu wa Sheria ya Petroli mikataba yote ni
ya siri.
“Najua watu wamekuwa wakipigia
kelele uwazi wa mikataba, sasa hili tunataka tulifanyie marekebisho ya
kisheria, kwa kuwa mimi kama waziri nimefungwa mikono siwezi kuweka hadharani kutokana
na sheria kukataza hilo, nikiiweka wazi kampuni hizi zina uwezo wa kunishitaki
na nitalipa mamilioni ya fedha,” Simbachawene.
Alisema ili kuendana na wakati na kasi ya ugunduzi wa gesi asilia
nchini na nchi nyingine za jirani, ikiwa ni pamoja na ushindani wa soko la
gesi, wizara hiyo inataka kuomba Bunge lifanyie kazi haraka sheria hizo,
ikiwezekana kabla ya Bunge la bajeti.
“Wenzetu Msumbiji wamegundua
gesi nyingi kuliko sisi, sasa tukiendelea kusuasua na jambo hili la sheria kwa
mwaka mmoja pekee, tutaachwa sana nyuma, tunataka suala hili liishe muda si
mrefu,” alisisitiza.
Hata hivyo, Simbachawene alisema si kweli kwamba mikataba iliyopo
ilikuwa na usiri mkubwa, kama ilivyodhaniwa kwani mingi, ilikuwa ikiwasilishwa
kwenye Kamati za Bunge na kupitiwa na wabunge.
Akizungumzia ugunduzi mpya wa gesi asilia, waziri huyo alisema
kisima kilichogunduliwa gesi hiyo cha Mdalasini 1, kimechimbwa katika urefu wa
meta za maji ya bahari 2,296 Kusini mwa Kitalu namba mbili chenye miamba yenye
umri miaka 66 hadi 145.
HABARI LEO
Utekelezwaji wa adhabu ya kifo kwa watu 10 waliohukumiwa kunyongwa
hadi kufa, kutokana na kuhusika katika mauaji ya watu wenye ulemavu (albino),
unasubiri saini ya Rais Jakaya
Kikwete.
Hayo yalibainishwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima, wakati
akijibu swali la nyongeza la mbunge wa Lindi Mjini, Salum Barwany (CUF).
Katika swali lake, Barwany, alitaka kufahamu ni lini utekelezaji
wa hukumu ya kifo kwa watu 10, waliokwisha hukumiwa adhabu ya kifo na Mahakama
kutokana na kuhusika na mauaji ya albino, itatekelezwa. Silima, alisema kwa
mujibu wa taratibu za kisheria, adhabu ya kifo inapotolewa, utekelezaji wake
husubiri saini ya Rais.
“Sijapata taarifa kama hukumu
hizi tayari Rais ameziwekea saini ili zitekelezwe ila nitafuatilia ili Sheria
ichukue mkondo wake,” alisema.
Katika swali la msingi la mbunge huyo, alitaka kufahamu hadi sasa
kuna kesi ngapi za mauaji ya walemavu wa ngozi zilizokwishatolewa hukumu baada
ya kufikishwa mahakamani na kesi ngapi bado zinasubiri huku na ni kwanini
zimechelewa kutolewa maamuzi.
Waziri alisema kati ya mwaka 2006 na 2015, jumla ya matukio 56 ya
uhalifu dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi yaliripotiwa nchini na kati ya
matukio hayo 41 yalihusisha vifo 43, matukio 13 yahusisha majeruhi na mawili ya
kupotea watu hao albino.
Alisema kesi 46 kati ya matukio 56 zilifikishwa mahakamani na kesi
10 zenye watuhumiwa 12 zilitolewa hukumu ya kifo na kesi 10 badi ziko chini ya
upelelezi.
Aidha kesi 26 watuhumiwa wake waliachiwa huru kwa kukosa ushahidi.
Silima alisema pia kesi 10 bado zinaendelea kusikilizwa mahakamani na ziko
katika hatua mbalimbali.
“Kuhusu kuchelewa kwa hukumu au
upelelezi wa baadhi ya kesi, kunachangiwa na sababu mbalimbali kama vile
matokeo ya uchunguzi wa vinasaba (DNA) kutoka mamlaka za uchunguzi na mashahidi
kutopatikana kwa urahisi na wakati”.
Katika swali la nyongeza la mbunge wa Viti Maalum, Al Shamaar Kwegyir (CCM), alitaka kujua Serikali imefikia
wapi katika kumtafuta mtoto Pendo
Emmanuel mwenye
ulemavu wa ngozi mkazi wa Kwimba, aliyechukuliwa mikononi mwa mama yake mzazi
na mpaka sasa hajulikani alipo.
Akijibu swali hilo, Silima alikiri kuwa mpaka sasa Polisi
inamtafuta na katika upelelezi unaoendelea jumla ya watu 14 wanashikiliwa na
kuhojiwa kwa kuhusika kwa namna moja ama nyingine na tukio hilo, akiwemo.
Source:-Millardayo.
Pata Picha, Habari za Kisiasa, Kijamii, Kiuchumi na Michezo kila stori inayonifikia wakati wowote ukijiunga na mimi kwa kubonyeza…..FACEBOOK , TWITTER , INSTAGRAM , Pia tutumie tukio la Picha kwa WhatsApp +255789925630.
|
No comments:
Post a Comment