Ochieng
kulia na Akuffo kushoto
|
Hapo jana zoezi la kuwasilisha usajili wa wachezaji
wa klabu za Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara na timu za vijana ukifikia tamati,
mabingwa wa ligi hiyo Simba, wamefunga usajili wao kwa kuwasajili wachezaji
wawili wa kimataifa Mghana Danniel Akuffo na Mkenya Pascal Ochieng.
Aidha, Simba
inatarajia kupokea mchezaji wa kimataifa kutoka nchini Mali Abdul Azizi ambaye ataletwa na wakala wa
wachezaji Vaier St. Claire na Simba itaangalia jinsi gani itamfanyia mchezaji huyo
kwani zoezi limeshafungwa.
Simba ambayo
jana iliwatambulisha wachezaji hao wapya kwa waandishi wa habari, imewasilisha
pia majina ya Emmanuel Okwi, Mussa Mudde na Felix Mumba Sunzu hivyo kufikisha
wachezaji watano wa kimataifa wanaohitajika kusajiliwa kwa mujibu wa kanuni.
Ofisa habari
wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema jana kwamba, wamemsajili Akuffo kwa mkataba
wa mwaka mmoja baada ya wakala wake kuwaeleza kuwa nyota huyo yupo katika
mpango wa kwenda Ulaya kucheza soka la kulipwa mwakani.
Alisema wachezaji
hao wanatarajiwa kushuka dimbani na kikosi cha Simba kitakachokwaana na AFC
Leopards keshokutwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha, pia
watakuwapo katika mechi ya Ngao ya Hisani dhidi ya Azam FC itakayopigwa Uwanja
wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Alisema
mbali na hao, katika usajili wao wamewasilisha majina ya wachezaji wake Kelvin
Yondan aliyesajiliwa Yanga na Ramadhan Chombo ‘Redondo’ waliomsajili kutoka
Azam na kusema kuwa suala lao litamalizwa na Kamati ya Sheria, Katiba na Hadhi
za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Mashabiki wa Simba |
Yondan
ambaye alizua utata baada ya kumwaga wino kuichezea Yanga, huku Simba ikidai
kuwa bado ina mkataba naye, jina lake pia limeorodheshwa na watani zao hao
katika usajili wa wachezaji watakaoichezea timu hiyo katika msimu wa 20012/13.
Wachezaji
wengine waliojumuishwa kwenye usajili wa Simba ni pamoja na Juma Kaseja, Mwinyi
Kazimoto, Amri Kiemba, Nassoro Said Cholo, Amir Maftah, Juma Nyoso, Uhuru
Seleman, Haruna Moshi ‘Boban’, Paul Ngalema na Abdallah Juma.
Wengine ni
Hamad Waziri Mwinyimani, Salum Kinje, Mrisho Ngassa, Haruna Shamte, Jonas
Mkude, Edward Christopher, Shomary Kapombe, Haruni A. Chanongo, Omary Seseme,
Hassan Kondo na Kiggi Makasi.
No comments:
Post a Comment