Kasi ya
wananchi kujiweka katika hatari ya kupata magonjwa ya kansa imeendelea kupamba
moto jijini Dar es Salaam na kwingineko nchini licha ya jitihada kubwa
zinazoendelea kufanywa kila uchao katika kudhibiti hali hiyo, imefahamika.
Wananchi
hao, hasa kina mama na wasanii wa fani mbalimbali wakiwamo wa filamu, muziki wa
dansi na bongofleva, wamekuwa vinara wa kununua vipodozi vyenye viambata vya
sumu na kujipaka mwilini kwa nia ya kujiongezea urembo na utanashati lakini
bila kujua kuwa wanajiweka katika hatari ya kupata magonjwa ya kansa, hasa ya
ngozi na ini.
Uchunguzi
uliofanywa na NIPASHE kuanzia wiki iliyopita umebaini kuwa watu wanaojiweka
katika hatari hiyo hununua vipodozi hivyo kwa kati ya Sh. 750 hadi Sh. 7,000
kwa chupa kutegemeana na ujazo na pia aina ya kipodozi na chapa yake (brand)
huku mkorogo wenye mchanganyiko wa vipodozi hivyo, maarufu kama 'manjano' au
'kijiko special' ukiuzwa kwa Sh. 1,000 kwa kipimo cha kijiko kimoja kikubwa cha
chai.
Kadhalika,
imebainika kuwapo kwa utitiri wa vipodozi vyenye sumu katika maduka na masoko
mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam na kwingineko nchini huku wauzaji na wateja
wao wakionekana kupuuza au kutofahamu lolote juu ya ukweli kwamba bidhaa hizo
zinahatarisha afya yao na vilevile wanajiweka katika hatari ya kukumbana na
mkono wa dola kwani kuuza au kutumia bidhaa hizo kunakiuka sheria za nchi.
Katika
maeneo kama ya masoko ya Tandika, Buguruni, Manzese, Magomeni, eneo la Mbagala Rangi
Tatu na kwingineko nchini, vipodozi hivyo huuzwa bila kificho na baadhi huuzwa
kwa kuwekwa kwenye viroba na kupangwa ardhini huku vikipigiwa debe na wauzaji
kama ilivyo kwa biashara ya nguo za mitumba.
Katika
tovuti yao (http://www.tfda.or.tz) na pia kupitia kampeni mbalimbali za
kuelimisha umma, Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) imekuwa ikivitaja
viambata vyenye sumu kwenye vipodozi kuwa ni pamoja ni Bithionol,
Hexachlorophene, Mercury, Vinyl chloride, Zirconium, Halogenated salicylanilides
(di-, tri- metabromsalan and tetrachlorosalicynilide), Chloroquinone, Steroids,
Chloroform, Chlofluorocarbon na Methyelene chloride.
Aidha, TFDA
imetaja vipodozi zaidi ya 100 vyenye viambata vyenye sumu. Hata hivyo,
uchunguzi umebaini kuwa baadhi ya vipodozi hivyo ndivyo vilivyojaa sokoni na
kwenye baadhi ya maduka, vikiwamo vya Mekako, Rico, Princess Cream, Butone
Cream, Extra Clear Cream, Viva Super Lemon Cream, Ultra Skin Tone Cream.
Vingine ni Clere Extra, Top Lemon, Diproson, sabuni aina ya Jaribu, Riki, Amira
na pia cream kama Movate, Demovate na Oranvate.
HATARI
ILIYOPO.
Vipodozi
hivi vyenye viambata vya sumu husababisha pia ngozi kuharibika na kuifanya kuwa
nyepesi, hivyo kusababisha miale hatari ya jua (UV-B) kupenya kirahisi kwenye
ngozi na kusababisha kansa.
Kaimu Mkuu
wa Idara ya Kuzuia Udhibiti wa Kansa katika Hospitali ya Ocean Road jijini Dar
es Salaam, Dk. Maguhwa Stephano, ameiambia NIPASHE kuwa vipodozi vyenye
viambata vya sumu vina madhara makubwa na wananchi wanapaswa kujua kuwa kuvitumia
ni kujihatarishia uhai kwani magonjwa ya kansa ni ya hatari na kutibu kwake
huligharimu taifa fedha nyingi.
Kwa mujibu
wa Dk. Maguhwa, gharama za kuwatibu wagonjwa wa kansa ni kubwa na hivyo
serikali hufanya kazi ya ziada ya kutenga kiasi kikubwa cha fedha katika kila
mwaka ili kuwatibu wananchi wake; rasilimali ambayo pengine inaweza kutumiwa
kwa shughuli nyingine za maendeleo ikiwa wananchi watajiepusha kutumia vipodozi
hatari wanavyovinunua kwa fedha kidogo lakini wakijiweka katika hatari kubwa
kiafya.
Anasema tiba
kubwa wanazotoa kwa wagonjwa wa kansa huwa ni za aina tatu, ambazo ni kwa
kutumia mionzi, drip na pia kwa dawa maalum (chemotherapy). Na matibabu yote
hayo huhitaji gharama kwa kila mgonjwa.
"Kwa
kawaida, gharama ya kipimo cha wagonjwa wa kansa (Biops) ni Sh. 50,000 hadi
80,000 kulingana na mahala anakokwenda mgonjwa.
Gharama
nyingine ni mionzi huwa kati ya Sh. 800,000 hadi 1,200,000. Katika hali ya
kawaida, wastani wa gharama za kuwatibu wagonjwa wa kansa ya ngozi kwa mwaka
huwa ni zaidi ya 2,000,000. Isipokuwa, lazima ifahamike kuwa gharama kuwa juu
au chini hutegemeana na stage ya ugonjwa wenyewe na mahala ulipo katika mwili,”
anasema.
Kwa mujibu
wa Shirika la Afya Duniani (WHO), watu takriban milioni 3 hupata kansa kila
mwaka, huku milioni moja kati yao wakiwa ni watu wanaopata saratani ya ngozi.
TFDA WANENA.
Afisa
Uhusiano wa TFDA, Gaudencia Simwanza anasema vipodozi vya sumu ni janga kubwa
linalopaswa kudhibitiwa kwa ushirikiano wa pamoja baina ya mamlaka yao na wadau
wengine, hasa wananchi wenyewe.
Anasema
tafiti mbalimbali zimethibitisha kuwa watumiaji wa vipodozi vyenye sumu
wanajiweka katika hatari kubwa ya kupata maradhi ya kansa na pia athari
nyingine nyingi za kiafya.
Anataja
madhara mengine mbali na kansa ya ngozi kuwa ni kansa ya ini, kina mama
wajawazito kuzaa watoto wenye mtindio wa ubongo, shinikizo la damu na pia
uwezekano wa kina mama kuota ndevu pindi wanapotumia vipodozi vyenye sumu kwa
muda mrefu.
Kuhusiana na
udhibiti, Simwanza anasema kuwa mamlaka yao hujitahidi kufanya ukaguzi wa
kustukiza kila mara kwenye maduka na maeneo mengine yauzayo vipodozi,
kushirikiana na mamlaka nyingine kama jeshi la polisi katika kufanya ukaguzi
maeneo ya mpakani mwa nchi na pia kufanya kampeni mbalimbali za kuelimisha
umma.
Anaongeza
kuwa kasi ya uingizaji wa vipodozi vyenye sumu nchini ni kubwa lakini
wameendelea kufanya jitihada za kutosha za kudhibiti. Hadi kufikia sasa,
wamekuwa wakikamata na kuteketeza wastani wa tani 54 za vipodozi vyenye
viambata hivyo kila mwaka, thamani yake ikiwa ni takriban Sh. milioni 354.
Anasema
Sheria ya Chakula, Dawa na Vipodozi ya mwaka 2014 inawapa mamlaka ya
kukamata na kuteketeza vipodozi vyenye viambata vya sumu.-"Sheria inapiga
marufuku viambato vyenye sumu na vipodozi vyenye viambato viletavyo madhara...
ni katika vifungu 87(i) na 90," anasema Simwanza.
Hata hivyo,
anasema kuna changamoto kadhaa za kisheria kwani kadri inavyoonekana sasa,
adhabu kwa wahusika zinaonekana zimepitwa na wakati na kwamba hazitishi
wahalifu kiasi cha kutosha. "Watuhumiwa wanaokutwa na vipodozi
visivyofaa hunyang'anywa vipodozi hivyo na hulipia gharama ya kuviteketeza.
Sambamba na hilo, wengine hufikishwa mahakamani. Kesi 10 zilifikishwa
mahakamani."
Anasema
matumizi ya vipodozi visivyofaa yatakoma mara moja pindi jamii ikibadilika na
kwamba, TFDA inaamini kwa kuendelea kutoa elimu, lengo hilo litatimizwa
kwani kidogokidogo jamii itakuwa ikibadilijka.
KWINGINEKO
AFRIKA.
Katika
makala kuhusiana na vipodozi vyenye vimabata vya sumu iliyochapishwa na mtandao
wa BBC Januari 1, 2013, ilielezwa kuwa matumizi ya vipodozi hivyo ni janga
kubwa barani Afrika. Kwa mfano, madaktari wa ngazi katika hospitali moja jijini
Dakar, Senegal walikaririwa wakisema kuwa hupokea takriban kina mama 200 kila wiki
wanaokuwa wameathiriwa vibaya ngozi zao baada ya kutumia vipodozi vyenye sumu
kwa nia ya kubadili rangi za ngozi zao.
Mtandao wa
voices in bioethics unakariri taarifa za utafiti wa Shirika la Afya Duniani
(WHO) unaoonyesha kuwa nchi za Mali, Nigeria, Senegal, Afrika Kusini na Togo
ndizo zinazoongoza kwa matumizi ya vipodozi vyenye viambata vya sumu barani
Afrika. Katika utafiti huo, inaelezwa kuwa wanawake ndiyo vinara kwani kila
uchao, asilimia 77 ya wanawake wa Nigeria hutumia vipodozi hivyo, wakifuatiwa
na Togo (59), Afrika Kusini (35), Senegal (27) na Mali (25).
Chanzo:-
NIPASHE
|
No comments:
Post a Comment