NGUVU YA HOJA TANZANIA:-Bunge kuanza kesho jANUARI 27,2015 Dodoma. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Monday, January 26, 2015

NGUVU YA HOJA TANZANIA:-Bunge kuanza kesho jANUARI 27,2015 Dodoma.

Pichani ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Mcheche Masaju.

 Mkutano wa 18 wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania unatarajia kuanza kesho Januari 27,2015 mjini Dodoma hadi Februari 7, mwaka huu.

Mkutano huo utaambatana na kuapishwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG),  George Mcheche Masaju, baada ya kuteuliwa na Rais Jakaya Kikwete hivi karibuni baada ya kujiuzulu kwa Jaji Frederick Werema kutokana na kuhusishwa na kashfa ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 300 kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow iliyokuwa Benki Kuu Tanzania (BoT).

Katika mkutano huo, Wabunge watajadili miswada mitatu ya serikali ambayo ni pamoja na wa sheria ya usimamizi wa kodi wa mwaka 2014, ambao utapigiwa kura tu, wa sheria ya takwimu wa mwaka 2013 ambao utasomwa kwa mara ya tatu na ule  wa marekebisho ya sheria mbalimbali namba 2 wa mwaka 2014.

Pamoja na miswada hiyo, Bunge pia litajadili taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali zilizowasilishwa katika mkutano wa 15 wa Bunge kuhusu hesabu zilizokaguliwa za serikali Kuu, serikali za mitaa na mashirika ya umma kwa mwaka 2012/2013 na serikali kutakiwa kuzitolea majibu kwa baadhi ya hoja.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Idara ya Habari, Elimu kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa kutoka  Ofisi Ndogo za Bunge, katika mkutano  huo, kamati za Bunge pia zitapewa nafasi ya kuwasilisha taarifa za mwaka ikiwamo Kamati Teule ya Bunge iliyoundwa kuchunguza na kuchambua sera  zinazohusu ardhi, kilimo, mifugo, maji na uwekezaji ili kubaini kasoro zilizomo katika matumizi ya ardhi.

Vilevile maswali ya kawaida 125 yanatarajiwa kuulizwa na kujibiwa, maswali 15 kwa siku na 10 kwa Alhamisi. 

Mkutano wa 19 wa Bunge unatarajia kufanyika  katikati ya Machi hadi mwanzoni mwa Aprili huku ule wa 20 wa Bunge la Bajeti mwanzoni  Mei hadi  Juni 30, mwaka huu.

UNGANANASI KATIKA  FACEBOOK , TWITTER , INSTAGRAM , Pia tutumie tukio la Picha kwa WhatsApp +255789925630.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad