Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 27 Septemba, 2016 amepokea msaada
wa Shilingi Milioni 545 kutoka kwa Waziri Mkuu wa India Mhe. Narendra Modi kwa
ajili ya kusaidia wananchi wa Mkoa wa Kagera waliopatwa na maafa ya tetemeko la
ardhi lililotokea tarehe 10 Septemba, 2016.
Hundi ya fedha hizo imekabidhiwa leo
Ikulu Jijini Dar es Salaam na Balozi wa India hapa nchini Mhe. Sandeep Arya na
baadaye Rais Magufuli akaikabidhi kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa.
Katika barua yake kwa Rais Magufuli
iliyosomwa na Balozi Sandeep Arya, Waziri Mkuu wa India Mhe. Narendra Modi
amesema Serikali na Wananchi wa India wamepokea kwa masikitiko makubwa taarifa
za kutokea kwa maafa hayo yaliyosababisha vifo vya watu na uharibifu wa mali.
"Tunaziombea amani na uvumilivu
familia zote zilizopatwa na madhara na pia tunapenda kuwahakikishia kuwa tupo
pamoja na marafiki zetu Serikali ya Tanzania katika kipindi hiki kigumu"
amesema Waziri Mkuu Modi.
Kwa Upande wake Rais Magufuli
amemshukuru Waziri Mkuu wa India Mhe. Narendra Modi na Serikali yake kwa kutoa
mchango huo na kutuma salamu za rambirambi, na amesema Serikali yake imeguswa
na moyo wa upendo waliounesha.
"Mhe. Balozi Sandeep Arya naomba
unifikishie shukrani zangu za dhati kwa Waziri Mkuu Mhe. Narendra Modi, mwambie
kwa niaba ya Serikali yangu tunamshukuru sana kwa kutoa msaada huu muhimu kwa
ajili ya Watanzania wenzetu waliopatwa na maafa kule Kagera.
"Mwambie ameonesha moyo wa
upendo na ushirikiano kwetu na tumefarijika kwamba marafiki zetu mmeguswa kwa
namna ya kipekee na tatizo lililoipata nchi yetu" amesema Rais Magufuli.
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais,
IKULU
Dar es Salaam
27 Septemba, 2016
|
No comments:
Post a Comment