Mamba katika Hifadhi ya
Taifa ya Kisiwa cha Rubondo Mkoani Geita.
|
Moja ya Fukwe katika
Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo.
|
Huduma za malazi katika
Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo.
|
Huduma bora ya vyumba
inapatikana katika Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo.
|
Huduma za usafiri wa
boti zinapatikana katika Hifadhi ya Taifa ya Rubondo.
NA HAMZA TEMBA - WIZARA
YA MALIASILI NA UTALII
____________________________________________________________
Naibu Waziri wa
Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani ameitaka Mamlaka ya Hifadhi za Taifa
Tanzania (TANAPA) kuzishirikisha jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi hapa
nchini kutambua umuhimu wa kuhifadhi maeneo hayo ili kutoa ulinzi shirikishi
katika kupambana na Ujangili.
Eng. Makani amesema
hayo jana wakati akizungumza na viongozi pamoja na watumishi wa Mamlaka hiyo
akiwa ziarani Mkoani Geita katika Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo.
“Wananchi waoishi
jirani na maeneo haya ya hifadhi ni muhimu wakaelimishwa juu ya faida za
uhifadhi kiikolojia na kiuchumi kwenye maisha yao ambapo itawapa msukumo wa
kuyatunza na kuyalinda” Alisema Eng. Makani.
Aliongeza kuwa vita
dhidi ya Ujangili hapa nchini haiwezi kufanikiwa kirahisi iwapo jamii
inayozunguka maeneo ya Hifadhi haitatoa ushirikiano kwa Serikali katika kulinda
na kuhifadhi Maliasili zilizopo.
“Pamoja na mbinu
nyingine, washirikisheni wananchi watusaidie kupambana na ujangili ili fedha ambayo
ingetumiwa na Serikali kwa kazi hiyo itumike kuendeleza hifadhi zetu pamoja na
kutoa huduma nyingine za kijamii” Alisema Eng. Makani.
Akizungumzia faida za
uhifadhi kiuchumi hapa nchini alisema kuwa, Sekta ya utalii ndio sekta pekee
inayoongoza kwa kuliingizia taifa mapato mengi ya nje (foreign currency) ambayo
ni asilimia 25 ya mapato yote. Sekta hiyo pia inachangia pato la taifa kwa
asilimia 17.2.
Eng. Makani aliongeza
kuwa “Serikali ya awamu ya tano ina mpango wa kuboresha sekta ya utalii ili
iweze kuiingizia zaidi mapato, katika kufanikisha hilo tumeweka mkakati wa
kuboresha ofisi zetu za utalii za Kanda ili ziweze kutangaza na kukuza zaidi
utalii wa ndani”.
Kwa upande wa hoteli
zinazotoa huduma ya kitalii hapa nchini alisema kuwa ifikapo mwezi Septemba
mwaka huu, Serikali itaanza rasmi zoezi la kuorodhesha hoteli zote zinazotoa
huduma hiyo na kuzipanga kwenye makundi ya ubora ambapo zile zitakazoonekana
hazina hadhi kabisa zitaondolewa katika mtandao wa kutoa huduma hiyo.
Alisema
zoezi hilo litaboresha huduma za kitalii nchini na kusaidia watalii kufikia
hoteli wanazozihitaji na kupata huduma stahiki .
Katika kushirikisha
sekta binafsi kwenye kukuza utalii nchini, amewaomba watoa huduma za ndege
kuangalia upya viwango vya gharama zao za usafiri ili wananchi wengi zaidi
waweze kumudu na kunufaika na huduma hiyo.
Wakati huo huo aliwaasa
watumishi wa Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo kufanya kazi kwa bidii,
kuwa na maadili mema na uadilifu kazini. Aliwataka pia kuwa mstari wa mbele
kupiga vita ujangili, kuboresha ukusanyaji wa mapato na kushirikisha wananchi
kwenye uhifadhi.
Hapo awali akiwasilisha
taarifa ya hifadhi hiyo kwa Naibu Waziri wa Maliasili, Eng. Ramo Makani, Mkuu
wa Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo, Massana Mwishawa alisema kuwa
changamoto kubwa inayoikabili hifadhi hiyo ni ujangili na upatikanaji mdogo wa mapato
ambao hauwiani na mahitaji ya hifadhi hiyo.
Kwa upande wake Mbunge
wa Jimbo la Geita Vijijini, Joseph Luiza Kasheku maarufu kama Msukuma,
alimuomba Naibu Waziri huyo wa Maliasili kuboresha Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa
cha Rubondo ambayo ipo Jimboni kwake iweze kupata mapato ya kutosha na
kujiendesha yenyewe. Hifadhi hiyo kwa sasa inategemea mapato kutoka kwenye
hifadhi nyingine kujiendesha.
Hifadhi ya Taifa ya
Kisiwa cha Rubondo iliyopo Mkoani Geita ni moja ya sehemu pekee na muhimu
katika uzalishaji wa mazalia ya samaki katika ziwa Victoria. Sehemu nyingine ni
Hifadhi ya Kisiwa cha Saanane iliyopo Mkoani Mwanza. Hifadhi hizi zina umuhimu
mkubwa katika upatikanaji wa samaki katika Ziwa Victoria.KWA PICHA ZAIDI/HABARI BOFYA HAPA.
|
No comments:
Post a Comment