Waziri Mkuu
wa Tanzania, Mizengo Pinda.
Serikali
imesema kasoro zilizotokea kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa jana katika
maeneo mbalimbali ya Tanzania hazikuathiri uchaguzi huo kwa sababu maeneo mengi
ulifanyika kwa ufanisi.
Hayo yalielezwa jana na Mkurugenzi wa Uchaguzi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Khalist Luanda, wakati akizungumza na
NIPASHE kuhusu kasoro hizo.
Luanda alisema kasoro hizo zilizosababisha baadhi ya maeneo kuahirisha
uchaguzi, haziepukiki kutokana na ukubwa wa uchaguzi huo, ambao aliutofautisha
na ule wa madiwani, wabunge na urais.
“Kutokana na ukubwa wa uchaguzi, nathubutu kusema kasoro zilizojitokeza ni
vigumu kuziepuka, hapa tunazungumzia vitongoji elfu 64, mitaa elfu 30 na vijiji
elfu 13 tofauti uchaguzi wa wabunge takribani 300,” alieleza Luanda.
Kwa mujibu wa Luanda, Wilaya nzima ya Kaliua mkoani Tabora, uchaguzi
uliahirishwa kwa sababu mbalimbali mpaka Jumapili ijayo.
Alisema hatua ya wasimamizi wa uchaguzi kuahirisha chaguzi kwenye maeneo yao,
ni kwa mujibu wa kanuni ambazo zinaelekeza ufanyike tena, ndani ya muda
usiyozidi siku saba.
Alitaja maeneo mengine ambayo kwa wakati huo alikuwa na taarifa kwamba uchaguzi
uliahirishwa, kuwa ni Kata ya Dodoma Makulu, Mtaa wa Njedengwa – West.
Maeneo mengine yaliyokumbwa na kasoro mbalimbali kiasi cha kusababisha uchaguzi
huo kuahirishwa, yalitajwa na Luanda kuwa ni pamoja na baadhi ya maeneo
wilayani Ilala, jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, hakueleza sababu za kucheleweshwa kwa vifaa wakati wiki iliyopita
alisema maandalizi yalikuwa yamekamilika kwa asilimia 100.
Chanzo:-NIPASHE
|
No comments:
Post a Comment