Shirika la afya duniani, WHO limearifu kuwa liko mbioni kufanya majaribio
ya chanjo dhidi ya ugonjwa wa Ebola, ambao umeripotiwa kuua takribani watu
4,500 huku nchi za Afrika Magharibi zikiripotiwa kuathirika zaidi tangu
kulipuka kwa ugonjwa huo mwaka huu (2014).
Taarifa iliyoripotiwa na CNN, imesema kuwa shirika hilo
limepanga kuanza utekelezaji wa jaribio hilo mapema Januari mwaka 2015 katika
nchi za Afrika Magharibi, huku wakisisitiza kuwa chanjo zote hazina madhara kwa
afya ya binadamu, japo chanjo hiyo haitowahusu wagonjwa ambao tayari wana
maambukizi Ebola.
Mratibu wa zoezi hilo Dk. Marie Paule Kieny amesema, chanjo hiyo
itatolewa kwa mtu yoyote atakayekuwa tayari kujitolea kushiriki.
Amezitaja nchi za Mali, Uingereza na Marekani kuwa ni baadhi ya nchi
ambazo jaribio la chanjo hiyo litafanyika.
Shirika la afya limesema limeagiza wataalamu kufanya ziara Afrika
Magharibi katika nchi ambazo wananchi wake wameathirika zaidi na ugonjwa huo,
ambapo pia ziara hiyo itahusisha pia zoezi la ukaguzi wa vituo ambavyo
vitatumika kutolea huduma hiyo ya chanjo.
Iwapo chanjo hii itafanikiwa itafufua matumaini kwa watu wa Afrika ya
Magharibi ambao wameshuhudia athari kubwa zilizosababishwa na Ebola ambapo watu
zaidi ya 4,500 wameripotiwa kufariki na wengine zaidi ya 9,000 wana maambukizi
ya ugonjwa huo
|
No comments:
Post a Comment