Klabu kongwe nchini za Simba na Yanga, zimekabidhiwa
vifaa mbalimbali vyenye thamani ya sh milioni 34 kila moja kutoka kwa mdhamini
wao mkuu, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia yake ya Kilimanjaro
Premium Lager.
| George Kavishe |
Akikabidhi
vifaa hivyo katika Ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), jijini Dar es
Salaam, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro, George Kavishe, alisema, kukabidhi vifaa
hivyo ni moja ya sehemu katika mkataba baina yao na klabu hizo.
Kavishe
alisema lengo kubwa la kudhamini timu hizo ni kutokana na historia kubwa ya
klabu hizo, pamoja na kuleta ushindani wenye burudani kwa Watanzania, ambao ni
wadau wakubwa wa kunywa kinywaji hicho.
“Sisi
tunafanya kazi vema na klabu hizi, tunajisikia faraja kubwa kutokana na timu
hizi kuwa na historia kubwa hapa nchini na ushindani mkubwa katika soka na huu
ni udhamini wa nusu msimu peke yake,” alisema Kavishe.
Aidha vifaa hivyo vilivyotolewa ni pamoja na jezi, bukta, soksi, viatu, bips, nguo za
kusafiria, vikinga ugoko na mifuko.
Katika hatua
nyingine, Kavishe alisema, kuhusu mabasi ya timu hizo, wako katika hatua za
mwisho kuyakabidhi kwa wahusika, kwani tayari yamewasili hapa nchini, ambapo
kuna mambo kadhaa wanayakamilisha.
| Kaburu |
Akizungumza
kwa niaba ya klabu ya Simba, Makamu Mwenyekiti, Geofrey Nyange ‘Kaburu’,
aliwashukuru wadhamini hao kwa moyo walionao, huku akiwaahidi kuhakikisha
wanafanya vema na kushinda ili kuonesha umuhimu wa vifaa ambavyo wamewapa.
“Nawashukuru
TBL kwa kutudhamini na kuona umuhimu kwa sisi Simba bila ya kupepesa macho na
ndiyo maana hata sisi tutapigana kufa na kupona ili kuhakikisha tunavitendea
haki vifaa hivi,” alisema Kaburu.
| Louis Sendeu |
Kwa upande
wa Yanga, Ofisa Habari wake, Louis Sendeu, naye aliishukuru TBL, huku akiwaomba
kutoishia kwa Simba na Yanga, bali waziangalie na timu nyingine.
“Tunawashukuru
sana ila msiishie kwa Yanga na Simba tu, mziangalie na klabu nyingine ambazo
zinasuasua,” alisema Sendeu.
|
Ofisa Habari
wa Yanga, Louis Sendeu (kushoto) akipokea vifaa vya michezo kutoka kwa Meneja
wa Bia ya Kilimanjaro, George Kavishe.
|
Kwa mujibu
wa shirikisho la mpira wa miguu nchini Tanzania TFF,Michuano ya Ligi Kuu
kuwania ubingwa wa Tanzania Bara kwa msimu wa 2012/2013 itaanza Septemba 15
mwaka huu kwa timu zote 14 kujitupa kwenye viwanja tofauti.
Mechi za
ufunguzi zitakuwa kati ya Simba vs African Lyon (Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam), Polisi Morogoro vs Mtibwa Sugar (Jamhuri, Morogoro), Tanzania Prisons
vs Yanga (Sokoine, Mbeya), Mgambo JKT vs Coastal Union (Mkwakwani, Tanga), JKT
Ruvu vs Ruvu Shooting (Azam Complex, Dar es Salaam), Kagera Sugar vs Azam
(Kaitaba, Bukoba) na Toto Africans vs Oljoro JKT (Kirumba, Mwanza).
Mzunguko wa
kwanza (first round) utamalizika Novemba 11 mwaka huu ambapo kwenye mzunguko
huo mechi ya watani wa jadi Yanga na Simba itachezwa Oktoba 3 mwaka huu kwenye
Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ligi hiyo
itamalizika Mei 18 mwakani kwa mechi kati ya Toto Africans vs Ruvu Shooting
(Kirumba), Mgambo JKT vs African Lyon (Mkwakwani), JKT Ruvu vs Mtibwa Sugar
(Azam Complex), Tanzania Prisons vs Kagera Sugar (Sokoine), Simba vs Yanga
(Uwanja wa Taifa), Oljoro JKT vs Azam (Sheikh Amri Abeid Kaluta) na Polisi
Morogoro vs Coastal Union (Jamhuri).
Endapo Simba
na Azam hazitafanikiwa kuvuka hatua mojawapo ya michuano ya Ligi ya Mabingwa
Afrika na Kombe la Shirikisho, ratiba hiyo itafanyiwa marekebisho.






No comments:
Post a Comment