Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amepokea kwa
mshtuko na masikitiko makubwa taarifa za vifo vya Askari Polisi 8 waliouawa kwa
kushambuliwa na watu wenye silaha jana jioni tarehe 13 Aprili, 2017 katika eneo
la Jaribu Mpakani, Wilaya ya Kibiti Mkoani Pwani.
Askari Polisi
hao walikuwa wakitoka kubadilishana doria na wameshambuliwa kwa kupigwa risasi
wakiwa wanasafiri kwa gari katika barabara ya Dar es Salaam – Lindi.
Mhe. Rais
Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini
IGP-Ernest Mangu, familia za askari wote waliouawa, Askari Polisi wote na
Watanzania wote walioguswa na vifo hivyo.
“Nimeshtushwa
na nimesikitishwa sana na vifo vya askari wetu 8 ambao wamepoteza maisha wakiwa
wanalitumikia Taifa, naungana na familia za marehemu wote, Jeshi la Polisi na
Watanzania wote katika kipindi hiki kigumu cha huzuni na majonzi ya kuondokewa
na vijana wetu shupavu.
“Namuomba Mwenyezi Mungu atupe moyo wa subira,
uvumilivu na ustahimilivu” amesema Mhe. Rais Magufuli.
Aidha, Mhe.
Dkt. Magufuli amelaani tukio hilo na matukio yote ya kuwashambulia askari
polisi ambao wanafanya kazi kubwa na muhimu ya kulinda raia na mali na ametaka
Watanzania wote watoe ushirikiano katika kukomesha vitendo hivyo.
Mhe. Rais
Magufuli amewaombea marehemu wote wapumzishwe mahali pema peponi, Amina.
Gerson
Msigwa.
Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es
Salaam
14 Aprili,
2017
|
No comments:
Post a Comment