|
Meneja Mawasiliano na
Uhusiano wa Umma kutoka TFDA, Gaudensia Simwanza.
Serikali kupitia
Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) imesema hivi karibuni itaanza msako mkali wa
kuwatafuta na kuwakamata wauzaji wa dawa zinazokatazwa pamoja na vipodozi
vikali ambao wanajitangaza kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii.
Katika mahojiano na wanahabari, Meneja
Mawasiliano na Uhusiano wa Umma kutoka TFDA, Gaudensia Simwanza alitaja bidhaa
hizo kuwa ni dawa za kuongeza ukubwa wa viungo vya mwili, kupunguza uzito wa mwili
na vipodozi vyenye kemikali za kuchubua ngozi bidhaa ambazo zinasababisha
madhara makubwa kwa binadamu ikiwemo ugonjwa wa Saratani.
“Kumezuka wafanyabiashara holela wanaotumia
mitandao ya kijamii kama vile Instagram, Facebook, Whatsup Groups na kwengineko kutangaza biashara ya dawa na vipodozi vyenye
kemikali hatari ambavyo vimepigwa marufuku na TFDA hivyo wanaohusika wajiandae,
hivi karibuni tutaanza kuwashughulikia.” Alisema Simwanza.
Alieleza kuwa TFDA kwa kushirikiana na Jeshi
la Polisi wameandaa mkakati madhubuti wa kuhakikisha wanawabaini na kuwakamata
wafanyabiashara wote wanaouza dawa na vipodozi hivyo kupitia mitandao na
kuwachukulia hatua ikiwemo kuwafikisha mahakamani au kuwatoza faini.
Hivi karibuni kumeibuka wimbi la wafanyabiashara
wa dawa mbalimbali pamoja na vipodozi ambao wanajitangaza kupitia mitandao ya
kijamii na kuna baadhi ya watu wananunua bidhaa hizo bila ya kuhakikisha
usalama wake jambo ambalo ni hatari kwa afya zao.
|
No comments:
Post a Comment