KAMATI KUU YA CCM:-Yaipongeza Serikali Ya Awamu Ya Tano Kwa Utendaji Wake. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, December 09, 2015

KAMATI KUU YA CCM:-Yaipongeza Serikali Ya Awamu Ya Tano Kwa Utendaji Wake.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
 
Tarehe 07/12/2015 Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ilifanya kikao chake cha kawaida mjini Dar es salaam kwa siku moja. Kikao hicho kiliongozwa na Mwenyekiti wa CCM, Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.
Kamati Kuu pia ilipokea taarifa juu ya utendaji wa Serikali katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020. 
 
 Kwa ujumla na kwa kauli moja Kamati Kuu ya CCM Taifa iliipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu na Waziri Mkuu Mhe. Kassim M. Majaliwa kwa kasi nzuri waliyoanza nayo katika utekelezaji wa Ilani hiyo.

Kamati Kuu kwa niaba ya Chama imeunga mkono hatua kadhaa zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuhakikisha Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2015-2020 inatekelezwa kwa ufanisi. Aidha, inapongeza na kuunga mkono juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali katika maeneo ya:-

(1) Kusimamia vyanzo vya mapato ya Serikali:

Kamati Kuu inapongeza na kuunga mkono juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuhakikisha kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) zinasimamia ukusanyaji wa kodi za Serikali ipasavyo. 
 
Juhudi hizi za Serikali ya Awamu ya Tano kwa muda mfupi zimezaa matunda yanayoonekana wazi. Aidha, Kamati Kuu inawataka wahusika mbalimbali kwenye maeneo hayo ya udhibiti wa vyanzo vya mapato kuhakikisha wanatoa ushirikiano kwa Serikali ili lengo liweze kutimia.

(2) Kudhibiti matumizi ya Serikali:

Kama ilivyoagizwa na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2015-2020, Serikali ya Awamu ya Tano imeanza vizuri na kwa kasi kusimamia udhibiti wa matumizi yasiyo ya lazima katika Serikali, ili kutumia fedha hizo kwenye utoaji wa huduma kwa wananchi.
 
 Kamati Kuu inaunga mkono juhudi hizi na kuwataka wote wanaohusika kwa namna moja ama nyingine na udhibiti wa matumizi hayo wamuunge mkono Rais Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali yake katika jitihada hizi.

(3) Uhimizaji wa wananchi katika kufanya kazi kwa bidii:

Kamati Kuu inawataka wanaCCM na wananchi wote kwa ujumla nchini kumuunga mkono Rais na Serikali yake kwa kuitikia wito wa kufanya kazi kwa bidii, kwa maarifa na uzalendo. 
 
Kamati Kuu inawahimiza watu wote kwenye maeneo yao ya kazi kujituma na kuchapa kazi ili kujenga nchi yetu na kumuunga mkono Rais Magufuli.

(4) Kusimamia na kuhimiza uwajibikaji katika Serikali, Taasisi na Mashirika yake: 

Kamati Kuu pia inapongeza na kuunga mkono juhudi zinazoendelea za kuhakikisha kunakuwa na uwajibikaji mkubwa Serikalini ili kuongeza kasi na ubora wa utoaji huduma. 
 
Katika kipindi cha muda mfupi matunda yake yameanza kuonekana na hivyo kuweka msingi mzuri wa kuboresha huduma kwa umma kwa njia endelevu. 

(5) Juhudi na jitihada hizi za Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais Dkt. Magufuli zimeleta matumaini mapya kwa sehemu kubwa ya wananchi na kukuza imani kwa Serikali yao. Hivyo, kila Mtanzania ana wajibu wa kuunga mkono jitihada hizi.

Pamoja na kuunga mkono na kupongeza kasi waliyoanza nayo Rais Magufuli, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu, Kamati Kuu inawataka Viongozi wengine wote kuiga mfano huu mzuri na kuhakikisha wanatimiza wajibu wao ipasavyo ili kutekeleza kwa haraka zaidi Ilani ya Uchaguzi ya CCM na kuleta maendeleo nchini.

Aidha, Kamati Kuu inawatakia Watanzania wote kheri ya Krismas na mwaka mpya wa 2016, na inaamini mwaka ujao utakuwa wa kuchapa kazi na wenye mafanikio zaidi.

Imetolewa na:-
Abdulrahman O. Kinana,
KATIBU MKUU WA CCM 08/12/2015.
 
 Papo kwa Papo >>>> Pata Picha, Habari za  Siasa, Kijamii, Biashara, Muziki na Michezo na Nyingine kwa kujiunga  na mimi hapa…..FACEBOOK , TWITTER INSTAGRAM , Pia tutumie tukio la Picha kwa WhatsApp .
 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad