Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya
Kikwete akiongoza kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichofanyika Ikulu, jijini Dar
es Salaam jana Februari 28,2015. Picha na Ikulu.
Kamati Kuu
ya CCM imezidi kuwaweka gizani makada sita waliomaliza adhabu ya kufungiwa kwa
miezi 12 baada ya kueleza kuwa uchunguzi dhidi yao unaendelea kwa muda
usiojulikana, uamuzi utakaowazuia kujitokeza rasmi kutangaza nia ya kuwania
urais kwa tiketi ya chama hicho tawala.
Edward
Lowassa, Bernard Membe, Frederick Sumaye, William Ngeleja, Stephen Wasira na
January Makamba, ambao walipewa adhabu hiyo Februari 18 mwaka jana 2014, sasa
watalazimika kusubiri hadi hapo Kamati Ndogo ya Maadili ya CCM itakapomaliza
uchunguzi wake, ikiwa imebaki miezi isiyopungua mitatu kabla ya wanachama
kuanza harakati za kuwania nafasi mbalimbali.
Kwa kawaida,
CCM huruhusu wanachama wake kuanza kuchukua fomu za kuwania urais, ubunge na
udiwani kati ya mwezi Mei na Juni na kabla ya hapo huruhusiwa kutangaza nia ya
kugombea nafasi wanazotaka, fursa ambayo makada hao wameikosa hadi sasa.
Katibu wa
itikadi na uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye aliwaambia waandishi wa habari
jana baada ya kumalizika kwa kikao cha Kamati Kuu, kuwa kwa kuzingatia kanuni
za maadili ya CCM, mwanachama aliyepewa onyo kali atakaa chini ya uangalizi kwa
kipindi kisichopungua miezi 12.'',-“Baada ya
miezi hiyo kwisha, Kamati Ndogo ya Maadili inaendelea na kazi yake kuchunguza
mienendo yao hao waliokuwa wamepewa adhabu katika kipindi chao cha adhabu cha
miezi 12 kama wametekelezaje masharti ya adhabu,” alisema Nnauye.
Alisema kazi
ya kamati hiyo ndogo ni kuchunguza ili kubaini kama makada wote sita walitimiza
masharti ya adhabu waliyopewa na kwamba itakapomaliza uchunguzi katika muda
usiojulikana itapeleka taarifa Kamati Kuu.
“Itachukua
wiki, itachukua mwezi, itachukua miezi ni kwamba itakapokamilika na Kamati Kuu
kama kutakuwa na taarifa yoyote tutautaarifu umma juu ya kinachoendelea,”
alisema Nnauye.
Kikao cha
Kamati Kuu, ambacho huhusisha viongozi wa juu serikalini na kwenye chama hicho
tawala pamoja na wanachama 14 wa kuchaguliwa kutoka Zanzibar na Bara,
kilifanyika Ikulu na Nape aliongea na waandishi wa habari kwenye ofisi ya Umoja
wa Vijana wa CCM iliyo Lumumba.
Kati ya
waliofungiwa, Wasira, ambaye ni Waziri wa Kilimo na Ushirika, ni mjumbe wa
Kamati Kuu.
Lowassa,
aliyekuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Nne, na Membe, Waziri
wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, ndiyo wanaochuana vikali na
wafuasi wao wamekuwa wakishambuliana kwenye mitandao ya kijamii.
Sumaye pia
alikuwa Waziri Mkuu kwenye Serikali ya Awamu ya Tatu, wakati Ngeleja, ambaye
amepewa adhabu kubwa zaidi kutokana na kuhusika kwake kwenye sakata la Akaunti
ya Tegeta Escrow, alikuwa Waziri wa Nishati na Madini, na Makamba ni Naibu
Waziri wa Sayansi na Teknolojia.
Makada hao
ambao walipewa kifungo cha miezi 12 Februari 18 mwaka jana, baada ya chama
hicho kubaini kuwa walianza kupiga kampeni mapema kinyume na utaratibu wa CCM,
bado hawajatangaza nia ya kutaka kuwania urais mwaka huu 2015, ingawa habari zinasema
kuwa walishakusanya nguvu za kuanza mchakato huo baada ya kutoka kifungoni.
Habari zinasema kuwa makada hao walikuwa wanasubiri uamuzi wa Kamati Kuu ili
waingie rasmi kwenye kinyang’anyiro cha urais huku baadhi wakipanga hafla kubwa
za kutangaza nia.
Source:-Mwananchi Jumapili.
UNGANA NASI KATIKA FACEBOOK , TWITTER , INSTAGRAM , Pia tutumie tukio la Picha kwa WhatsApp +255789925630.
|
Sunday, March 01, 2015
KAMATI KUU YA CCM:-Urais wa Membe, Lowassa gizani..''
Tags
# SIASA
Sambaza Hii
Chief Editor | Mhariri
SIASA
Labels:
SIASA
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
Kuhusu Mwandishi
Journalist / Chief Editor / Tanzanian Blogger
Simu: 0756830214 / 0620197747 / 0789925630.
No comments:
Post a Comment