NIPASHE.
Watu wanne waliohukumiwa
jana na Mahakama Kuu kunyongwa hadi kufa baada ya kupatikana na hatia ya kuua
albino, wameongeza idadi ya waliokwisha kutiwa hatiani ili wanyongwe kwa kosa
hilo kufikia 17 nchini.
Idadi hiyo imeongezeka
baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza kuwatia hatiani
watu wanne jana kwa mauaji ya mwanamke mwenye ulemavu wa ngozi yaliyofanyika
mwaka 2008.
Kabla ya jana, watu 13
walihukumiwa kunyongwa hadi kufa kutokana na mauaji ya watu wenye ulemavu wa
ngozi katika maeneo kadhaa ya Tanzania hususan mikoa ya Kanda ya Ziwa kutokana
na imani za kishirikina.
Watu wanne jana akiwamo
mume wa marehemu, walihukumiwa adhabu ya kunyongwa hadi kufa baada ya
kupatikana na hatia ya kumuua mlemavu wa ngozi, Zawadi Mangidu (22),
mkazi wa Nyamalulu, Kata ya Kaseme, wilayani Geita.
Hukumu hiyo ilitolewa na
Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza, huku ndugu wa waliohukumiwa adhabu hiyo ya
kunyongwa hadi kufa ambao walikuwa miongoni mwa wakazi wengi wa mji huo
waliofurika mahakamani hapo kushuhudia hukumu hiyo, wakiangua vilio.
Waliokumbwa na adhabu
hiyo ni Masalu Kahindi (54), Ndahanya Lumola (42), Singu
Nsiyantemi (49) na Nassor Said (47), mume wa marehemu Zawadi
Mangindu.
Mahakama hiyo
iliwahukumu watu hao ambao ni wakazi wa wilaya hiyo, baada ya kupatikana na
hatia ya kula njama na kushiriki kumuua kwa kukusudia mlemavu huyo wa
ngozi.
Akitoa hukumu hiyo, Jaji
De-Mello, alisema amezingatia kwa makini na tahadhari kubwa katika kufikia
uamzi huo baada ya kuridhishwa na ushahidi uliotolewa na mashahidi 12 wa upande
wa mashtaka na utetezi, kwamba washtakiwa walitenda kosa hilo bila kuwa
na shaka yoyote.
Jaji De-Mello alisema
katika hukumu zilizotangulia, pia zilibainisha kuwa mauaji ya watu wenye
ulemavu wa ngozi yamekuwa yakitekelezwa na mtandao mkubwa na siyo rahisi kuubaini
kirahisi.
Awali, upande wa
mashitaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Hezron Mwasimba,
akisaidiana na wakili Janeth Kisibo, ulidai kuwa washtakiwa kwa
pamoja kwa makusudi walishirikiana kula njama na kutenda kosa la kumuua mlemavu
huyo wa ngozi, saa moja usiku, Machi 11, mwaka 2008 katika kijiji cha Nyamalulu
kata ya Kaseme wilayani Geita.
NIPASHE.
Wakati idadi ya watu
waliopoteza maisha katika maafa yaliyosababishwa na mvua iliyonyesha
ikiambatana mawe, upepo mkali na kubomoa nyumba za wananchi Wilaya ya Kahama
mkoani Shinyanga, ikiongezeka kutoka 42 na kufikia 46, baadhi ya wananchi wa
eneo hilo wamelihusisha janga hilo na ushirikina.
Mwenyekiti wa Serikali
ya kijiji cha Mwakata wilayani Kahama, Salum Mohamed,alimweleza
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuwa baadhi ya wananchi wamejenga dhana
kuwa tukio hilo limetokana na ushirikina.
Hata hivyo, Pinda
aliyewasili hapa jana, aliwataka wananchi hao kuachana na dhana hiyo potofu
kuwa mvua zilizonyesha na kusababisha maafa hayo, zimetokana na ushirikina.
Mvua hiyo ilinyesha juzi
usiku na kuleta maafa katika vijiji vya Mwakata, Nyumbi na Magung’hwa vilivyopo
kata ya Isaka wilayani Kahama.
Idadi hiyo imeongezeka
kufuatia majeruhi wanne waliokuwa wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya
Kahama kufariki dunia usiku wa kuamkia jana kuongeza idadi ya waliokufa
katika janga hilo kufikia 46.
Waziri Mkuu, alitembelea
vijiji vilivyoathirika na kuwapa pole waathirika na kusema serikali
itahakikisha waathirika wote wanapewa msaada unaotakiwa na kwamba tayari
chakula kimeanza kugawiwa kwa wananchi na mahema ya kutosha yametolewa.
Pinda aliagiza waatalam
kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kuweka kambi katika kijiji cha Mwakata
kilichoathirika kwa ajili ya kufanya tathmini.
Waziri Mkuu alisema
kutokana na janga hilo, kuna uwezekano wa kutokea magonjwa ya mlipuko.
Aidha, aliiagiza timu
ndogo ya uratibu wa maafa iliyoundwa na Mkoa wa Shinyanga, isimamie vizuri
misaada inayotolewa na wasamaria wema ili iwafikie waathirika wote.
Waziri Mkuu, Mizengo
Pinda, jana aliwasili Kahama na kutembelea vijiji vilivyoathirika na kuwapa
pole waathirika na kuwataka wananchi waondokane na fikra potofu kuwa tukio
limetokana na masuala ya kishirikina.
NIPASHE.
Serikali imekiri kuwapo
kwa uhaba wa tani 100,000 za sukari nchini ikieleza kuwa kiasi kilichopo sasa
cha tani 67,000 kinatosheleza hadi mwisho wa mwezi huu pekee.
Kutokana na uhaba huo,
serikali imezuia tani 11,059.75 za sukari iliyokuwa inasafirishwa kwenda nje ya
nchi ili itumike nchini kuziba pengo hilo.
Hayo yalibainishwa na
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira, wakati
akiwasilisha taarifa yake kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na
Maji, kuhusu hali ya uzalishaji na usambazaji wa sukari nchini.
Alisema uhaba huo
unatokana na uzalishaji wa sukari kutotosheleza mahitaji ya nchi, baadhi ya
viwanda kutokuwa na akiba yoyote hadi sasa na vingine kufungwa kwa ajili ya
kusubiri msimu mwingine wa uzalishaji.
Alisema kiasi halisi
kinachotosheleza mahitaji ya nchi ni tani 420, 000 kwa mwaka, lakini kiasi
kilichozalishwa kwa msimu wa 2013/2014 ni tani 300,000 pekee hivyo kuwa na
upungufu wa tani 120, 000.
Kwa mujibu wa Wasira,
hali hiyo inatokana na changamoto mbalimbali ikiwamo ya kuyumba kwa soko la
sukari ambako kulisababishwa na uingizwaji wa bidhaa hiyo kwa njia za magendo.
Hata hivyo, alisema
utaratibu wa kuagiza sukari kwa pamoja ni mpya na unaweza kuchukua muda mrefu
hivyo, imeamuliwa kuwa sukari iliyohifadhiwa kwenye maghala kwa muda mrefu
kiasi cha tani 11, 059.75 ifanyiwe tathmnini ya ushuru na Mamlaka ya
Mapato (TRA) na iingizwe kwenye soko kuziba pengo.
MTANZANIA.
Wakazi wa Kijiji cha
Mwakata, Wilaya ya Kahama, Mkoa wa Shinyanga, jana walilazimika kufukua
makaburi mawili walimokuwa wamezika watoto watano wa familia moja
waliofariki dunia juzi baada ya mvua kubwa ya mawe kunyesha kijijini hapo.
Ufukuaji wa kaburi hilo
ulifanyika mchana na kuitoa miili ya watoto hao, Luku Masemba(14), Paschal Masemba (11), Mulyante
Masemba (9), Sesela Masemba (7) naMasele Masemba (5).
Taarifa zilizopatikana
zinasema kuwa kaburi hilo lilifukuliwa baada ya Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya,
kuagiza lifukuliwe ili marehemu hao wazikwe kila mmoja katika kaburi lake.
Kabla ya agizo hilo
lililotolewa na Mpesya mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Ali Rufunga, miili
ya watoto watatu wote wa kike ilikuwa imezikwa katika kaburi moja.
Wakati watoto hao wa
kike walikuwa wamezikwa katika kaburi moja, maiti mbili za watoto wa kiume
zilikuwa zimezikwa katika kaburi moja.
Kwa mujibu wa taarifa
hizo, maiti hizo zilikuwa zimefungwa kwenye mifuko ya sandarusi baada ya
wananchi kukosa sanda kutokana na Serikali kuchelewa kutoa utaratibu wa namna
ya kuzikwa miili hiyo.
“Nimeambiwa mmewazika hawa watoto watatu kaburi
moja na wengine kaburi lao moja. Hapana, hapana, huu siyo utaratibu hata
kidogo.nataka hawa marehemu wafukuliwe na kila mmoja azikwe kwenye kaburi lake
siyo kama mlivyofanya ninyi.a watu kwa pamoja labda itokee hawatambuliki na
ndugu zao hawajajitokeza.
“Hawa watoto ni wa familia
moja na mnawafahamu kwa majina na umri wao, iweje muwazike kaburi moja watatu
na jingine wawili?
“Naagiza wafukuliwe na
wazikwe upya katika mazingira ya binadamu,”:- Mpesya.
MTANZANIA.
KATIKA hali isiyokuwa ya
kawaida, watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino), wamepigana ngumi na mateke
wakigombea kuingia kumwona Rais Jakaya Kikwete, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Tukio hilo la aina yake
lilitokea jana majira ya saa nne asubuhi ambapo lilianzia kwenye eneo la
mapokezi Ikulu mara baada ya walemavu hao kukaguliwa na kuwekwa kwenye chumba
maalumu cha kupumzikia wageni.
Baada ya muda, ofisa wa
Ikulu alifika kwenye chumba walipokuwa walemavu hao akiwa na karatasi yenye
orodha ya watu 15, ambao ndiyo waliopaswa kumwona Rais.
Baada ya ofisa huyo
kuanza kusoma majina ya wahusika, albino wote waliokuwa kwenye chumba hicho
walinyanyuka kutoka kwenye viti vyao na kusimama karibu na mlango, ambako
alikuwa amesimama.
Kila ofisa huyo
alipokuwa akisoma jina, mhusika alitoka nje ya chumba hicho tayari kwa kwenda
kumwona Rais.
Baada ya ofisa huyo kumaliza kusoma majina hayo, alisema: “Hawa ndio
wanaokwenda kuwawakilisha kwa sababu hamuwezi kuingia kundi lote hili.”
Baada ya majina hayo
kutajwa, mmoja wa albino hao, Nuru Chagutu, ambaye hakutajwa,
alisema hakubalini na kitendo cha viongozi pekee kumwona Rais ili hali wajumbe
wengine ambao pia ni wahathirika wa mauaji ya albino wakibaki getini.
Alisema pia yeye na
wanaharakati wenzake wa Chama cha Tunataka Haki ya Kuishi (THK), hawamtambui Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu wa Ngozi Tanzania (TAS),Ernest Kimaya,
ambaye alikuwa kwenye orodha ya watu 15 waliopangwa kumwona rais.
Alihoji pia sababu za
Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Walemavu Tanzania (Shivyawata), Amon Mpanju, ambaye si mlemavu wa ngozi, kuwamo
kwenye orodha hiyo huku akiwa si mlemavu wa ngozi.
MWANANCHI.
Wakati CCM ikielekea
katika kipindi kigumu cha kuamua mgombea wake wa urais kwenye Uchaguzi Mkuu
ujao, Makongoro Nyerere, ambaye ni mtoto wa Baba wa TaifaMwalimu
Julius Nyerere, amezungumzia taarifa zilizoenea kwenye mitandao ya kijamii
zikimtaja kuwa na mpango wa kuwania nafasi hiyo ya juu nchini.
CCM, ambayo imeshika
nchi tangu kurejeshwa kwa siasa za vyama vingi, hujikuta katika
wakati mgumu kila wakati inapotakiwa kutoa mgombea wa kurithi nafasi ya Rais
aliye madarakani baada ya kuongoza vipindi viwili vya miaka mitano kila kimoja.
Tayari wanachama wanne
wa chama hicho tawala wameshatangaza rasmi kuwania urais huku wengine sita
wakifungiwa kwa makosa ya kudaiwa kuanza kampeni mapema, huku kukiwa na
mlolongo wa watu wanaotajwa kuwa na mpango wa kujitokeza kuwania nafasi hiyo,
akiwamo Makongoro, ambaye imeelezwa kuwa ameshauriwa kuchukua uamuzi huo kujaribu
kukinusuru chama kutokana na makundi yanayoonekana kujitokeza katika mbio hizo.
“Mimi si mtabiri, siwezi
kukwambia nitagombea au la, lakini uamuzi wangu utajulikana mara kipenga
kitakapopulizwa na CCM,” alisema Makongoro ambaye ni ofisa wa zamani wa
Jeshi la Wananchi (JWTZ) na mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (Eala).
Vyanzo hivyo vya habari
vimeeleza kuwa mkakati wa kuhakikisha Makongoro anakuwa rais, unaratibiwa na
baadhi ya makada waliowahi kufanya kazi na Mwalimu Nyerere.
Mkakati huo pia unatajwa
kuwa ulianza pale alipochaguliwa kuwa mbunge wa Eala.
Tayari Waziri Mkuu
Mizengo Pinda, January Makamba, ambaye ni Naibu Waziri wa
Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Lazaro Nyalandu ambaye ni
Waziri wa Maliasili na Utalii na Hamisi Kigwangala wametangaza
nia ya kuomba ridhaa ya CCM kuwapitisha kuwania urais.
Hata hivyo, upinzani
mkubwa unaonekana kuwa kwa vigogo ambao hawajatangaza nia hiyo na ambao
wanatumikia adhabu ya kufungiwa kwa zaidi ya miezi 12 kutokana na
kikiuka taratibu za chama hicho.
Miongoni mwa ambao
hawajajitokeza ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa,ambaye
wafuasi wake wamekuwa wakijitokeza katika siku za karibuni kueleza wazi msimamo
wao kuwa ndio chaguo sahihi, na Bernard Membe, ambaye ni
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Pia yumo Waziri Mkuu wa
Serikali ya Awamu ya Tatu, Frederick Sumaye, Spika wa zamani wa
Bunge, Samuel Sitta, Waziri wa Kilimo na Chakula, Steven
Wasira na Naibu Waziri wa Fedha-Sera, Mwigulu Nchemba, ambaye
alionywa na chama hicho dhidi ya safari zake mikoani zilizodaiwa kuwa na dalili
za kampeni.
Makongoro hakuonyesha
kukataa wala kukubali kuhusu uamuzi wa kugombea nafasi hiyo iliyoshikwa na baba
yake kwa takribani miaka 25.
“Ninachoweza kutabiri kwa sasa ni iwapo nina njaa
basi lazima nitakula au simba akitokea lazima nikimbie. Kama nina usingizi na
kuna kitanda karibu lazima nitalala lakini mambo mengine siwezi kuyasemea,” alisema Makongoro ambaye aliwahi kuwa mbunge
wa Arusha Mjini kwa tiketi ya chama cha NCCR-Mageuzi.
Alisema anasubiri siku
ambayo CCM itatangaza mchakato wa kuchukua fomu ndipo hatma yake itajulikana.
MWANANCHI.
Waziri wa Ujenzi, Dk
John Magufuli ameagiza kusimamishwa kazi aliyekuwa kigogo wa Kituo cha
Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC) ambaye hafanyi
kazi tena kituoni hapo.
Agizo hilo alilitoa
juzi, huku akitaka pia mkurugenzi wa zamani wa majengo na miradi wa AICC, Paul
Ndossa ambaye awali akifanya kazi Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) akiwa mtaalamu na mshauri, asimamishwe.
Wakati Dk Magufuli
akitoa agizo hilo, Ndossa alikuwa ameshaondoka AICC tangu Januari.
Agizo hilo lilitokana na
Mtendaji Mkuu wa TBA, Elius Mwakifugile kudai kuwa Ndossa
ndiye aliyesimamia ujenzi wa majengo ya ofisi za wakuu wa wilaya za Siha na
Moshi.
Majengo hayo mawili
yanadaiwa kugharimu mabilioni ya shilingi, lakini yalijengwa chini ya kiwango
tangu yalipokamilika miaka mitano iliyopita na hayafai kwa matumizi ya kiofisi.
Hata hivyo, Ndossa
alipotafutwa kuzungumzia madai hayo alishangazwa na kutuhumiwa kuwa alikuwa
mtaalamu mshauri wa miradi hiyo.
Ndossa alisema waziri
atakuwa amepewa taarifa potofu.
“Mimi sikuwa consultant (mtaalamu mshauri) wa
ujenzi wa hilo jengo (la Siha). Consultant wa mradi walikuwa TBA, Makao
Makuu…waliitumia ofisi ya Kilimanjaro mimi sikuwa Moshi.
“Nilikuwa nakwenda kule kusaidia tu. Wakati wa
kufanya Site meeting (vikao eneo la mradi). Mimi nilikuwa Arusha nitakuwaje
consultant Kilimanjaro? Watakuwa wamempotosha Waziri,” alisisitiza Ndossa.
Licha ya kukana, wakati
Dk Magufuli akikagua jengo la ofisi ya mkuu wa Wilaya Siha, alielezwa kuwa,
ujenzi wa jengo hilo uliokuwa chini ya viwango na ulisimamiwa na Ndossa .
HABARI LEO.
Baraza la Maadili ya
viongozi wa umma limesitisha kusikiliza mashauri mawili likiwemo la Mkurugenzi
Mkuu wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA), Philip Salibokohadi pale Mahakama Kuu itakapotoa
uamuzi juu ya uhalali wa mashauri hayo, kusikilizwa na baraza hilo.
Shauri lingine
lililositishwa kusikilizwa na baraza hilo ni la aliyekuwa Mkurugenzi wa Huduma
za Kisheria Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa
Mujunangoma ambaye pingamizi aliloweka lilikubaliwa kutokana na kuwa
na kesi ya jinai Kisutu inayofanana na shauri linalomkabili mbele ya baraza
hilo.
Baraza hilo lilifikia
uamuzi huo, baada ya upande wa mlalamikiwa kuweka pingamizi la kuendelea
kusikilizwa kwa mashauri hayo, lakini baraza hilo liliyatupilia mbali
mapingamizi hayo yanayomhusu Saliboko, ndipo upande wa mlalamikiwa ulipoamua
kukata rufaa Mahakama Kuu juu ya uamuzi huo.
Awali Mwenyekiti wa
baraza hilo, Jaji Hamisi Msumi, alipinga na kulitupilia mbali
pingamizi lililowekwa na wakili wa Saliboko, lililotaka baraza hilo lisitishe
kusikiliza shauri hilo kwa kuwa halina uwezo wa kufanya hivyo kutokana na amri
iliyotolewa mwaka jana Mahakama Kuu.
Akiwasilisha pingamizi
hilo mbele ya Baraza hilo, Dar es Salaam jana, Wakili wa mlalamikiwa, Jamhuri
Johnson, alisema kutokana na zuio lililowekwa na amri iliyotolewa
mwaka jana katika shauri namba 51 la Mahakama Kuu, baraza hilo halina uwezo wa
kuendelea na shauri hilo linalomkabili Saliboko.
“Katika amri ile inatokana na kesi ya msingi ya
IPTL dhidi ya Waziri Mkuu na wenzake saba, ilikataza na kuweka zuio kwa vyombo
vyovyote vya umma kujadili suala linalohusiana na IPTL na akaunti ya Escrow,
hadi kesi ya msingi itakapoamuliwa,”Johnson.
Alisema anafahamu kuwa
tayari baraza hilo lilishatolea uamuzi pingamizi kama hilo lililotolewa na
Mbunge wa Bariadi Magharibi Andrew Chenge, lakini bado
anaamini zuio hilo linalihusu pia na baraza hilo, hivyo halina uwezo wa
kuendelea kusikiliza shauri hilo.
Source:-Millardayo.
|
No comments:
Post a Comment