Mauaji
yanayotokana na migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji mkoani Morogoro,
yanazidi kutikisa baada ya watu wengine watatu kuuawa kwenye Kijiji cha Mbiligi, Kata ya Magole wilayani Kilosa.
Tukio hilo, ambalo
limetokea mwezi mmoja tu baada ya mkulima mmoja kuuawa kwenye Bonde la Mgongola
wilayani humo, ni kati ya matukio mengi ya mapigano baina ya jamii hizo mbili
na ambayo yalijadiliwa kwa kina kwenye mkutano uliopita wa Bunge la Muungano.
Habari kutoka eneo
la tukio zinaeleza kuwa, juzi saa 2.00 asubuhi wakulima wapatao 15 walikwenda
eneo la Matembele na Ming’oni, jirani na Kijiji cha Mbigili ili kupanda mpunga,
lakini saa nne baadaye vijana wawili wa Kimasai walifika na kuhoji sababu za
kutumia eneo hilo kwa kilimo wakati ni mali ya Kijiji cha Mabwegela na
kuwaamuru waondoke.
Lakini wakulima
hao walikaidi na ndipo muda mfupi baadaye likaibuka kundi la wafugaji wapatao
50 na kurejea swali hilo.
Kwa mujibu wa
habari hizo, wakulima waliamua kutoroka, ndipo baadhi yao waliposhambuliwa kwa
mikuki, virungu, mishale na visu na kusababisha vifo vya watu hao watatu.
Mkuu wa Wilaya ya
Kilosa, Elias Tarimo alisema watu wengine kadhaa walijeruhiwa
na wamelazwa katika Kituo cha Afya cha St
Joseph cha Dumila, Kilosa.
MWANANCHI.
Wakala wa Ukaguzi
wa Madini nchini (TMAA)
umetangaza dau nono kwa yeyote atakayewezesha kukamatwa kwa mfanyabiashara
yeyote anayesafirisha madini kwa njia za magendo kupitia njia za panya zaidi ya
400 zilizopo nchini.
Hayo yalisemwa
jana na Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa TMAA, Bruno Mteta alipokuwa
akitoa taarifa ya mwaka uliopita ya mapambano dhidi ya magendo ya madini mbele
ya waandishi wa habari.
“Kwa kipindi cha kuanzia Januari mpaka Desemba mwaka jana,
wakala umeweza kukamata watoroshaji wa madini ya aina mbalimbali katika matukio
27 tofauti. Tunawaomba Watanzania wazalendo kushirikiana nasi ili kuwabaini
watu wote wanaojishughulisha na magendo haya na tayari wizara imethibitisha
zawadi ya asilimia tano ya thamani ya madini yatakayokamatwa itatolewa,”:- Mteta.
Wakala umeanza
utekelezaji wa mkakati huo ulioratibiwa tangu mwaka 2012 wakati huo Serikali
ilisema itatoa asilimia 30 ya thamani ya mzigo baada ya kugundua kuwapo kwa
watu wanaolipwa asilimia 10 kusaidia kufanikisha magendo hayo na hivyo
kuchangia kuikosesha mapato.
Alisema hilo
lilikuwa ni pendekezo linaloendelea kutekelezwa na kwamba, kiasi hicho ni haki
ya mtoa taarifa ambaye hatotajwa mahali popote katika mchakato mzima wa hatua
za kisheria.
“Utoroshaji wa madini umekithiri, zinahitajika nguvu za pamoja
ili kuhakikisha Taifa linanufaika na rasilimali zake. Atakayekamatwa mali yake
itataifishwa na kama ni kampuni basi itanyang’anywa leseni yake na kutoruhusiwa
tena kufanya shughuli zake hapa nchini,” :- Mteta.
Kwa madini
yanayoingizwa ili yasafirishwe nje bila kuwa na vibali, alisema nayo
yakikamatwa yatataifishwa hivyo kuwataka wote wanaofanya hivyo kutumia ofisi za
ukaguzi zilizoko mipakani kuhalalisha madini waliyonayo.
NIPASHE.
Siku tatu baada ya
mtoto mwenye ulemavu wa ngozi (albino),
Yohana Bahati mwenye umri wa mwaka mmoja, kutekwa na watu
wasiofahamika, hatimaye mwili wake umepatikana ukiwa umekatwa miguu,
mikono yote na kiwiliwili chake kufukiwa shambani katika Kitongoji cha
Mapinduzi, Kijiji cha Rumasa ndani ya hifadhi ya msitu wa Biharamulo Wilaya ya
Chato, mkoani Geita.
Mtoto huyo
alinyakuliwa Jumapili iliyopita nyumbani kwao saa 2:15 usiku akiwa amebebwa na
mama yake mzazi, Esther Jonathan (30), baada ya kujeruhiwa kwa
kupigwa mapanga usoni, mwili wake ulipatikana baada ya msako uliofanywa na wananchi.
Kamanda wa Polisi
Mkoa wa Geita, Joseph Konyo, alisema mwili huo ulipatikana
juzi saa 12:30 jioni katika shamba la mahindi lisilo rasmi kutokana na kulimwa
ndani ya hifadhi ya msitu wa Biharamulo, wilayani Chato.
Mwili huo
ulipatikana kutokana na jitihada za wananchi walioshirikiana na makachero wa
Jeshi la Polisi baada ya mwananchi mmoja (jina wanalo polisi) kuonekana
akikatisha katika msitu huo, huku upande wa shati lake ukionekana ukiwa na
damu.
Kamanda Konyo
alisema baada ya raia huyo kuona viashiria hivyo, alilazimika kutoa taarifa kwa
wananchi wenzake, ambao walifuatilia mwelekeo wa nguo hiyo na kufanikiwa kuona
shimo limefunikwa na udongo mbichi kisha walipofanikiwa kufukua wakauona mwili
huo.
“Baada ya wananchi hao kufukua shimo hilo, walifanikiwa kukuta
mwili wa mtoto Yohana ukiwa umekatwa mikono na miguu yote…baadaye mwili huo
ulichukuliwa na askari hadi katika Hospitali ya Wilaya ya Chato kwa ajili ya
uchunguzi zaidi,”:- Konyo.
Hata hivyo, baada
ya kuupata mwili huo, wananchi hao walipandwa na jazba na kumtuhumu mwananchi
huyo kuhusika na mauaji hayo na kuanza kumshambulia kabla ya polisi kuingilia
kati na kumuokoa kutoka mazingira hayo.
NIPASHE.
Wanafunzi wa Chuo
cha Usimamizi wa Fedha (IFM)
jijini Dar es Salaam wametangaza azma yao ya kumuunga mkono Waziri Mkuu
mstaafu, Edward Lowassa (pichani), iwapo ataamua kugombea urais katika Uchaguzi
Mkuu wa mwaka huu.
Wamesema wataanza
kutekeleza azma yao hiyo kwa vitendo kwa kumsindikiza atakapokwenda kuchukua
fomu za kukiomba ridhaa chama chake ya kuwania nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu
wa mwaka huu.
Kauli hiyo
ilitolewa na Mbunge wa Bunge la Serikali ya Wanafunzi wa Chuo hicho,
Hafsa Masumai, kwa niaba ya wenzake, alipozungumza na waandishi wa
habari, jijini Dar es Salaam juzi.
Alisema wanamuunga
mkono Lowassa kwa kuwa ni miongoni mwa viongozi watetezi wa masuala ya elimu.
“Wanafunzi wamekuwa wanakabiliwa na changamoto mbalimbali
ambazo zimekuwa sugu hata kutatuliwa na serikali, ikiwamo mikopo kwa wanafunzi
wa elimu ya juu,” :-Masumai.
Aliongeza: “Tutamuunga mkono Lowassa, kwani ni kiongozi, ambaye
anaonekana kujali elimu na tunaamini anaweza kutatua matatizo haya, ambayo
yamekuwa yanatukabili kwa muda mrefu.”
Alisema Lowassa
mbali na kuwa kiongozi aliyetetea elimu pia amekuwa akisaidia vijana katika
nyanja mbalimbali, ikiwamo kuwasaidia kwenye vikundi vyao na kujikwamua dhidi
ya makali ya maisha.
NIPASHE.
Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika,
amemkosoa Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM)
Andrew Chenge, kwa kujiita ‘nyoka wa
makengeza’ kwa madai kwamba, anastahili kuitwa ‘nyoka wa ufisadi’.
Mnyika katika
taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, alisema wananchi wanapaswa kumuita
Chenge ‘nyoka wa ufisadi’ badala ya kujisifia kuwa ni ‘nyoka mwenye makengeza’
kwa kuwa amehusika katika kutafuna mali ya umma.
“Kauli ya Chenge kama ilivyokuwa kwa ile ya ‘vijisenti’, ni
kiburi cha kifisadi,”:- Mnyika.
Chenge alitoa
kauli hiyo juzi wakati akihutubia wananchi katika mkutano wa hadhara
uliofanyika katika kijiji cha Mahaha kata ya Vunamala, wilayani Bariadi, mkoani
Simiyu, akiwaeleza wananchi wa jimbo lake kuwa aitwe nyoka kwa kuwa ni mjanja
wa kutafuta fedha kwa ajili ya wananchi wake.
Mnyika alisema
udhaifu wa serikali na vyombo vyenye mamlaka ya kuchunguza na kuchukua hatua
dhidi ya tuhuma za ufisadi unaodaiwa kufanywa na Chenge na watuhumiwa wengine
wa ufisadi ndiyo unaowalinda nyoka wa ufisadi na sasa wanajigamba kuwa ni
wajanja wa kutafuta fedha kifisadi.
“Chenge anadai kwamba yeye ni mjanja wa kutafuta fedha za
wananchi wa jimbo lake ili hali yeye na wenzake wamesababisha wananchi wa jimbo
lake na mengine nchini kukosa fedha nyingi zaidi za miradi ya maendeleo mpaka
hivi sasa kutokana na ufisadi wa Tegeta-Escrow,” Mnyika.
NIPASHE.
Mwenyekiti wa
Serikali ya Mtaa wa Shamariwa ‘A’, Kata ya Igoma, Wilaya ya Nyamagana, jijini
Mwanza, Julias Makoye (CCM), amekutwa amejinyonga juu ya mti
ulio jirani na nyumba yake usiku wa jana.
Makoye
aliyetangazwa mshindi wa kiti hicho katika uchaguzi wa serikali za mitaa
uliofanyika Desemba 14, mwaka jana, ameuongoza mtaa huo kwa awamu ya pili baada
ya kuongoza miaka mitano iliyopita.
Mke wa marehemu, Ivona
Polikalapo, alisema saa 10 juzi jioni alimsikia mumewe akiongea na mtu
kwenye simu yake ya mkononi na kumsisitiza anahitaji mzigo wake wote.
“Jana (juzi) saa 10 jioni nilimsikia mume wangu akiongea na
mtu katika simu na kutaka alipwe mzigo wake wote kutokana na kukaa muda mrefu,
lakini aliyekuwa akizungumza naye sikumfahamu ni nani,”:- Polikalapo.
Aidha, alisema
ilipofika saa 10 alfajiri ya jana, mbwa wao walisikika wakibweka kwa muda mrefu
hali iliyomfanya marehemu atoke nje kuangalia kilichopo katika banda lao la
mifugo huku (mke) akiendelea kuandaa chakula cha mifugo hao.
“Baada ya mume wangu kuamka na kwenda kuangalia kilichopo nje,
hakuweza kurejea ndani hadi pale nilipotoka kwenda kumwaga uchafu shimoni
nikashangaa baada ya kumuona ananing’inia juu ya mti…nilipojaribu kumuita
hakuitika,” alisema.
Hata hivyo, mama
huyo anasema haamini kama mume wake amejinyonga bali kanyongwa kutokana na mti
aliojitundika kutoonekana kuwapo na jiwe la ‘sapoti’ ili kutekeleza azma yake
hiyo.
MTANZANIA.
Raia wa kigeni
wanaofanya biashara haramu ya madini wamekamatwa na madini yenye thamani ya
Dola za Marekani 113,807.11 sawa Sh milioni 641.853 katika uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).
Akizungumza na
waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa TMAA,
Bron Mteta alisema watu hao walikamatwa katika matukio 27
tofauti huku wakiwa na madini ya aina mbalimbali.
Alisema miongoni
mwa matukio hayo ni pamoja na lile la Juni 12 mwaka jana ambapo raia mmoja
alikamatwa kwenye uwanja huo akiwa na madini ya vito vyenye uzito wa gramu
1,290 yenye thamani ya dola za Marekani 11,591.82.
Alisema mtuhumiwa
alifikishwa mahakamani na kuhukumiwa adhabu ya kulipa faini ya Sh 300,000.
Alisema katika
tukio jingine la Desemba 14 mwaka jana,raia mwingine wa kigeni alikamatwa
kwenye uwanja huo akiwa na madini ya vito ya uzito wa karati 288 na thamani ya
dola za Kimarekani 23,235.50.
Alisema mpaka sasa
hatua za kisheria zimechukuliwa kwa mtuhumiwa huyo ikiwa ni pamoja na
kufikishwa mahakamani na kupewa adhabu ya kulipa faini ya sh.500,000.
HABARI LEO.
Mamlaka ya
Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) imeshikwa
kigugumizi kuhusu suala la kushusha nauli ya magari ya abiria kwa kutoa sababu
za kisheria pamoja na ukokotoaji wa tozo.
Kwa mujibu wa
Kanuni za Tozo pamoja na Sheria, Sumatra inapaswa kurejea tozo ya huduma baada
ya mtoa huduma au mtumiaji wa huduma kupitia Baraza la Ushauri la Watumiaji wa
Huduma zinazodhibitiwa na Sumatra (Sumatra CCC)
kuwasilisha maombi.
Pia huridhia
viwango kwa kuzingatia masuala yote yanayoathiri gharama za uendeshaji, mafuta
ikiwa ni moja ya eneo muhimu katika kukokotoa tozo zinazostahili kuridhiwa.
Meneja Mawasiliano
kwa Umma, David Mziray alisema mwasilishaji wa maombi awe ni
mtoa huduma au Sumatra CCC anapaswa atoe maelezo ya kina kuhusu sababu za
kuomba mabadiliko ya tozo, jinsi alivyoathirika, ikiwa ni pamoja na kuambatisha
nyaraka muhimu zinazoweza kuthibitisha hoja zake.
Alisema maoni ya
wadau huzingatiwa kwa pamoja na masuala yaliyoainishwa katika Sheria ya Sumatra
ambayo inatoa muongozo wa masuala ya kuzingatia katika kuridhia viwango vya
tozo mbalimbali.
Alisema masuala
hayo ni pamoja na gharama za uendeshaji, haja ya kukuza ushindani katika soko
na kulinda maslahi ya watumia huduma na watoa huduma.
Akizungumzia
kuridhia viwango kwa kuzingatia masuala yote yanayoathiri gharama za uendeshaji
wanazingatia umuhimu wa kuwa na huduma endelevu, kulinda maslahi ya watumiaji
na watoa huduma kwa kuweka mizania sawa na gharama za uendeshaji ikiwa ni
pamoja na mishahara na gharama za matengenezo.
Source:-Millardayo.
|
No comments:
Post a Comment