Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete
akisoma makabrasha ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa AU unaofanyika
kwa siku mbili jijini Addis Ababa kuanzia leo Januari 30,2015.
Nyuma ya Mhe. Rais ni Waziri wa
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb). Waziri wa
Jinsia na Maendeleo ya Jamii, Mhe. Sophia Simba (Mb) na Balozi wa Tanznia
nchini Ethiopia, Mhe. Naimi Aziz (mwenye ushungi).
Na Ally Kondo, Addis Ababa.
Wakuu wa Nchi za Afrika wamekumbushwa kuwa, Mwaka 2015 umeingia lakini
Bara la Afrika bado linakabiliwa na changamoto nyingi ambazo kama hazitapatiwa
ufumbuzi ustawi wa bara hilo utaendelea kudumaa.
Kauli hiyo ilikuwa inarudiwa
mara kwa mara na viongozi waliopata fursa ya kuhutubia wakati wa ufunguzi wa
Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika jijini Addis Ababa siku
ya Ijumaa tarehe 30 Januari 2015.
Changamoto hizo ni pamoja na mabadiliko ya tabianchi, ugaidi, migogoro ya
kutumia silaha, ukatili wa kutisha, biashara haramu ya binadamu, umasikini na
mlipuko wa ugonjwa wa Ebola. Walishauri katika mwaka wa 2015 lazima matatizo
hayo yajadiliwe kwa kina kwa madhumuni ya kuyatafutia ufumbuzi wa kudumu.
Alipokuwa anahutubia mkutano huo, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa
Afrika, Mhe. Nkosazana Zuma alisema kuwa, licha ya changamoto hizo, Bara la
Afrika linapiga hatua kimaendeleo na kwamba Agenda 2063 inayowasilishwa katika
Mkutano huo inatoa wito kwa Serikali na sekta nyingine kushirikiana kwa pamoja
ili kukuza uchumi kwa kuweka mkazo kwenye ubunifu katika sekta ya kilimo,
usindikaji wa mazao na ujenzi wa miundombinu.
Mhe. Zuma alisisitiza umuhimu wa kutumia fedha za ndani kwa ajili ya
kugharamia miradi ya kipaumbele ambayo imezingatiwa katika Mpango wa Maendeleo
wa Miaka 10 ambao nao utawasilishwa katika mkutano huo.
Alieleza kuwa
Sekretarieti imefanyia kazi pendekezo la kutafuta vyanzo mbdala vya fedha
ambapo Mawaziri wa Fedha walijadili na ripoti yao itawasilishwa wakati wa
mkutano huo.
Umoja wa Afrika pia umeanzisha Mfuko Maalum utakaozinduliwa wakati
wa mkutano huo kwa ajili ya kuhifadhi fedha hizo.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe. Ban Ki-moon
alieleza kuwa mwaka 2014, AU na UN zilishirikiana kutafuta amani katika nchi
zenye migogoro.
Alisema mafanikio makubwa yalipatikana na hivyo kusisitiza kuwa
pande zilizosaini mikataba ya amani lazima zitekeleze vipengele vya mikataba
hiyo.
Alitoa mfano wa Mkataba wa Arusha na kusema kuwa pande zinazohusika
zitekeleze makubaliano ya kugawana madaraka.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa
kukitokomeza kikundi cha waasi cha FDLR kinachoendesha uasi wake Mashariki mwa
DRC.
Mhe. Ban Ki-moon pia aliwakemea viongozi wa Afrika wanaong’ang’ania
madaraka. Aliwashauri viongozi hao waache tabia hiyo na kuruhusu demokrasia
ichukue mkondo wake.
Rais wa Kikao cha 69 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ambaye pia ni
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uganda, Mhe. Sam Kutesa pamoja na mambo mengine,
alizungumzia mabadiliko ya mfumo katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Alisema katika uongozi wake atafanya jitihada kuhakikisha kuwa mfumo wa Baraza
hilo, chombo ambacho alikitaja kama kisichokuwa na demokrasia kuliko vyombo
vyote duniani unafanyiwa mabadiliko.
Viongozi hao pia walihimiza juhudi za kutafuta tiba na chanjo ya ugonjwa
wa Ebola na kusisitiza kuwa kampeni ifanywe ili nchi zilizoathirika na ugonjwa
huo zisamehewe madeni.
|
No comments:
Post a Comment