BUNGE LA BAJETI 2014/2015 TANZANIA:-Soma Vidokezo muhimu kuhusu Bajeti ya Wizara ya Ulinzi. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Tuesday, May 13, 2014

BUNGE LA BAJETI 2014/2015 TANZANIA:-Soma Vidokezo muhimu kuhusu Bajeti ya Wizara ya Ulinzi.


Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wameendelea kuchangia hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kutenga Taifa Dk. Hussein Mwinyi aliyoitoa jana. Vifuatavyo ni baadhi ya vidokezo vilivyochangiwa na waheshimiwa wabunge wa Bunge la 10 Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mkutano wake wa 15 kwenye kikao chake cha Saba-May 13,2014 Mjini Dodoma.

Wataalamu tunao, tumewatelekeza- Anna Abdalah.

MBUNGE wa Viti Maalum, Anna Abdalah amesema nchi imewatelekeza wataalamu mbalimbali waliopo jeshini, ambao wanakaa kambini wakiwa hawana kazi ya kufanya. Alisema baadhi ya zana za kivita zinaweza kutengenezwa katika sehemu kama Nyumbu, lakini kutokana na ukosefu wa fedha za kuendeshea kitengo hicho, matokeo yake askari hao wameendelea kukaa kambini bila kazi na hivyo kutotumika kwa vipaji vyao.

Aidha, mbunge huyo mkongwe alisema alama nyingi za mipakani ambazo ziliwekwa na Jeshi zimeondolewa na hivyo kutojulikana wapi ni wapi, hasa katika mipaka ya nchi jirani.

Wanaofariki nje hulipwa na nani?

Wabunge wamehoji juu ya askari wanaotumika kulinda amani katika baadhi ya nchi duniani, kwamba wanalipwa na nani kati ya serikali au Umoja wa Mataifa, kwani wanapokuwa huko, hutumika chini ya kofia ya UN.

Wametaka pia kujua idadi ya askari waliofariki dunia wakiwa katika utumishi huo nje ya nchi na kutaka kufahamishwa jinsi familia zao zinavyolipwa fidia.

Mbona fedha za Jeshi zinacheleweshwa?

WAbunge pia wamezungumzia suala la Wizara ya Fedha kushindwa kupeleka fedha za Wizara ya Ulinzi kwa wakati kwa visingizio kwamba fedha hakuna, wakati inajulikana kuwa fedha zipo.

Walisema ni jambo la hatari kwa nchi iwapo askari ambao hufanya kazi usiku na mchana kwa ajili ya kulilinda taifa lao, litachoka kusubiri fedha, wakitolea mfano kuwa mwaka jana walipokea kiasi cha asilimia 20 tu ya fedha zao za bajeti.

Masilahi ya wastaafu yaliliwa.

Kapteni Mstaafu wa Jeshi, John Chiligati amesema ulipwaji wa mafao ya askari wastaafu wa Tanzania hauko vizuri na kupendekeza nchi ijifunze kutoka India, kwani huko, licha ya kulipwa vizuri, lakini pia huwezeshwa kwa namna mbalimbali ili wasipate taabu katika maisha yao.

Alisema kwa vile askari hustaafu kulingana na vyeo vyao, wale wenye ujuzi wa aina mbalimbali, hutafutiwa kazi mbadala uraiani au kukopeshwa pesa na vyombo vya fedha ili waweze kujiajiri kwa kutumia taaluma zao uraiani.

Maonyesho ya Jeshi Dar yawagawa.

Katika michango hiyo ya wabunge, baadhi yao walitofautiana kuhusiana na maonyesho yaliyofanywa na Jeshi la Wananchi (JWTZ) wakati wa maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, yaliyofanyika katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam April 26 mwaka huu.

Mmoja wa wachangiaji hao alishangaa ni kwa namna gani Jeshi hilo liliweza kuanika silaha zake hadharani, kwani kwa kufanya hivyo, ni rahisi kwa adui kujua namna ya kukabiliana naye. Alikifananisha kitendo hicho na mtu kuonyesha kila kitu chake hadharani, ikiwemo nguo yake ya ndani.

Hata hivyo, wachangiaji wengine walisema maonyesho hayo ni jambo la kawaida na kwamba baadhi ya nchi kubwa nazo hufanya namna hiyo, wakizitaja kama China, India na Marekani.

Wahindi wapigwe marufuku Jeshini.

Mbunge mmoja alimtaka Waziri Mwinyi kuangalia uwezekano wa kuwaondoa wafanyabiashara wa Kihindi katika maduka makubwa yaliyo ndani ya kambi za kijeshi (Supermarkets) na kutaka kazi hiyo kupewa wazawa.

Huku akisisitiza kuwa hakuwa mbaguzi wa rangi, alisema kazi za kuendesha maduka hayo, tena ndani ya kambi za jeshi, inapaswa kufanywa na watanzania wazawa, hasa kwa ajili ya kuimarisha ulinzi.

Aidha, mbunge mwingine alishangaa na kuhoji kwa nini bei za bidhaa katika maduka ya jeshi zimekuwa sawa na maduka ya uraiani wakati kule jeshini kuna msamaha maalum wa kodi kiasi cha asilimia 18.


Hee, Tanzania ya 20 nguvu za kijeshi Afrika.

Katika hali isiyotarajiwa, mbunge mmoja alisema licha ya mbwembwe nyingi zilizoonyeshwa na Jeshi la Wananchi siku ya Muungano jijini Dar es Salaam, Tanzania ni ya 20 kwa majeshi yenye nguvu barani Afrika, kwa mujibu wa mitandao inayozungumzia nguvu za majeshi duniani (hakutaja mtandao huo).

Alisema katika mataifa yote duniani, Tanzania inashika nafasi ya 102 kwa nguvu za kijeshi, huku akiponda kuwa nchi yetu inazidiwa hata na nchi za Uganda na Rwanda ambazo zipo juu kimsimamo, kwa sababu ya kile alichosema serikali kushindwa kuipa wizara husika fedha za kutosha kuweza kujitosheleza.


Wanaopitia JKT, JKU janga la kitaifa.

Baadhi ya wabunge pia walisema kuwaacha bila kuwapa ajira vijana wanaomaliza mafunzo ya kijeshi katika majeshi ya JKT na JKU ni janga la kitaifa kwa sababu wanapofika uraiani na kukutana na ugumu wa maisha, wanaweza kufanya lolote ili kukabiliana na ugumu huo.

Walisema wakiwa wanafahamu kutumia aina mbalimbali za silaha, ni rahisi kwao kushawishika kwenda kushiriki matukio ya uhalifu, endapo atajitokeza mtu na kuwaeleza juu ya uwezekano wa kupata kiasi kikubwa cha fedha.

Kwa ajili hiyo, waliitaka wizara kuwapa kipaumbele vijana hao wanaomaliza mafunzo katika ajira, ikiwa ni njia ya kusaidia kuokoa vijana ili wasijihusishe na vitendo vya kihalifu.

Kupima Ukimwi iwe lazima JWTZ.

Mbunge mwingine alisema kwa kuwa vijana wa JWTZ wana jukumu kubwa la kuhakikisha mipaka ya nchi yetu inakuwa salama muda wote, wakati sasa umefika kwa kila anayetaka kuajiriwa, lazima apimwe afya yake ili kujiridhisha.

Alisema jambo hili linapaswa kuzingatiwa hasa kwa vile kama hali itaachwa iendelee hivi hivi, ipo siku taifa linaweza kujikuta likimpeleka mtu mgonjwa vitani, ambaye anaweza kufariki kabla ya kufika katika uwanja wa mapambano.

Aidha, walisema wanajeshi wanapata ugonjwa huo kutokana na kuachwa nyuma kwa wake au wapenzi wao wakati wanapohama kutoka kambi moja kwenda nyingine, kitu kinachowafanya wachepuke.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad