Imefahamika
kuwa tendo hili likifanyika ipasavyo husaidia kuondoa msongo wa mawazo, maradhi
ya moyo, maumivu ya kichwa yasiyokoma na kupunguza kasi ya saratani ya tezi
dume.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Sayansi
ya Tiba Muhimbili (Muhas), Dk Yahya Kishashu anasema inategemea tendo
linafanywa na nani na mhusika yupo kwenye mazingira gani.
“Kwa mfano,
tendo la ndoa linaondoa msongo wa mawazo iwapo unayetenda naye unampenda
na amekupa maandalizi mazuri. Sidhani
kama alimradi utende hilo tendo na yeyote litakusaidia,” anasema mtaalamu huyo.
Anaongeza
kuwa ndiyo maana baadhi ya watu wanatoka
nje ya ndoa zao kwa sababu si mara zote tendo la ndoa linawafurahisha wanandoa.
“Wakati
mwingine tendo hilo laweza kuwa karaha kwao,” anasema
Mazoezi
Si hivyo tu,
utafiti uliofanyika Canada hivi karibuni
umebainisha kuwa kufanya tendo la ndoa kwa kipindi cha dakika 25 kwa wanamume
kunachoma kalori 100 na kwa wanawake kalori 69.
Tendo hilo
likifanyika kwa nusu saa, linaweza kupunguza kalori za mwili kuliko kutembea
kwenye mashine ya mazoezi ya ‘treadmill’.
“Ni sawa na
kucheza mpira wa tenisi au kutembea ukipanda mlima kwa dakika 20 au kucheza
gofu kwa kasi kwa dakika 33 au zoezi la yoga kwa dakika 40,” sehemu ya utafiti
hiyo inasema.
Utafiti huo wa Canada ulishabihiana na
kampeni iliyofanywa na Taasisi ya Moyo
ya Uingereza ambayo ilisema kuwa dakika
30 za tendo la ndoa kwa siku ni muhimu kama mazoezi ya kutembea kwa mashine.
Kwa undani
zaidi utafiti huo ulichambua na kusema kuwa, tendo la ndoa, lina manufaa kwa moyo na mapafu.
Inaelezwa
kuwa vichocheo vinavyotoka baada ya tendo la ndoa vinasaidia kupunguza
kiwango cha msongo wa mawazo na kuongeza
uzalishaji wa seli mpya za ubongo.
Kuhusu mazoezi, Dk Kishashu anasema
anakubaliana na utafiti huo na kusema kuwa ni kweli tendo hilo linasaidia
kupunguza kalori, lakini linapofanyika mara nyingi zaidi linazeesha.
Hata hivyo,
wanasayansi wanalipa uzito mdogo tendo hilo katika muktadha wa ujenzi wa hisia
na mwili na kuwa halisisitizwi vya kutosha kama aina mojawapo ya mazoezi.
Tiba kwa
moyo, mapafu na ubongo
Inaelezwa
kuwa tendo la ndoa, linasaidia kuondoa msongo wa mawazo hivyo kupunguza hatari
ya maradhi ya moyo.
Si hivyo tu,
bali tendo hilo husaidia mapafu kufanya kazi yake vyema, kuingiza na kutoa hewa
chafu.
Kitaalamu,
upo mchakato uitwao ‘Neurogenesis’ ambao husaidia kulinda seli za ubongo
zinazokufa kutokana na uzee. Kuna eneo kwenye ubongo linaloitwa ‘hippocampus’
ambalo ni eneo linalotengeneza kumbukumbu.
“Kazi kubwa
inafanyika kwenye ubongo, wakati wa tendo la ndoa, kiasi kikubwa cha viamsha
raha huanzia kwenye ubongo na kuleta taarifa kwenye maeneo mengine ya mwili.
Ndiyo maana
watu wengi hupotea kiufahamu wakati wa kilele” anasema Dk Gosh, ambaye ni
mtafiti.
Hata hivyo,
wanaume ambao wanaendelea na tendo la ndoa mara kwa mara hadi wanapofikisha
miaka 50 na zaidi, kwa maana ya kutoa mbegu za kiume mara kumi kwa mwezi, wapo
katika hatari ndogo ya kupata saratani ya tezi dume. Inaelezwa kuwa mbegu za kiume hazitakiwi
kukaa mwilini kwa muda mrefu.Zinatakiwa zitolewe mara kwa mara ili kuzifanya
seli mpya zizalishwe. Ni kama kusafisha mpira, inasaidia kusitisha ujenzi wa seli
za zamani ambazo zaweza kuwa chanzo cha saratani.
Kwa
wanawake, tendo la ndoa husaidia kuundwa kwa misuli ya nyonga ambapo misuli
hiyo ikiwa imara huondoa hatari ya kushindwa kuzuia mkojo,(urine incotinence)
jambo linaloathiri mwanamke mmoja kati ya wanne wenye umri wa miaka zaidi ya
50.
“ Wakati wa
tendo la ndoa, kwa kawaida sakafu ya nyonga za mwanamke hubana na kuachia. Hii
husababisha misuli hiyo kuwa imara’ anasema mtafiti huyo.
Hata
hivyo, utafiti wa Chuo Kikuu cha Nottingham
nchini Uingereza unaeleza kuwa, wanaume wanaofanya tendo hilo na kumwaga
mbegu mara 20 hadi 30 kwa mwezi, wapo katika hatari ya kupata saratani ya tezi
dume kwa sababu ya umri wao .
Kuondoa
maumivu ya kichwa
Utafiti
mwingine umebaini kuwa, wanawake wenye umri mdogo hukumbwa na msongo wa mawazo
iwapo hawatafanya tendo la ndoa kwa muda mrefu.
Wanawake
hao, wanapofika kilele cha tendo hilo, damu hutembea kutoka kwenye ubongo, jambo ambalo huondoa maumivu ya kichwa.
Dk Innocent
Mosha, Mchunguzi wa magonjwa wa Hospitali ya Taifa Muhimbili anasema kuwa inawezekana kuwa tendo la ndoa likasaidia
kuondoa msongo wa mawazo iwapo mtu
hajalifanya kwa muda mrefu na yupo katika hali kubwa ya uhitaji.
“Kama mtu
hajafanya tendo hilo muda mrefu na hivyo amelikamia, basi akilifanya
litamwondolea msongo wa mawazo,” anasema
Anasema mtu ambaye anahitaji kufanya tendo
hilo na hajalipata, aghalabu huwa na msongo wa mawazo lakini kama huliwazi
hawezi kuwa na msongo.
Kwenye
utafiti huo, wanawake 83 wenye maradhi ya kichwa walipata nafuu kubwa baada ya
kumaliza tendo la ndoa.
Ukaribu/
Upendo
Mwanasaikolojia,
wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Modesta
Kimonga anasema ni kweli kuwa tendo la ndoa linaleta faraja inayoondoa msongo
wa mawazo.
Anasema hali hiyo inatokana na nadharia au mfumo wa uambatano katika
saikolojia au ‘attachement theory’
“Hii
‘attachment theory’ ipo kwa watoto wanaponyonya maziwa ya mama zao, na kwa watu
wazima ni kwenye tendo la ndoa ambalo linaleta faraja na ukaribu,” anasema.
Anaongeza: “Faraja hupatikana baada ya wanandoa kutenda
tendo hilo na huweza kuondoa kabisa mawazo kichwani au huzuni.”
Watafiti
walibaini kuwa vichocheo vya ‘oxtocin’ vinavyotolewa wakati wa tendo hilo
husaidia hisia za upendo na mshikamano kwenye uhusiano ya muda mrefu.
Lipo
ongezeko kubwa la kemikali ya ‘oxtocin’ kwa wanawake na wanaume baada ya
kumaliza tendo la ndoa ambalo husaidia kukuza uhusiano na ukaribu wao.
Wanaume
kulala baada ya tendo la ndoa
Utafiti wa
jarida la Sayansi ya Mishipa ya Fahamu
na Tabia uliochapishwa mwaka 2012 umebaini kuwa, dawa za usingizi hufanya kazi
sawa na tendo la ndoa kwa wanaume.
Eneo la mbele la ubongo ‘pre –frontal cortex’,
ambalo linahusiana na ufahamu, au
umakini wa kiakili, huzima au kufungwa baada ya kumaliza tendo hilo.
Kwa baadhi ya utafiti, wanaume kumaliza tendo la ndoa, ni sawa na kunywa dawa za usingizi za
‘diazepam’ zenye ukubwa wa miligramu mbili.
Pia,
vichocheo vinavyotoka baada ya tendo hilo kama ‘melatonin,’ ‘oxytocin’ na
‘vasopresin’, zinamsababisha mwanaume apate usingizi mzito.
Chanzo:-Mwananchi.
No comments:
Post a Comment