Madiwani wanane Bukoba wagonga mwamba kortini. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Thursday, February 27, 2014

Madiwani wanane Bukoba wagonga mwamba kortini.


Mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa wa Kagera, imewataka madiwani wanane waliofunguliwa kesi ya kupoteza sifa kuwasilisha hoja mpya za utetezi baada ya mahakama hiyo kutamka kuwa ina mamlaka kisheria kusikiliza shauri lao.
Madiwani hao kutoka vyama tofauti, waliweka pingamizi kuwa mahakama hiyo haikuwa na uwezo wa kusikiliza shauri lililofunguuliwa dhidi yao na Diwani wa Kata ya Kahororo, Chifu Kalumuna (CCM) kuwa hawana sifa za kuendelea kuwa madiwani.

Kalumuna, ambaye pia ni Mwenyekiti wa UVCCM Manispaa ya Bukoba na Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu, Afya na Uchumi alifungua shauri dhidi ya madiwani hao kuwa wamepoteza sifa za kuendelea kuwa madiwani kwa kushindwa kuhudhuria vikao vya kisheria bila taarifa.

Walalamikiwa katika kesi hiyo ni Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba, Diwani Yusuph Ngaiza (Kashai), Dauda Kalumuna (Ijuganyondo), Samwel Ruhangisa (Kitendagulo) na Deusdedith Mutakyahwa wa Kata ya Nyanga.

Wengine ni Richard Gaspar (Miembeni), Mulungi Kichwabuta (Viti Maalumu), Israel Mulaki (Kibeta) na Rabia Badru (Viti Maalumu).

Baada ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kusoma taarifa ya ukaguzi kwenye manispaa hiyo, madiwani walitakiwa kuanza vikao mara moja.

Hata hivyo, Kalumuna aliweka pingamizi dhidi ya madiwani hao kutohudhuria vikao mpaka itakaposikilizwa kesi ya msingi aliyofungua dhidi yao.

Baada ya mahakama kupitia hoja za mlalamikaji na walalamikiwa kupitia kwa mawakili wao, Hakimu wa mahakama hiyo, Charles Uisso alisema mahakama hiyo ina uwezo kisheria kusikiliza shauri lao na kutaka upande wa walalamikiwa kupeleka hoja nyingine za msingi kama zitakuwapo.

Upande wa walalamikiwa umetakiwa kuwasilisha hoja mpya za utetezi Machi 3, kwa uamuzi huo vikao vya Baraza la madiwani vitaendelea kusimama kusubiri uamuzi wa mahakama.

Walalamikiwa wanatetewa na Wakili Mathias Rweyemamu, huku mlalamikaji ukiwakilishwa na Wakili Aaron Kabunga.

Chanzo cha kesi hiyo ni mgogoro ambao umechukua muda mrefu na kusimama kwa maendeleo kati ya Mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagasheki na Meya wa Manispaa hiyo, Dk Anatoly Amani.

Habari na:-Mwananchi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad