Noah, Fuso zaua 10 mkoani Dodoma na Morogoro. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Tuesday, November 19, 2013

Noah, Fuso zaua 10 mkoani Dodoma na Morogoro.

Watu saba wamekufa papo hapo kwenye ajali mbaya iliyotoka jana (Novemba 18,2013)  katika kijiji cha Dakawa - Sokoine Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro.
 Ajali hiyo iliyohusisha gari ya abiria aina ya Noah yenye namba za usajili T 502 AUP iliyokuwa ikitoka Wilaya ya Gairo kuelekea Morogoro mjini kugongana uso kwa uso na lori aina ya Scania lenye namba za usajili T129 AGB ambalo lilikuwa likitoka Dar es Salaam kuelekea Tabora.
Watu 10 wamefariki dunia na wengine 18 kujeruhiwa katika ajali mbili zilizotokea katika Mikoa ya Dodoma na Morogoro jana (Novemba 18,2013).

Katika ajali ya Dodoma, watu saba wakiwamo wanaume sita na mwanamke mmoja, wamekufa papo hapo na watano kujeruhiwa, baada ya gari ndogo aina ya Noah waliyokuwa wakisafiria kutoka Gairo kwenda Morogoro, kugongana uso kwa uso na lori kisha kupinduka, katika eneo la Dakawa Ranchi , wilayani Mvomero.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, alisema gari hilo dogo liligongana na lori aina ya Scania lililokuwa likitokea Morogoro kwenda Dodoma.

Alisema ajali hiyo ilitokea saa 11:45 alfajiri ya jana na kwamba chanzo ni dereva wa gari ndogo aina ya Noah, Masoud Hamis, mkazi wa Kihonda, kujaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake na hivyo kukutana na lori hilo.

Dereva huyo ni miongoni mwa waliokufa katika ajali hiyo.

Mwananchi ilishuhudia Noah ikiwa imeharibika kwa kiasi kikubwa huku jitihada za kuisogeza kando ya barabara zikifanywa baada ya kuwatoa maiti na majeruhi.

Kamanda Shilogile alisema majeruhi wa ajali hiyo wamepelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro kwa matibabu, na miili ya waliokufa, imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali hiyo.

Waliofariki kwenye ajali hiyo ni Isack Mehele (25) mfanyakazi wa Kiwanda cha Tumbaku cha Alliance One cha mjini Morogoro.

Wengine ni, Sam Elisha (40), ambaye ni daktari wa Mimea, Maugo Salum (30), Sophia Hassan (20) na Adini Mwisholwa (70) wote wakazi wa Gairo.

Maiti mwingine ambaye ni mwanaume hajatambuliwa.

Majeruhi wametambuliwa kuwa ni, Juma Mohamed (21) mkazi wa Gairo, Hashim Ally Dafa (42) mkazi wa Lushoto, Junior Msenga, Selemani Hamis (20) mkazi wa Babati Manyara, Martin Msobi, mkazi wa Dumila, Festo Paulo mkazi wa Kimara Mwisho jijini Dar es Salaam na mwingine ambaye jina lake halikufahamika mara moja.

Daktari bingwa wa upasuaji katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Dk Francis Semwene, alisema hali za majeruhi wawili ni mbaya.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Wami Sokoine, Marco Ndesse, aliiomba Serikali kuweka matuta katika eneo hilo la makazi, ili kuepusha ajali.

Wakati huohuo, watu watatu wamefariki dunia na wengine 13 kujeruhiwa katika ajali ya gari iliyotokea katika Kijiji cha Gulwe, Wilaya ya Mpwapwa.

Ajali hiyo ilikuja baada ya lori kuacha njia na kuparamia kingo za daraja kabla ya kutumbukia katika korongo na kupinduka.

Mashuhuda walisema ilitokea saa 12.00 asubuhi na kuhusisha lori hilo lililokuwa limesheheni mizigo na watu waliokuwa wanakwenda mnadani.


Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Suzan Kaganda, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo iliyopoteza maisha ya Idd Mbelwa, Burhani Mzuza na mtu aliyefahamika kwa jina moja la Bakari. Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa, Mohamed Pathan, alisema hospitali yake ilipokea miili ya watu watatu na majeruhi 13.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad