Mtoto anayedaiwa kufariki miaka miwili iliyopita na kufanyiwa matanga aonekana akiwa hai * Wananchi wamiminika Hospitali ya Geita kumshuhudia. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Sunday, September 29, 2013

Mtoto anayedaiwa kufariki miaka miwili iliyopita na kufanyiwa matanga aonekana akiwa hai * Wananchi wamiminika Hospitali ya Geita kumshuhudia.

Mtoto Shabani Maulidi akiwa tayari melala kitandani katika hospitali ya wilaya ya Geita mkoani Geita ....
Habari/Picha Na:- Denice Stephano-Geita.
                         
Shabani akipelekwa wodini na wauguzi kupata matibabu zaidi katika Hospitali ya wilaya ya Geita mkoani Geita.

Penye mawe ni muonekano wa kabuli alilosadikiwa kuzikwa Shaban nyuma ya nyumba yao ambapo mtoto huyo anaelezwa ameonekana akiwa hai.

Wadogo zake na Shabani nao wakiwa wameshikwa na mshangao kama walivyokutwa  nyumbani kwao.
Mtoto anayedaiwa kufariki miaka miwili iliyopita  na kufanyiwa matanga ameonekana  akiwa hai  Septemba 28,mwaka huu majira ya mchana baada ya kukutana na mama yake mzazi uso kwa uso  wakati akienda kwenye shughuli zake za kibiashara.

Mtoto huyo  Shabani Maulidi (15) alifariki ,alishindwa kurudi nyumbani kwao tarehe 01.01.2011  wakati alipokuwa amepeleka Mbuzi machungani kisha kushindwa kurudi nyumbani na baadaye kuonekana baada ya siku tatu akiwa amefia kwenye kisima cha maji.

Kwa mujibu wa Baba mzazi wa mtoto huyo Bw. Maulid Shabani alisema mtoto wake hakurudi nyumbani siku hiyo,na waliendelea kumtafuta bila mafanikio na ndipo baada ya siku tatu walimkuta akiwa amefia ndani ya kisima cha maji kilicho maeneo ya Kijiji cha Nyankumbu Kitongoji cha Mwembeni wilayani Geita.

Baba huyo alisema baada ya hapo walitoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kisha waliruhusiwa kuuchukua mwili wa mtoto wao na kwenda kuuzika nyumbani kwao kitongoji cha 14 Kambarage ndani ya mji wa Geita.

Alisema walifanya shughuli zote za matanga na wakajua tayari mtoto wao ameishafariki na kwamba hawakuwa na wazo lolote na kumpata siku zote akiwa hai kama ilivyotokea  akisema ni tukio la kustaajabisha kwake.

Mama mzazi wa mtoto
Shabani menye kilemba
 kichwani akiwa amepigwa
 bumbuazi  akiwa
 maeneo ya hospitali.
Mama mzazi wa mtoto huyo Bi.Aziza Ramadhani akisimulia namna alivyokutana na mtoto wake alisema alikuwa akienda kwenye shughuli zake za ujasiriamali kama mfanyabiashara wa mbogamboga akiwa amefika eneo la Nyankumbu nje kidogo sana na mji wa Geita eneo la Mwembeni alikutana uso kwa uso na  mtoto wake.

Alisema alipomuona alimwita kwa jina lake akisema "mwanagu Shabani ni wewe naye akamwitikia ni mimi kisha alimshika mkono huku akiwa haamini macho yake ndipo alipompigia simu mumewe naye akaja wakamchunguza vizuri wakaabaini  kuwa ndiye mtoto wao Shabani aliyesadikiwa kuwa alifariki na kuzikwa.

Akithibitisha zaidi mama wa mtoto huyo alisema mwanae alikuwa na alama ya kinundu kwenye paji la uso na mguuni akiwa na alama ya kovu mguuni iliyosababishwa na kuchomwa na mwiba pia alikuwa na mwanya uliofanana na wa Baba yake mzazi.

Mtoto huyo aliyevuta hisia za watu wengi  mjini Geita ameendelea kuthibitishwa na walimu wake wa shule ya Msingi Mwatulole alikokuwa anasoma darasa la tano kabla ya kifo hicho cha utata kwa sasa.

Akiongea na Mwandishi wa Blog hii, Makamu mkuu wa shule ya msingi Mwatulole Bw.Joseph Nungula aliyekuwa akifuatilia kwa karibu tukio hilo alisema kweli mtoto huyo anaonekana ni yeye bila kutia shaka yoyote .

Mwalimu huyo alisema amemtambua mtoto huyo kwa sura na alama hasa ya usoni huku akimwelezea mtoto huyo kuwa alikuwa na mahudhurio mazuri shuleni pia maendeleo yake kitaaluma yalikuwa mazuri.

Mtoto huyo ambaye anaendelea kupewa huduma ya kitabibu katika Hospitali ya wilaya ya Geita kwa uchunguzi zaidi wa kiafya anaongea kwa shida wanapokuwepo watu watu wengi hata hivyo amemtambua Baba na mama yake mzazi ambapo wanapomuuliza baadhi ya maswali anawajibu.


Jeshi la Polisi mkoani Geita ambalo lilikuwa likifuatilia tukio hili kwa ukaribu sana limethibitisha kutokea kwa tukio hili huku wakiahidi kuendelea kutoa habari zaidi ambazo tutaendelea kuwajulisha huku Wananchi wakisubiri kibali cha Mahakama ili kufukua kaburi alililokuwa amezikwa mtoto huyo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad