Afya ya Mzee Mandela yazidi kudorora huku Wananchi wa Afrika Kusini na Dunia kwa jumla watakiwa kumwombea. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Tuesday, June 25, 2013

Afya ya Mzee Mandela yazidi kudorora huku Wananchi wa Afrika Kusini na Dunia kwa jumla watakiwa kumwombea.



Mzee Nelson Mandela.
Ikulu ya Afrika Kusini imetoa taarifa kuwa hali ya Rais wake wa zamani,Mzee Nelson Mandela imezidi kuwa mbaya katika siku mbili zilizopita.




Taarifa hiyo ilithibitishwa na Rais Jacob Zuma ambaye kwa mara ya kwanza alikiri hadharani kwamba hali ya afya ya Mzee Mandela ni mbaya na madaktari wanaendelea na juhudi za kuokoa maisha yake.



Zuma ambaye pia ni Rais wa Chama cha African National Congress (ANC), alikiri kufadhaishwa na hali ya kiongozi huyo wa zamani, alipomtembelea katika Hospitali ya Magonjwa ya Moyo ya Medi-Clinic mjini Pretoria na kuzungumza na mkewe, Graca Machel kuhusu hali yake.




Kumekuwa na taarifa kwamba tangu alipofikishwa hospitali, Mzee Mandela amekuwa hajitambui na amekuwa akipumua kwa msaada wa mashine.




Pia, kumekuwa na ulinzi mkali katika hospitali hiyo alikolazwa huku waandishi wa habari na watu wasiokuwa wanafamilia wakizuiwa kwenda kumwona.




Ilielezwa pia kwamba ulinzi ulizidi kuimarishwa jana(Juni 24,2013) katika maeneo yanayozunguka hospitali hiyo.





Rais Mstaafu wa Afrika Kusini, Bw.Thabo Mbeki  amewatoa hofu wananchi wa nchi hiyo kuwa Mzee Mandela anaendelea vizuri, ingawa katika siku za hivi karibuni amekuwa akipelekwa hospitali mara kwa mara kwa ajili ya kutibiwa.




Rais Mbeki aliyemrithi Mandela mwaka 1999, alisema kuwa ni vizuri wananchi wakadumisha sala kwa kumwombea mzee huyo badala ya kukata tamaa na kuamini uvumi kwamba ameshafariki dunia.





Chama cha ANC, Jumamosi iliyopita, kilitoa tamko kuwa Mzee Mandela inabidi aheshimiwe na kwamba siyo kila mtu anaweza kuwa msemaji wa maendeleo ya afya yake.




Taarifa hiyo ilieleza kuwa Ikulu ya Afrika Kusini inabidi ifanye kazi vizuri kuhakikisha wananchi wanapata taarifa za kweli na zenye uhakika kuhusu kiongozi huyo aliyeiongoza nchi hiyo kuanzia mwaka 1994 mpaka 1999.




Chama chetu cha The African National Congress kwa mara nyingine kinataka pande zinazohusika zifanye kazi yake. Vilevile tunataka vyombo vya habari na familia, kuheshimu taarifa za faragha kuhusu Mandela.”





Msemaji wa chama hicho, Jackson Mthembu aliwataka wananchi wa Afrika Kusini na dunia kwa jumla kuwaombea Mandela, ndugu zake na madaktari.




Mzee Mandela ambaye mwezi ujao anatarajiwa kutimiza umri wa miaka 95, kwa muda mrefu sasa anasumbuliwa na tatizo la mapafu kujaa maji.



Hatua hiyo imesababisha simanzi na majonzi kwa wananchi wa Afrika Kusini ambao wamekuwa wakimwombea na kutoa salamu za kumtakia afya njema.




Habari zinasema kuwa tatizo la mapafu, ni matokeo ya athari alizozipata akiwa gerezani kipindi alipofungwa miaka 27 jela katika miaka ya 1900.





Mzee Mandela amekuwa kielelezo chema siyo tu kwa Afrika Kusini, bali Afrika na duniani kote. Nasi Watanzania kila mtu kwa imani yake ni vema kumuombea salama ili Mungu ampe nafuu na kumponya maradhi yanayomsibu kwa sasa.




Mzee Mandela alilazwa katika Hospitali ya Moyo ya Medi-Clinic, Juni 8, mwaka huu kutokana na maradhi ya homa ya mapafu yanayomsumbua na iliripotiwa kwamba tangu wakati huo hajitambui.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad