Serikali ya Tanzania
imesema itachukua hatua kali za kisheria kwa atakayebainika kutumia vibaya simu
za mkononi, na mitandao ya kijamii kuleta uchochezi au kwenda kinyume na
maadili ya nchi.
Kauli hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki na
Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa
alipozungumza na waandishi wa habari na kusema kuwa lengo la kufanya hivyo ni
kutaka kukomesha vitendo hivyo.
“Hatua hizo
zitachukuliwa dhidi ya kampuni au mtu yeyote atakayetoa kashfa na kuitukana
serikali, viongozi wa serikali, dini, siasa na watu binafsi,” alisema na
kuongeza kuwa vitendo hivyo vinakiuka sheria za nchi.
Alisema
hatua hizo pia zitawakumba watu wote wanaojihusisha na uonyeshaji wa picha za
ngono kwenye mitandao, unyanyasaji wa watoto na ukiukaji wa maadili na kutoa
taarifa zenye lengo la kuvunja utulivu na amani.
“Matumizi mabaya ya teknolojia
ya habari na mawasiliano (TEHAMA) kama simu za mikononi, barua pepe, na
mitandao ya kijamii yanafanywa na watu wachache kwa kusambaza taarifa zenye nia
ya kuchafua taifa letu,” alisema.
Alisema
pamoja na kwamba teknolojia hiyo katika miaka ya karibuni imechangia kuleta
maendeleo makubwa nchini, baadhi ya watu wanaitumia kwa mambo yasiyofaa.
Aliendelea kusema kuwa watu wengine wamekuwa wakiitumia kwa kufanya wizi,
ujambazi, ubakaji, biashara ya dawa za kulevya na ukahaba na kusambaza siri za
watu binafsi bila idhini ya wahusika.
Aidha,
alisema pia hatua kali zitachukuliwa kwa wakala au kampuni ya simu yoyote
itakayouza SIM card kwa mtu yeyote bila ya kuwa na kitambulisho
kinachotambulika kisheria.
Alisema pia ni kosa la jinai kutoa taarifa za uongo
wakati wa usajili wa SIM card na serikali imejipanga kuzima zote ambazo
hazijasajiliwa.
No comments:
Post a Comment