Big mechi ya Jiji la Dar es Salaam kati ya Watani wa Jadi, Simba na Yanga yamalizika kwa sare ya bao 1-1 , Bahanuzi akiwaokoa Yanga kulala kwa mtani wake. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, October 03, 2012

Big mechi ya Jiji la Dar es Salaam kati ya Watani wa Jadi, Simba na Yanga yamalizika kwa sare ya bao 1-1 , Bahanuzi akiwaokoa Yanga kulala kwa mtani wake.



Mabingwa wa soka Africa Mashariki na kati ,Timu ya Yanga imelazimisha  matokeo ya sare ya kufungana bao 1-1 na wapinzani wao wa jadi,ambao ni Mabingwa watetezi wa Ligi kuu,Timu ya  Simba SC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, uliopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kuanzia saa 1:02 usiku.


Yanga ambao walimaliza mechi hiyo wakiwa pungufu baada ya Simon Msuva kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 77 kwa kumrudishia rafu Juma Nyosso, ndio waliohaha kusawazisha bao, baada ya kutanguliwa kwa bao la mapema la kiungo Amri Kiemba dakika 4 tu ya mchezo baada ya kupokea pande zuri toka kwa Mwinyi Kazimoto.


SIMBA: Juma Kaseja, Nassor Chollo, Paul Ngalema, Juma Nyosso, Shomary Kapombe, Jonas Mkude/Haruna Moshi, Amri Kiemba, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Edward Christopher/Daniel Akuffo na Mrisho Ngassa.


Simba walicheza vizuri kipindi chote cha kwanza wakigongeana pasi za uhakika na kuwazidi kasi uwanjani wapinzani wao, wakati Yanga pamoja na kuzinduka baada ya kufungwa bao, lakini makosa yalikuwa mengi.


Pasi zao zilikuwa nyingi hazifiki, walikuwa wanapokonyeka mipira kirahisi, wanazidiwa nguvu na wapinzani wao katika kugombea mipira na hata mashambulizi yao hayakuwa ya mpangilio, zaidi ya kuonekana kubahatisha zaidi huku Mbuyu Twite alifumua shuti zuri dakika ya 38 kutoka wingi ya kulia, ambalo lilitoka nje sentimita chache.  

  
Kabla hata ya dakika 45 za kipindi cha kwanza kumalizika, kocha Mholanzi Ernie Brandts alimtoa Hamisi Kiiza na kumuingiza Frank Domayo ili kuimarisha safu ya kiungo, ambayo ilionekana kuzidiwa na Simba inayofundishwa na Mserbia, Milovan Cirkovick.


YANGA: Yaw Berko, Mbuyu Twite, Stefano Mwasyika, Nadir Cannavaro, Kevin Yondan/Juma Abdul, Athumani Iddi, Simon  Msuva, Haruna Niyonzima, Said Bahanuzi, Hamisi Kiiza/Frank Domayo na Nizar Khalfan/Didier Kavumbangu.



Kipindi cha pili, Yanga walianza na mabadiliko, kocha Ernie Brandts akimtoa kiungo Nizar Khalfan na kumuingiza mshambuliaji Didier Kavumbangu, ambaye alikwenda kuongeza nguvu ya safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.


Katika dakika ya 63, beki Paul Ngalema aliunawa mpira katika harakati za kuokoa na refa Mathew Akrama akaamuru penalti, ambayo ilikwamisha kimiani kiufundi na Said Bahanuzi ‘Spider Man’.





Katika dakika ya 77 Mathew Amkrama alimtoa nje kwa kadi nyekundu ya moja kwa moja Simon Msuva, baada ya kumkita Juma Nyosso, aliyemkanyaga ‘kwa bahati mbaya’. 

Msuva alichezewa rafu na Nyosso na tayari refa alikwishapuliza filimbi na kumpa kadi ya njano beki huyo wa Simba, lakini kiungo huyo wa Yanga akaponzwa na hasira za kitoto.


Bahanuzi anafunga penalti.

Aidha  kocha wa Simba, Milovan amesema kwamba ulikuwa mchezo mzuri na Yanga walicheza vizuri, lakini timu yake ilicheza vizuri na anajivunia.
Amesema  Yanga imeimarika tofauti na ilivyokuwa awali na kwamba hizo ni dalili Ligi Kuu msimu huu itakuwa ngumu.


Kwa upande wake, kocha wa Yanga, mwanzoni hawakucheza vizuri, lakini baadaye walitulia na kucheza vizuri. “Hii ni mechi ya kweli ya upinzani, unaweza kuona rafu na kadi nyingi,”alisema Brandts.



Kwa matokeo hayo, Simba imefikisha pointi 13, ndani ya mechi tano na kuendelea kuongoza Ligi Kuu, wakati Yanga imefikisha pointi nane na kubaki nafasi ya tano, kwani Coastal Union imetoa sare ya 2-2 na JKT Oljoro mjini Arusha na kufikisha pointi tisa.    
 


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad