na
Happiness Mtweve.
Jakaya Kikwete |
Hatimaye
Panga la Mwenyekiti wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, limewashukia vigogo wa chama hicho na
kuwatupa nje ya kinyang’anyiro cha kuwania nafasi za uongozi wa jumuiya za
chama na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC).
Wakati
panga hilo likiwashukia baadhi ya vigogo, Rais Kikwete ametoa kauli nzito ya
kutaka wagombea waliopata kutoa kauli za vitisho dhidi ya chama hicho kufanya
kile walichokusudia kukifanya.
Kikwete
katika kauli yake hiyo alionekana waziwazi kukerwa na kauli za ‘patachimbika’
au zile za kutishia kujitoa na kujiunga na vyama vya upinzani.
Akizungumza
kwa ukali, Kikwete ambaye juzi alitamba akisema CCM haitakufa kama
inavyotabiriwa na baadhi ya watu, alihitimisha kauli yake kwa kusema watu wenye
kauli za namna hiyo walikuwa hawafai kuendelea kuwa wanachama wa chama hicho.
Panga
la Rais Kikwete limewaangukia wagombea wenye nyadhifa zaidi ya moja serikalini
na ndani ya chama pamoja na baadhi ya wabunge.
Wengine
waliokatwa na vikao hivyo vya juu vya CCM vilivyomalizika jana mjini Dodoma, ni
wagombea waliokuwa wakiibua malumbano na wakati mwingine kuikosoa CCM
hadharani, makada waliojipambanua kama wapiganaji na wapambanaji wa ufisadi na
baadhi ya wabunge walioweka saini zao bungeni kuunga mkono hoja ya Mbunge wa
Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ya kutaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ajiuzulu.
Baadhi
ya wajumbe wa NEC wakiwa ukumbini kwenye kikao cha NEC mjini Dodoma.
|
Habari
kutoka ndani ya NEC, ziliwataja walioenguliwa kuwa ni pamoja na Mbunge wa
Nzega, Dk. Hamisi Kigwangalla na Mjumbe wa Baraza Kuu la Vijana la CCM Taifa
(UVCCM), Hussein Bashe.
Bashe
na Kigwangalla ambao wamekuwa katika mvutano mkubwa wa kusaka madaraka ndani ya
chama, majina yao yalipendekezwa kukatwa kuwania nafasi hiyo kuanzia kwenye
sekretarieti, Kamati ya Maadili na Kamati Kuu kabla ya kuthibitishwa na NEC.
Makada
hao wamekuwa kwenye mvutano wa kisiasa uliodumu toka mwaka 2010 wakati wa
uchaguzi mkuu ambapo Bashe alienguliwa kuwania ubunge, Jimbo la Nzega na nafasi
yake kuchukuliwa na Dk. Kigwangalla aliyeshika nafasi ya tatu. Nafasi ya pili
ilichukuliwa na mbunge wa zamani wa jimbo hilo, Lucas Selelii.
Mbali
ya hao, panga hilo limemkata Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja
na Mbunge wa Kahama, James Lembeli.
Mgeja
na Lembeli nao wamekuwa katika mvutano mkubwa ndani na nje ya chama. Uhasama
wao unachochewa na kambi mbili kubwa zenye uhasama mkubwa.
Wengine
waliokatwa ni Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina na Mbunge wa Ludewa, Deo
Filukunjombe.
Wabunge
hao ni miongoni mwa waliotia saini kutaka Waziri Mkuu Pinda ang’oke. Duru za
siasa zinasema kuwa msimamo wa wabunge hao kuhusu Pinda, ndio ulisababisha wakatwe
kuwania NEC.
Mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Samwel Sitta akimsalimia kwa unyenyekevu
Mjumbe mwenzake, Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya, nje ya ukumbi, kabla ya
kikao cha NEC mjini Dodoma.
|
Athari
za saini za kutaka kumng’oa Pinda ambazo zilisababisha Baraza la Mawaziri
lipanguliwe na kuundwa upya, zimeonekana pia kumgusa Mbunge wa Musoma Vijijini,
Nimrod Mkono, ambaye ametupwa nje kuwania nafasi ya uenyekiti wa wazazi CCM taifa.
Mkono
ambaye ni wakili maarufu nchini, jina lake pia ni miongoni mwa majina
yaliyokatwa katika vikao vya ngazi za chini na hivi karibuni alitahadharisha
kuwa endapo hatarejeshwa na NEC, patachimbika.
Mbunge
wa zamani wa Nyamagana, Antony Diallo na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza
aliyekuwa akitetea nafasi yake, Clement Mabina nao wamekatwa.
Akizungumza
baada ya kufanya maamuzi hayo magumu, Rais Kikwete alisema anashangaa kuona
baadhi ya wagombea wa nafasi mbalimbali ndani ya chama hicho wakitaka kuuana
kuingia NEC na kugeuza uchaguzi huo kuwa uwanja wa mapambano na kuwa na ndimi
mbili.
Alisema
hivi sasa wagombea wengi wamekuwa wakijitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi
ndani ya CCM na kung’ang’ania kupata ushindi kiasi cha wengine kufikia hatua ya
kutoa kauli za vitisho kwa kusema wasipopata nafasi ‘patachimbika’.
“Inashangaza
kuona kugombea NEC tu watu wanataka kuuana, wanakimbilia nini huko ndani?”
alihoji Rais Kikwete.
“Ina
maana watu hawa wanaonyesha dhahiri kuwa hawana nia njema na chama, bali
wanaingia kwa maslahi yao binafsi, hivyo tuna kila sababu ya kuwakataa ili
tujenge timu ya ushindi ambayo ndiyo nia yetu,” aliongeza mwenyekiti huyo.
Alitumia
nafasi hiyo kuwataka wanachama kutogeuza uchaguzi huo kuwa uwanja wa fujo kwa
kutumia silaha, majembe, ngumi na mikuki kwani hiyo ni fedheha kubwa kwa chama
hicho.
Rais
Kikwete alisema kama kuna wagombea ambao watajitoa ndani ya CCM na kuhamia
chama kingine kutokana na majina yao kutopendekezwa, wajitoe.
“Hatuchagui
wagombea wenye ndimi mbili ambao wanasema kama hatutapitishwa tutahamia chama
kingine, hao tunawatakia kila la heri waende tu, kwani hawana nia njema na
chama hiki,” alisema.
wajumbe wa NEC |
Mwenyekiti
huyo ambaye alikuwa akizungumza kwa ukali, alisema anajua suala la kuwaengua
baadhi ya wagombea litazua mjadala, lakini nia ya chama ni njema katika kuleta
sura mpya na uhai.
“Kufanya
hivyo ni pamoja na kupata viongozi watakaokiletea chama ushindi katika chaguzi
za Serikali za Mitaa 2014 pamoja na Uchaguzi Mkuu mwaka 2015, hivyo lazima watu
hao watambue kuwa kazi wanayoifanya ni kuunda timu ya ushindi wa chama na si wa
watu.
“Najua
kuna ndugu na marafiki ambao hawatateuliwa kutokana na kujaa kwa nafasi na
mapungufu na madhaifu ambayo yalionekana baada ya Kamati ya Maadili kupitia
majina yao, hivyo wasione kama wameonewa bali wajue kama ndio utaratibu wa
chama wa kuhitaji viongozi shupavu, hodari na mwenye uwezo wa kukitetea na
kukipigania chama na kukipa ushindi,” alisema Rais Kikwete.
Aliwatahadharisha
wagombea watakaotumia rushwa kwenye kampeni zao watambue kuwa Taasisi ya Kuzuia
na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wanafanya kazi yao muda wote, hivyo
atakayekamatwa asije akamlaumu mtu.
Chanzo
:Tanzania daima.
No comments:
Post a Comment