Kamati kuu cha Chama cha Mapinduzi CCM yawaengua wagombea wakongwe na kutoa nafasi kwa vijana huku Mwenyekiti wake taifa Jakaya Kikwete akisema anayetaka kuondoka CCM ‘ruksa’ - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, September 26, 2012

Kamati kuu cha Chama cha Mapinduzi CCM yawaengua wagombea wakongwe na kutoa nafasi kwa vijana huku Mwenyekiti wake taifa Jakaya Kikwete akisema anayetaka kuondoka CCM ‘ruksa’


  Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, kabla ya kikao cha NEC, leo mjini Dodoma. Wengine, waliokaa. Kutoka kushoto ni Mawaziri Wakuu wa zamani, John Malecela na Cleopa Msuya, Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama,  Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Pius Msekwa, Rais wa Zanzibar  Dk. Ali Mohamed Sheni, Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi na Kulia ni Mawaziri wakuu wa zamani Frederick Sumaye na Edward Lowassa.



na Happiness Mtweve.


Jakaya Kikwete
Hatimaye  Panga la Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, limewashukia vigogo wa chama hicho na kuwatupa nje ya kinyang’anyiro cha kuwania nafasi za uongozi wa jumuiya za chama na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC).


Wakati panga hilo likiwashukia baadhi ya vigogo, Rais Kikwete ametoa kauli nzito ya kutaka wagombea waliopata kutoa kauli za vitisho dhidi ya chama hicho kufanya kile walichokusudia kukifanya.


Kikwete katika kauli yake hiyo alionekana waziwazi kukerwa na kauli za ‘patachimbika’ au zile za kutishia kujitoa na kujiunga na vyama vya upinzani.


Akizungumza kwa ukali, Kikwete ambaye juzi alitamba akisema CCM haitakufa kama inavyotabiriwa na baadhi ya watu, alihitimisha kauli yake kwa kusema watu wenye kauli za namna hiyo walikuwa hawafai kuendelea kuwa wanachama wa chama hicho.


Panga la Rais Kikwete limewaangukia wagombea wenye nyadhifa zaidi ya moja serikalini na ndani ya chama pamoja na baadhi ya wabunge.


Wengine waliokatwa na vikao hivyo vya juu vya CCM vilivyomalizika jana mjini Dodoma, ni wagombea waliokuwa wakiibua malumbano na wakati mwingine kuikosoa CCM hadharani, makada waliojipambanua kama wapiganaji na wapambanaji wa ufisadi na baadhi ya wabunge walioweka saini zao bungeni kuunga mkono hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ya kutaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ajiuzulu.



Baadhi ya wajumbe wa NEC wakiwa ukumbini kwenye kikao cha NEC mjini Dodoma.


Habari kutoka ndani ya NEC, ziliwataja walioenguliwa kuwa ni pamoja na Mbunge wa Nzega, Dk. Hamisi Kigwangalla na Mjumbe wa Baraza Kuu la Vijana la CCM Taifa (UVCCM), Hussein Bashe.


Bashe na Kigwangalla ambao wamekuwa katika mvutano mkubwa wa kusaka madaraka ndani ya chama, majina yao yalipendekezwa kukatwa kuwania nafasi hiyo kuanzia kwenye sekretarieti, Kamati ya Maadili na Kamati Kuu kabla ya kuthibitishwa na NEC.


Makada hao wamekuwa kwenye mvutano wa kisiasa uliodumu toka mwaka 2010 wakati wa uchaguzi mkuu ambapo Bashe alienguliwa kuwania ubunge, Jimbo la Nzega na nafasi yake kuchukuliwa na Dk. Kigwangalla aliyeshika nafasi ya tatu. Nafasi ya pili ilichukuliwa na mbunge wa zamani wa jimbo hilo, Lucas Selelii.


Mbali ya hao, panga hilo limemkata Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja na Mbunge wa Kahama, James Lembeli.


Mgeja na Lembeli nao wamekuwa katika mvutano mkubwa ndani na nje ya chama. Uhasama wao unachochewa na kambi mbili kubwa zenye uhasama mkubwa.


Wengine waliokatwa ni Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina na Mbunge wa Ludewa, Deo Filukunjombe.


Wabunge hao ni miongoni mwa waliotia saini kutaka Waziri Mkuu Pinda ang’oke. Duru za siasa zinasema kuwa msimamo wa wabunge hao kuhusu Pinda, ndio ulisababisha wakatwe kuwania NEC.



Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Samwel Sitta akimsalimia kwa unyenyekevu Mjumbe mwenzake, Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya, nje ya ukumbi, kabla ya kikao cha NEC mjini Dodoma.


 Athari za saini za kutaka kumng’oa Pinda ambazo zilisababisha Baraza la Mawaziri lipanguliwe na kuundwa upya, zimeonekana pia kumgusa Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono, ambaye ametupwa nje kuwania nafasi ya uenyekiti wa wazazi CCM taifa.


Mkono ambaye ni wakili maarufu nchini, jina lake pia ni miongoni mwa majina yaliyokatwa katika vikao vya ngazi za chini na hivi karibuni alitahadharisha kuwa endapo hatarejeshwa na NEC, patachimbika.


Mbunge wa zamani wa Nyamagana, Antony Diallo na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza aliyekuwa akitetea nafasi yake, Clement Mabina nao wamekatwa.


Akizungumza baada ya kufanya maamuzi hayo magumu, Rais Kikwete alisema anashangaa kuona baadhi ya wagombea wa nafasi mbalimbali ndani ya chama hicho wakitaka kuuana kuingia NEC na kugeuza uchaguzi huo kuwa uwanja wa mapambano na kuwa na ndimi mbili.


Rais Kikwete alitoa kauli hiyo mjini hapa jana wakati akifunga kikao cha NEC.


Alisema hivi sasa wagombea wengi wamekuwa wakijitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya CCM na kung’ang’ania kupata ushindi kiasi cha wengine kufikia hatua ya kutoa kauli za vitisho kwa kusema wasipopata nafasi ‘patachimbika’.


“Inashangaza kuona kugombea NEC tu watu wanataka kuuana, wanakimbilia nini huko ndani?” alihoji Rais Kikwete.


Ina maana watu hawa wanaonyesha dhahiri kuwa hawana nia njema na chama, bali wanaingia kwa maslahi yao binafsi, hivyo tuna kila sababu ya kuwakataa ili tujenge timu ya ushindi ambayo ndiyo nia yetu,” aliongeza mwenyekiti huyo.


Alitumia nafasi hiyo kuwataka wanachama kutogeuza uchaguzi huo kuwa uwanja wa fujo kwa kutumia silaha, majembe, ngumi na mikuki kwani hiyo ni fedheha kubwa kwa chama hicho.


Rais Kikwete alisema kama kuna wagombea ambao watajitoa ndani ya CCM na kuhamia chama kingine kutokana na majina yao kutopendekezwa, wajitoe.


Hatuchagui wagombea wenye ndimi mbili ambao wanasema kama hatutapitishwa tutahamia chama kingine, hao tunawatakia kila la heri waende tu, kwani hawana nia njema na chama hiki,” alisema.


wajumbe wa NEC
Mwenyekiti huyo ambaye alikuwa akizungumza kwa ukali, alisema anajua suala la kuwaengua baadhi ya wagombea litazua mjadala, lakini nia ya chama ni njema katika kuleta sura mpya na uhai.


“Kufanya hivyo ni pamoja na kupata viongozi watakaokiletea chama ushindi katika chaguzi za Serikali za Mitaa 2014 pamoja na Uchaguzi Mkuu mwaka 2015, hivyo lazima watu hao watambue kuwa kazi wanayoifanya ni kuunda timu ya ushindi wa chama na si wa watu.


“Najua kuna ndugu na marafiki ambao hawatateuliwa kutokana na kujaa kwa nafasi na mapungufu na madhaifu ambayo yalionekana baada ya Kamati ya Maadili kupitia majina yao, hivyo wasione kama wameonewa bali wajue kama ndio utaratibu wa chama wa kuhitaji viongozi shupavu, hodari na mwenye uwezo wa kukitetea na kukipigania chama na kukipa ushindi,” alisema Rais Kikwete.


Aliwatahadharisha wagombea watakaotumia rushwa kwenye kampeni zao watambue kuwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wanafanya kazi yao muda wote, hivyo atakayekamatwa asije akamlaumu mtu.


Chanzo :Tanzania daima.
 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad