Picha/Habari:Tumaini Fung Yajenga Visima vya Maji Wilayani Ngara/Kagera. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, February 01, 2017

Picha/Habari:Tumaini Fung Yajenga Visima vya Maji Wilayani Ngara/Kagera.

Mmoja wa wahisani wa kanisa la Anglikana Dayosis ya Kagera kutoka kisiwa cha Gumsey nchini Uingereza Paul Smith akimtwisha ndoo ya maji Jovina John mkazi wa kijiji cha Kasharaza wilayani Ngara mkoani Kagera baada ya kutembelea mradi wa maji jana akiambatana na wenzake kutoka nchini Canada.


Baadhi ya wafadhili   kutoka nchini Uingereza na Canada kupitia  kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kagera, wakifurahia matumizi ya fedha zao za kujenga miradi ya maji wilayani Ngara ambapo jana walitembelea kisima cha maji cha kijiji cha Kasharazi wilayani humo.

Picha na habari kwa Hisani ya Shaaban Ndyamukama

Kanisa la Anglikana  dayosisi ya Kagera limejenga visima vya maji 16 kwa mwaka 2016  katika vijiji mbalimbali wilayani Ngara vyenye thamani ya Sh 90.6 milioni ili kuwapatia wananchi huduma ya maji safi   kuwaepusha na magonjwa ya matumbo baada ya kutumia maji ya mito na madimbwi wilayani humo

Visima hivyo vimefadhiliwa na Marafiki wa kanisa hilo kutoka nchini Canada na Uingereza ambapo wananchi  huchangia asilimia 20 ya rasilimali zinazowazunguka ikiwa ni pamoja na kutumia nguvu zao kujenga visima hivyo kwa kushirikisha kamati za maji na serikali za vijiji .

Mratibu wa mfuko wa Tumaini ulio chini ya kanisa la Anglikana  wilaya ya Ngara Bw Alex Nyamkara, amebainisha hayo jana wakati wafadhili wa kanisa hilo  walipotembelea miradi ya maji katika vijiji vya Kasharazi, Nyamahwa, Nyakisasa, Kibirizi na Kanyinya wilayani Ngara.

Bw.Nyamkara alisema ujenzi wa kisima kimoja  hugharimu Sh 5.64 milioni na kwamba wananchi wengi  hutumia maji ya mito na madimbwi kwa kuchanganyikana na  wanyama wa aina mbali mbali na kusababisha magonjwa ya matumbo, kuharisha na homa za vipindi kwa watoto chini ya  umri wa miaka mitano.

Alisema kata ambazo zimenufaika na miradi ya maji kupitia kanisa hilo ni Ntobeye, Muganza Nyamiaga, Bukiriro, Mbuba, Nyakisasa , Kibogora na Kanazi na kwamba mfuko wa tumaini hutoa mafunzo kwa wajumbe wa kamati za  maji ili kuhifadhi vyanzo na mazingira vinapojengwa visima kwa kukarabati miundombinu ya maji

Aidha alisema kwa mwaka huu wameomba wafadhili  kuwaongezea fedha za kujenga visima 13 katika kata zenye mahitaji makubwa ya maji kama Keza, Murusagamba, Rusumo,Kasulo na Kabanga ili kuwawezesha wananchi kupata unafuu wa huduma baad ya miradi ya maji ya Benki ya dunia kukwama kukamilika

Tunachohimiza wananchi ni kutunza miradi ya maji kwa kuwa ni mali yao si ya Tumaini Fund na ikiboreshwa wanaweza kunufaika nayo kwa muda mrefu na kuwashawishi wafadhili kuwaongezea miradi mingine” Alisema Nyamkara

Wakati huo huo  alisema wafadhili hao walitoa fedha za kuwajengea nyumba wajane na wagane  wanaoishi na watoto yatima katika mazingira magumu ambapo na  mwaka jana zilijengwa nyumba 28 zenye thamani ya Sh 70 milioni na mwaka mwaka huu zitajengwa nyumba 17 zenyethamani ya Sh 42.5 milioni.

Hata hivyo mmoja wa wafadhili wa kanisa hilo kutoka nchini Canada, Linda Winey aliwahimiza  wachungaji na waumini mbalimbali katika vijiji alivyotembelea kumtumainia Mungu kwa kufanya kazi kwa bidii wakitumia juhudi na maarifa  ili kuboresha maisha yao.

Wafadhili hao walisema walitembelea wilaya ya Ngara katika shughuli za kiroho lakini  wananchi wa  Tanzania wanakabiliwa na ugumu wa maisha hivyo kunahitajika uboreshaji wa muiundombinu na mazingira  katika utoaji huduma bora za kijamii hasa maji, Afya, elimu na makazi kwa wasiojiweza kiuchumi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad