Rais Magufuli:..Mahusiano ya kiuchumi na kibiashara kati ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ulaya (EPA) hadi Januari 2017. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Friday, September 09, 2016

Rais Magufuli:..Mahusiano ya kiuchumi na kibiashara kati ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ulaya (EPA) hadi Januari 2017.


Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli  akiongoza mkutano wakati wa Mkutano wa 17 wa Dharura wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu jijini Dar es salaam ,Septemba 8, 2016. 

Anafuatiwa na Rais Paul Kagame wa Rwanda, Mwakilishi maalum wa Rais wa Sudan ya Kusini Mhe Aggrey Tisa Sabuni, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Ali Mohamed Shein na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Balozi Liberat Mfumukeko.

Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wamekubaliana kutumia kipindi cha miezi 3 hadi Januari mwakani ili kuupitia upya mkataba wa mahusiano ya kiuchumi na kibiashara kati ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ulaya (EPA) kabla ya kukubaliana na baadhi ya vipengele vya mkataba huo.

 Akizungumza katika mkutano wa dharura wa 17 wa Jumuiya hiyo Jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli alisema hatua hiyo imetokana na mjadala na majadiliano ya kina kutoka kwa Wakuu wa Jumuiya hiyo.

 Rais Magufuli alisema kwa mujibu wa mkataba huo, Umoja wa Ulaya ulitaka mkataba huo usainiwe mwaka huu, ambapo hata hivyo kwa kuzingatia maslahi na ustawi wa jumuiya hiyo, viongozi wa nchi wanachama wamehitaji muda zaidi wa kufanya maamuzi juu ya mkataba huo.

 Dkt. Magufuli alisema kufuatia uamuzi huo, Viongozi hao wameitaka Sekretarieti ya Jumuiya hiyo kuandaa utaratibu wa kusimamia masuala ya mahusiano kuhusu mkataba huo kwa kufanya mawasiliano na Umoja wa Ulaya.

 Tumewaomba wenzetu wa Umoja wa Ulaya wasiiadhibu nchi ya Kenya kwa kuwashinikiza kusaini mkataba wa EPA ifikapo oktoba mosi mwaka huu, ni vyema nchi zote wanachama tujiridhishe na vipengele vya mkataba huo kabla ya kuweka saini ya makubaliano” alisema Rais Magufuli.

 Akitolea mfano baadhi ya sababu zinazoifanya nchi za Jumuiya hiyo kuhitaji muda zaidi wa majadiliano kuhusu mkataba huo ni pamoja na uhakika wa kulinda viwanda vya ndani vya nchi wanachama, njia bora za kulinda maslahi ya wakulima, namna bora ya makusanyo ya kodi za bidhaa kutoka nchi za Ulaya.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli  akiongoza mkutano. 

Kushoto kwake ni  Rais Paul Kagame wa Rwanda, Mwakilishi wa Rais wa Sudan ya Kusini Mhe Aggrey Tisa Sabuni, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Ali Mohamed Shein. 

Kulia kwake ni Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda, Naibu Rais wa Kenya Mhe William Rutto na mwakilishi wa Rais wa Burundi na Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo  Balozi Alain Aime Nyamitwe

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli akipigiwa makofi na wahudhuriaji.


Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli  akiongoza mkutano akiwa na Rais Paul Kagame wa Rwanda na Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda.


Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli akihutubia.

Kwa upande wake, Rais wa Uganda Yoweri Museveni alisema katika ulimwengu wa sasa suala la utengamano wa jumuiya unahitaji zaidi wingi wa watu na uwezo wa kujitosheleza kwa uzalishaji na masoko yatakayoyosaidia ukuaji wa uchumi kwa nchi wanachama.


 Mwaka 1960 idadi ya watu katika nchi za Afrika Mashariki ilikuwa na takribani watu Milioni 40 ukilinganisha na watu Milioni 165 waliopo sasa ambapo uwezo wa uzalishaji na masoko umeongezeka, hivyo hatuna budi kuwa na jumuiya yenye uwezo wa kuzalisha bidhaa kwa wingi na kutoa huduma” alisema Museveni.

 Aidha Rais Museveni aliutaka Umoja wa Ulaya kukubaliana na uamuzi wa wakuu wa jumuiya hiyo kuwapa muda zaidi wa kufanya maamuzi kuhusu mkataba huo ambao umebeba maslahi mapana zaidi kwa wananchi wa jumuiya.

 Naye Naibu Rais wa Kenya, William Ruto alisema maamuzi kuhusu mkataba huo yanalenga usawa na kuimarisha umoja baina ya nchi wanachama hivyo ili dhana hiyo iweze kwa wananchi ni wajibu wa Viongozi kuweka maslahi ya wananchi wao.

 Katika mkutano huo, Wakuu wa Jumuiya hiyo walipokea ripoti mbalimbali ikiwemo ripoti ya mgogoro wa Burundi, ripoti ya mabaraza la mawaziri wa jumuiya hiyo kuhusu hali ya kisiasa inayoendelea nchini Sudan Kusini pamoja na uteuzi wa Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo.


Ujumbe wa Burundi.


Sehemu ya mabalozi wa nchi mbalimbali wakiwa mkutanoni hapo.


Waziri Mkuu Mstafu Jaji Joseph Sinde Warioba (kati) na Katibu Mkuu Mstaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Balozi Juma Mwapachu (kushoto) wakiwa na viongozi wastaafu wa Jumuiya.


Wageni kutoka nchi wanachama


Mabalozi wa nchi mbalimbali wakiwa mkutanoni hapo.. Kwa picha zaidi BOFYA HAPA

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad