HABARI / TASWIRA PICHA:- Rais Magufuli afungua Daraja la Kigamboni Leo hii April 19, 2016. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Tuesday, April 19, 2016

HABARI / TASWIRA PICHA:- Rais Magufuli afungua Daraja la Kigamboni Leo hii April 19, 2016.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 19 Aprili, 2016 amefungua rasmi Daraja la Kigamboni linalounganisha usafiri wa barabara kati Kigamboni na Kurasini Jiji la Dar es salaam na amependekeza Daraja hilo liitwe Daraja la Nyerere (Nyerere Bridge). 

Sherehe za ufunguzi wa daraja hilo kubwa na la kipekee kwa Afrika Mashariki na Kati zimefanyika kando ya daraja hilo upande wa Kigamboni na kuhudhuriwa na viongozi na wageni mbalimbali wakiwemo Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli, Balozi wa China nchini Tanzania Dkt. Lu Youqing, Naibu Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Mhandisi Edwin Ngonyani, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu) Mheshimiwa  Antony Mavunde, Wabunge na Mameya wa Jiji na Dar es salaam.
Ujenzi wa daraja hilo umehusisha nguzo mbili za pembezoni na mihimili miwili inayoshikilia nyaya 36, na daraja zima lina urefu wa meta 680, upana wa mita 32, njia sita za magari, njia mbili za watembea kwa miguu na barabara unganishi zenye urefu wa kilometa 2.5.

Daraja hilo limejengwa kwa fedha za ndani na kugharimu jumla ya shilingi Bilioni 254.12 ambapo kati ya fedha hizo asilimia 60 zimetolewa na Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), na asilimia 40 zimetolewa na Serikali ya Tanzania.
Kujengwa kwa Daraja hili kutaondoa kero ya msongamano wa magari na usafiri kwa wakazi wa Kigamboni na wakazi wa katikati ya Jiji la Dar es salaam ambao walilazimika kutumia kivuko (Ferry) ili kukatiza eneo la mkondo wa bahari ya Hindi ama kutumia barabara ya kuzunguka kupitia Kongowe lenye urefu wa kilometa 52.

Daraja hilo limefanyiwa majaribio kwa kutumia Malori 44 yenye uzito wa tani 30 na limethibitika kuwa na uwezo wa kubeba jumla ya tani 1,320 na hivyo linatarajiwa kusaidia usafirishaji wa mizigo ya kutoka na kuingia katika bandari ya Dar es salaam.

Akizungumza katika sherehe hizo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameagiza vyombo husika vianze mchakato wa daraja hilo kupewa jina la "Daraja la Nyerere" (Nyerere Bridge) ikiwa ni kuuenzi mchango mkubwa wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyefanya kazi kubwa ya kuijenga Tanzania.
Aidha,Rais Magufuli amewapongeza wadau wote waliohusika kufanikisha ujenzi wa Daraja hilo likiwemo Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi na wakandalasi kutoka China, na ametaka watanzania wajivunie daraja hilo kubwa na lililojenga heshima kubwa kwa nchi.

Pia Dkt. John Pombe Magufuli ametoa wito kwa Vyombo vya Habari vya Tanzania kuitangaza vyema Tanzania na kuwa na uzalendo wa kweli kwa nchi yao badala ya kubeza kazi nzuri zinazofanywa ndani ya nchi kwa manufaa ya watanzania.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad