Ucsaf yagawa Kompyuta 25 Shule za Sekondari wilayani Kibondo Mkoani Kigoma. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Saturday, April 28, 2018

Ucsaf yagawa Kompyuta 25 Shule za Sekondari wilayani Kibondo Mkoani Kigoma.

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akisalimiana na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Boni Consilii alipowasili kuzungumza nao wakati wa ziara yake jimboni kwake Muhambwe, Kibondo mkoani Kigoma.

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye amepokea kompyuta 25 zenye thamani ya shilingi milioni 45 kutoka kwa Mkuu wa Uendeshaji  kutoka Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) Mhandisi Albert Richard kwa ajili ya shule za Sekondari zilizopo Wilayani Kibondo mkoani Kigoma ili ziwawezeshe wanafunzi na waalimu kujifunza na kufundishia na kwenda sambamba na ulimwengu wa kisasa wa sayansi na teknolojia.

Mhandisi Richard amesema kuwa ugawaji wa kompyuta 25 zenye thamani ya shilingi milioni 45 kwa shule za sekondari za Wilaya ya Kibondo ni mpango wa UCSAF kupitia Mradi wa Kuunganisha Mashule.  “Tunaamini kuwa kompyuta hizi zitasaidia kuinua elimu katika mkoa wa Kigoma na katika jimbo zima”, amesema Mhandisi Richard.

Nditiye ameishukuru UCSAF kwa kutoa kompyuta 25 kwa ajili ya shule za sekondari za jimboni kwake Muhambwe, Kibondo mkoani Kigoma. Ameshukuru kwa kupata msaada huo kwa ajili ya shule mbalimbali ambazo zipo katika Wilaya ya Kibondo ambapo zitasaidia kuiweka wilaya hiyo na shule hizo katika masuala ya mawasiliano kwa urahisi zaidi. “Hizi kompyuta zitawasaidia na kuwafanya wanafunzi wajifunze kwa kukiona kitu moja kwa moja na waweze kufanya mawasiliano kwa urahisi zaidi,” amesema Nditiye.

 Amewashukuru UCSAF kwa huduma nzuri wanazozifanya kwa shule na kwa taifa kwa ujumla.
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akipokea kompyuta 25 zenye thamani ya shilingi milioni 45 kutoka kwa Mkuu wa Operesheni wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) zilizotolewa na Mfuko huo kwa ajili ya shule za sekondari za jimboni kwake Muhambwe, Kibondo mkoani Kigoma.
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (katikati) akisikiliza kwa makini maelezo kutoka kwa Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mkugwa Mwalimu Salome (kushoto) kuhusu mafunzo kwa vitendo kwa ajili ya masomo ya sayansi kwenye moja ya maabara ya shule hiyo jimboni kwake Muhambwe, Kibondo mkoani Kigoma.
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akikagua majengo ya mabweni ya Sekondari ya Wasichana ya Mkugwa wakati wa ziara yake shuleni hapo jimboni kwake Muhambwe, Kibondo mkoani Kigoma.

Katika hatua nyingine Nditiye ametembelea shule ya sekondari ya Wasichana ya Mkugwa na ya Kibondo ambapo alikuwa mgeni rasmi kwenye mahafali ya kidato cha sita ya shule hizo. Pia, alikagua miundombinu ya mabweni, madarasa, vyoo, maabara, viwanja vya michezo na mahali pa kulia chakula kwenye shule hizo na shule ya Boni Consilii zilizopo kwenye jimbo lake la Muhambwe wilayani Kibondo mkoani Kigoma.

Nditiye amewashukuru wanafunzi na waalimu kwa kusoma kwa bidii na kufundisha kwa uzalendo ambapo imeiwezesha Wilaya ya Kibondo kushika nafasi ya kwanza katika ngazi ya mkoa wa Kigoma, nafasi ya nane kitaifa kati ya kumi bora katika halmashauri zote 187 zilizopo nchini.

Amewaasa wanafunzi waliohitimu kidato cha sita kwenye sekondari hizo kuwa wamebakiza muda mfupi kuwepo shuleni ambapo mara baada ya mitihani ya taifa, watarejea kwa wazazi na walezi wao na watajiunga na jamii ambapo hamna waalimu wala walinzi wa kufuatilia mienendo yao. 

Pia, kwa wale watakaobahatika kufaulu na kuendelea na masomo ya chuo kikuu wawe makini na mienendo na tabia zao na wazingatie masomo kwa kuwa ufaulu wao unategemea kujisomea kwa bidii.

Ameongeza kuwa wazazi na walezi wawe karibu na wahitimu hao mara warejeapo nyumbani na watenge muda kuzungumza nao mara kwa mara ili waendelee kuwasihi na kuwaonya wajiepushe na vishawishi ili waweze kufikia ndoto zao kwa manufaa yao, familia zao na taifa kwa ujumla ili Serikali ipate wataalamu wa kutosha kuendesha viwanda vyetu kuendana na azma ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwa nchi ya viwanda na yenye wataalamu wa kutosha kuendesha viwanda hivyo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad