Naibu Waziri
wa Madini, Stanslaus Nyongo amesema kuwa Serikali itaboresha mazingira ya
uwekezaji wa Madini ya Nickel yanayopatikana Ngara mkoani Kagera lakini pia
itahakikisha wawekezaji wanayaongezea thamani Madini hayo hapa nchini kabla ya
kuyasafirisha nje ya nchi ili kuleta tija zaidi.
Aliyasema
hayo jana, Machi Mosi alipotembelea Mradi wa Uwekezaji wa Madini ya Nickel wa
Kabanga, uliopo wilayani Ngara, Mkoa wa Kagera, akiwa katika ziara ya kazi.
“Sisi kama Serikali tutahakikisha tunawaletea wawekezaji miundombinu ya
Barabara, Reli na Umeme ili kuwajengea mazingira rafiki ya uzalishaji lakini
kwa upande wao tunataka kuona uwekezaji makini; wachimbe na kuongeza thamani ya
madini hayo hapa nchini.
Badala ya kutoa Nickel kama malighafi, watoe bidhaa
zinazotokana na Nickel.”
alisema Nyongo.
Alisema
kuwa, lengo la Serikali ni kuhakikisha Madini hayo muhimu, ambayo kwa sasa Soko
lake Duniani limeanza kupanda, yanalinufaisha Taifa kwa kiwango kinachostahili.
Akifafanua,
Naibu Waziri alisema kuwa, Nickel ikiongezewa thamani hapa nchini, miundombinu
ya Reli, Umeme na Barabara ikaboreshwa; kutakuwa na uhakika wa kuuza Madini
hayo kwa bei nzuri na kuleta ushindani kwenye Soko la Dunia.
“Tunataka wawekezaji wachimbe ili tupate kodi, tupate mrabaha lakini
pia wananchi wa maeneo haya waweze kupata ajira.” alisema.
Akijibu
swali kutoka kwa mmoja wa waandishi wa habari walioshiriki katika ziara hiyo,
ambaye alitaka kujua Serikali ina mtazamo gani kuhusu umakini wa mwekezaji
aliyepo sasa, Naibu Waziri alisema kuwa Serikali inamchukulia mwekezaji huyo
kama mwekezaji makini kutokana na namna alivyojipambanua katika shughuli hiyo.
“Mtu ambaye amewekeza kiasi cha Dola Milioni 275 hadi kufikia sasa,
sioni kwamba anatania katika uwekezaji. Namwona ni mwekezaji aliyedhamiria na
aliye makini.” alisema.
Hata hivyo,
Nyongo alibainisha kuwa Serikali itaendelea kukaribisha wawekezaji wengine
makini katika sekta hiyo ili kwa pamoja wasaidie kuinua Pato la Taifa kupitia
uwekezaji wao.
Awali,
akiwasilisha Taarifa ya utendaji kazi wa Mradi wa Kabanga Nickel, Meneja Mkazi
wa Mradi huo, Andrew Msola alimweleza Naibu Waziri kuwa changamoto kubwa
waliyonayo ni ukosefu wa miundombinu muhimu ya Barabara, Reli pamoja na Umeme;
ambapo Naibu Waziri aliahidi Serikali kushughulikia suala hilo kwa haraka.
Ilielezwa
kuwa Mradi wa Kabanga Nickel ulianza uzalishaji wa Madini ya Nickel zaidi ya
miaka 40 iliyopita, lakini tangu mwaka 2009 ilisimamisha uzalishaji kutokana na
kuporomoka kwa bei ya Madini hayo katika Soko la Dunia.
Akizungumza
na waandishi wa habari, Naibu Waziri aliwaeleza kuwa, kwa sasa Soko la Madini
hayo limeanza kuimarika kutokana na kukua kwa teknolojia ambayo imesababisha
kuongezeka kwa matumizi ya Madini ya Nickel ikiwemo kutumika katika Magari ya
Umeme badala ya yale yanayotumia mafuta.
“Mathalani Miji mikubwa ya Ulaya hivi sasa, wanataka waachane na Magari
yanayotumia mafuta na kujikita kwenye yale yanayotumia Betri zinazochajiwa kwa
umeme.
Aidha, Dunia nzima sasa inazungumzia suala la utunzaji wa mazingira,
hivyo kila mmoja anataka kuachana au kupunguza matumizi ya mafuta ili kutunza
mazingira.”
Baada ya
Kagera, Naibu Waziri ameelekea Mkoa wa Kigoma ambako anatarajia kuhitimisha
ziara yake. Awali, katika ziara hiyo, alitembelea Mikoa ya Mwanza na Geita.
|
No comments:
Post a Comment