Aliyekuwa Mbunge wa
Biharamulo Magharibi kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (CHADEMA), Dk. Anthony Mbassa alifariki dunia jana,June 26,2016, usiku akiwa
usingizini nyumbani kwake.
Taarifa zilizopatikana
kutoka Biharamulo na kuthibitishwa na Msemaji wa familia, Pendo Ngonyani,
zilieleza kuwa kifo cha Dk. Mbassa kilifahamika alfajiri ya jana.
Alisema watoto
walipokwenda kumuamsha hakuamka hali iliyowalazimu kumuita Mama yao ambaye aliwasiliana na madaktari wa Hospitali ya Biharamulo na
kuthibitishwa kuwa alikuwa amefariki dunia.
Dk. Mbasa ambaye
alikuwa Mbunge mwaka 2010 baada ya kushinda uchaguzi mkuu,
hakurejea kwenye ubunge baada ya kuangushwa na mshindani wake, Oscar Mkasa wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2015.
Akizungumzia kifo
hicho, Pendo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema
(BAWACHA) Mkoa wa Kagera, alisema Dk. Mbassa alifariki dunia akiwa usingizini.
Pendo alisema haijafahamika
sababu ya kifo chake ingawa familia imedokeza inataka uchunguzi ufanyike
kubaini sababu ya kifo hicho.
Kwa mujibu wa maelezo
ya familia, juzi mkewe akiwa kazini, yeye (Dk. Mbasa) alitoka na
kurudi jioni saa 12 na kuacha gari lake nyumbani na kwenda
ambako hakujajulikana. Alirudi nyumbani saa 5.00
usiku akiwa akionekana kuwa amelewa.
“Nimeelezwa kuwa baada ya kuacha gari
alitoka kwa mguu kuanzia hiyo saa 12 na kurejea yumbani saa 5.00
usiku. Haijajulikana alikwenda wapi lakini alirejea akiwa amekunywa
alikuwa akihangaika na ilidhaniwa ni hali ya pombe, ndiyo hivyo asubuhi
alikutwa akiwa amefariki dunia.
“Leo alikuwa na safari ya kwenda
Bukoba kuwasiliana na mawakili wake kwa ajili ya kushughulikia
madai ya fidia ya Sh milioni 60 za gharama za kesi namba 5/2010,
iliyofunguliwa na aliyekuwa mgombea ubunge wa CCM jimbo hilo, Oscar Mkasa,” alisema.
Alisema kinachosubiriwa
hivi sasa ni ndugu na jamaa kupanga utaratibu wa maziko.
|
No comments:
Post a Comment