MWANZA / BUKOBA:-MV Serengeti yapata hitilafu, Abiria wapata wakati mgumu. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Thursday, January 07, 2016

MWANZA / BUKOBA:-MV Serengeti yapata hitilafu, Abiria wapata wakati mgumu.

Abiria 268 waliokuwa ndani ya meli ya Mv Serengeti (Pichani) iliyokuwa ikisafiri toka bandari ya Mwanza wakati ikielekea bandari ya Bukoba,mkoani Kagera wamepata wakati mgumu baada ya meli hiyo kupata hitilafu kwenye moja ya injini zake muda mfupi baada ya kuanza safari.
Meli hiyo iliyokuwa pia na wafanyakazi 37 na mizigo yenye uzito wa tani 50 iliondoka kwenye bandari ya Mwanza January 05, 2016  jioni majira ya saa kumi na dakika arobaini na ilitajiwa kufika bandari ya Bukoba January 06, 2016, asubuhi majira ya saa kumi na mbili na katika hali isiyokuwa ya kawaida imewasili leo majira ya saa saba mchana.

Ilipata itilafu kwenye injini baada ya moja ya propera kunaswa na mitego ya kuvulia samaki hali iliyopelekea maofisa wa meli hiyo waitembeze kwa kutumia injini moja hadi kuifikisha bandari ya Bukoba hali ambayo abiria waliokuwa ndani ya meli hiyo hawakuridhika nayo kwa kuwa ilikuwa ikihatarisha usalama wao na mali zao.
Kwa upande wake, ambaye ni Mathias Mathew ni afisa wa kampuni ya huduma za meli katika mkoa wa Kagera, amethibitisha kutokea kwa hitilafu katika injini ya meli hiyo na pia amesema kuwa meli itaendelea na safari zake, huku, Patric Machia, afisa mfawidhi wa mamlaka ya usafiri wa majini na nchi kavu (SUMATRA) na mkaguzi wa mamlaka hiyo wa vyombo vya majini katika mkoa wa Kagera, akieleza kuwa meli hiyo haitaruhusiwa kuondoka katika bandari ya Bukoba kwa kutumia injini moja.

Meli ya Mv. Serengeti mara kwa mara imekuwa ikipoteza mwelekeo pale inapokumbana na dhuruba na wakati mwingine injini za meli hiyo zimekuwa zikizimika mara kwa mara hali ambayo pia inahatarisha usalama wa abiria na mali zao, meli ya Mv serengeti ni mbadala ya meli ya Mv Victoria iliyoko kwenye matengenezo kwa sasa ambavyo hadi sasa yameishachukua kipindi cha zaidi ya miaka mitatu.

Papo kwa Papo >>>> Pata Picha, Habari za  Siasa, Kijamii, Biashara, Muziki na Michezo na Nyingine kwa kujiunga  na mimi hapa…..FACEBOOK , TWITTER INSTAGRAM , Pia tutumie tukio la Picha kwa WhatsApp .

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad