Katibu
Mtendaji wa NECTA, Dk Charles Msonde akizungumza na waandishi wa habari jijini
Dar es Salaam jana Januari 17,2015.
Wanafunzi
Elfu 29,770 waliofanya mtihani wa kidato cha pili mwaka 2014, wamepata alama
ambazo haziwawezeshi kuendelea na kidato cha tatu hivyo watalazimika kurudia
kidato hicho cha pili.
Sambamba na
hilo, matokeo yaliyotolewa jana Januari 17,2015 na Katibu Mtendaji wa Baraza la
Mitihani la Tanzania (NECTA), Dk Charles Msonde zimeonesha kuwa ufaulu wa
masomo ya Hisabati, Sayansi, Kilimo na Biashara upo chini ya asilimia 50.
Akitangaza
matokeo hayo kwa waandishi wa habari jana Januari 17,2015, Dk Msonde alisema
ufaulu kiujumla umeongezeka kwa asilimia 3.32.
Alisema
jumla ya watahiniwa 375,434 ambao ni asilimia 92.66 ya watahiniwa waliofanya
mtihani huo mwaka jana wamepata alama zinazowawezesha kuendelea na masomo ya
sekondari kidato cha tatu.
Kati ya hao
wasichana ni 195,328 (asilimia 92.63) na wavulana ni 180,106 (asilimia 92.69):
Mwaka 2013, watahiniwa walioweza kupata alama za kuendelea na kidato cha tatu
walikuwa 422,446 ambayo ni asilimia 89.34 ya watahiniwa 472,833 waliofanya
mtihani. Waliorudia kidato cha pili walikuwa ni asilimia 10 (zaidi ya wanafunzi
47,000).
Akizungumzia
ufaulu wa kimadaraja, Dk Msonde alisema idadi ya wanafunzi waliopata madaraja
mazuri ya ufaulu (Distinction, Merit na Credit) ni 180,965 ambao ni asilimia
44.66 ya watahiniwa waliofanya mtihani huo.
Ufaulu wa
juu ni wanafunzi 35,656 (asilimia 8.80), ufaulu wa kati ni 57,945 (asilimia
14.30), ufaulu wa kawaida ni 87,364 (asilimia 21.56), ufaulu wa chini ni
194,469 (asilimia 47.99).
Kuhusu
ufaulu wa kimasomo, Msonde alisema watahiniwa wamefaulu zaidi katika masomo ya
Uraia, Historia, Kiswahili, Kiingereza ambapo ufaulu huo uko kati ya asilimia
84, huku masomo ya Jiografia, Baiolojia, Utunzaji Hesabu ufaulu wa masomo upo
kati ya asilimia 50 hadi 70 wakati ufaulu wa masomo ya Hisabati, Fizikia,
Kemia, Sayansi ya Kilimo na Biashara ufaulu wa masomo uko chini asilimia 50.
Aidha, Dk
Msonde alisema ufaulu wa juu zaidi ni wa somo la historia ambao ni asilimia
90.71 ya watahiniwa waliofanya somo hilo na ufaulu wa chini ni wa somo la
hisabati ambalo ni asilimia 18.15 ya watahiniwa waliofanya somo hilo.
Dk Msonde
alisema baadhi ya watahiniwa wameonesha umahiri wa juu katika baadhi ya masomo
kwa kupata alama 100, ambapo watahiniwa 41 ni kwenye somo la Kiingereza, tisa
katika somo la Hisabati, huku masomo ya Biolojia, Uraia na Utunzaji Hesabu kuna
mwanafunzi mmoja mmoja aliyepata alama 100.
Alama 10 za
kila somo katika Mtihani wa Kidato ya Pili, huchangia katika Tathimini Tamati
ya Mtihani wa Kidato cha Nne kama sehemu ya alama endelevu ya mwanafunzi.
Mtihani wa
Kidato cha Pili wa 2014 ni wa kwanza kusimamiwa na Necta. Awali ulikuwa
ukiendeshwa na Idara ya Ukaguzi wa Elimu kuanzia mwaka 1999 uliporejeshwa baada
ya kusitishwa mwaka 1994.
|
No comments:
Post a Comment