UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA 2014:-Mbona Majanga……Soma Hapa zaidi. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Thursday, December 18, 2014

UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA 2014:-Mbona Majanga……Soma Hapa zaidi.

Wananchi wakiutoa mwili wa marehemu Bandoma Mabele (58) majini.

Wakati vuguvugu la uchaguzi wa serikali za mitaa 2014 likiwa bichi, baadhi ya sehemu zikiwa zinasubiri zoezi hilo kutokana na sababu tofauti, matukio mbalimbali, yakiwemo ya kusikitisha, yameripotiwa.

Huku washindi wa nafasi mbalimbali zilizokuwa zikigombewa wakisheherekea kwa namna ya aina yake, katika Kijiji cha Mwagika, Sengerema mkoani Mwanza, kulitokea msiba wa kusikitisha, baada ya mgombea wa nafasi ya Uenyekiti, aliyetambulika kwa jina la Bandoma Mabele (58) kufariki dunia kufuatia kuzama ndani ya maji ya ziwa Victoria.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka eneo la tukio, Mabele alikuwa akisubiri kuwania nafasi hiyo kabla ya uchaguzi huo kuahirishwa, hali iliyomlazimu kuamua kwenda ziwani kuvua kwa ajili ya kitoweo akiwa ameongozana na vijana wawili waliotajwa kwa majina ya Paulini Ruchiri na Samweli Malulu.

Baada ya kuingia ziwani, katika hali isiyotarajiwa, mtumbwi wao ulipata hitilafu na kupinduka na kuwafanya watu hao watatu kuanza kupigana kuokoa maisha yao, kitu ambacho kilimshinda mzee Mabele na hivyo kupoteza maisha.
Bw. Godfrey Ferdinand akiwa chakari.

Wakati hali ikiwa hivyo mkoani Mwanza, jijini Dar es Salaam katika jimbo la Kawe, mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Godfrey Ferdinand, alikutwa akiwa amelewa chakari, mfukoni mwake akiwa amechukuliwa vitu vyake vyote vya thamani.

Habari kutoka eneo la tukio zinasema awali, jamaa huyo alikuwa ametoka kujiandikisha tayari kwa ajili ya uchaguzi uliofanyika Jumapili iliyopita Desemba 14,2014. 

Kana kwamba haitoshi, baada ya kutoka huko, alisikika akiwaambia marafiki zake kuwa waende sasa wakatumie, kwa vile alikuwa na fedha maana alipata mshahara kazini.

Inadaiwa kuwa baada ya kuwa wamekaa mezani, watu aliokuwa nao walimzunguka na kumwekea vitu vilivyomzidishia kilevi na kujikuta akipoteza fahamu.

Baada ya kupoteza fahamu ilidaiwa watu hao walichukua fedha zote alizokuwa nazo pamoja na vitu vingine vya thamani, wakimwacha na vitambulisho vyake tu!

Wananchi wakiwa kwenye kisima kilichopoteza maisha ya marehemu Beatha Mchimani Ngosha.

Wakati hayo yakiendelea jijini Dar es Salaam, huko Geita nako hali ya hewa ilibadilika baada ya mgombea ujumbe wa mtaa wa Msalaba Road, huko Geita kwa tiketi ya Chadema, Beatha Mchimani Ngosha, ambaye alishinda, kukutwa ndani ya kisima akiwa ameshafariki.

Ilidaiwa kuwa mshindi huyo alikuwa amekaa na wenzake wakisherehekea ushindi alipoaga kuwa anaenda kujisaidia, lakini hakurejea tena hadi mwili wake ulipokutwa kisimani asubuhi ya siku iliyofuata.
Bi.Hellen Kijo Bisimba,Mkurugenzi mtendaji LHRC.

KAULI YA LHRC.

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimelaani vikali vurugu zilizotokea na kusababisha uharibifu mkubwa wa mali  katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Ezekiel Masanja, aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari na kufafanua kuwa taarifa zao zinaonyesha kuwa vurugu nyingi zilitokea kutokana na udhaifu wa usimamizi, kuwapo kwa maandalizi hafifu na ya kubabaisha  ambayo ndiyo yaliyoibua hasira kwa wananchi na kusababisha vurugu hizo.

Aidha, alisema ni dhahiri kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) imeshindwa kuandaa na kusimamia vyema uchaguzi  huo na kusababisha usumbufu mkubwa na ukiukwaji haki ya kikatiba ya wananchi kupiga kura.

 “Kama vituo vingefunguliwa kwa wakati, majina ya wapiga kura yangekuwapo tayari na pia uratibu wa zoezi zima ungefanyika kama inavyotakiwa kisheria kwa kiasi kikubwa tungepunguza vurugu nyingi zilizojitokeza,” alisema Masanja.

Aliongeza kuwa LHRC kinatoa wito kwa kwa Waziri mwenye dhamana kuwajibika mara moja na wote waliohusika kuzembea na kuharibu uchaguzi huu wawajibishwe.

Aliyataja maeneo yaliyokumbwa na vurugu na uvunjifu wa amani mara baada ya matokeo kutangazwa  kuwa ni Kimara na  Kawe kwa mkoa wa Dar es Salaam, Ilemela kwa mkoa wa Mwanza na Sumbawanga, Mkoa wa Rukwa.

Pia waangalizi walishuhudia tukio la ukiukwaji wa haki ya kuishi kwa kijana mmoja huko Nzega aliyeripotiwa kuwa alipigwa risasi kwa bahati mbaya katika harakati za kusubiri matokeo baada ya kuzuka kwa vurugu na polisi kuingilia kati kwa kuwatawanya wananchi kwa kutumia risasi za moto.

Alizitaja dosari nyingine kuwa ni ushiriki mdogo wa wananchi katika kampeni uliosababishwa na mkanganyiko wa tarehe ya kampeni, uelewa mdogo wa umhimu wa kushiriki katika uchaguzi, kampeni nyingi kumalizika baada ya saa 11 jioni na wanachama kupita mitaani wakiimba na kupiga tarumbeta kuhamasisha wananchi kuwapigia kura wagombea wao.


UNGANANASI KATIKA  FACEBOOK , TWITTER , INSTAGRAM , Pia tutumie tukio la Picha kwa WhatsApp +255789925630.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad