Baraza la
Mitihani la Taifa (Necta) limetangaza kuanza kutoa vyeti mbadala kwa gharama ya
Sh100,000 kwa wote ambao vyeti vyao vimeharibika kiasi cha kutofaa kwa matumzi.
Tangazo hilo
lililotolewa jana Septemba 29,2014, na Necta, linawalenga wote waliohitimu
elimu zao kuanzia Oktoba 2008, ambao vyeti vyao vina picha za watahiniwa
husika, huku likifafanua kuwa waliomaliza kabla ya hapo, utaratibu wa kuwatumia
uthibitisho wa matokeo katika taasisi zenye mahitaji utaendelea.
Kwa mujibu
wa tangazo hilo: “Ombi la cheti mbadala litapokewa baada ya miezi mitatu kupita
tangu upotevu wa cheti halisi kutangazwa gazetini.
Uchunguzi wa
uthibitisho utafanyika kwa siku 30 tangu kupokewa kwa ombi la cheti mbadala kwa
kuihusisha polisi (kitengo cha uchunguzi wa picha).”
Katika
kukabiliana na udanganyifu unaoweza kujitokeza kutoka kwa watu wasio waaminifu,
baraza hilo lilisema kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya
watakaoshiriki katika uombaji wa vyeti hivyo vitakavyokuwa na neno ‘duplicate’
ili kuvitofautisha na vyeti halisi.
“Cheti
mbadala kitatolewa mara moja tu na endapo itabainika kuwa cheti halisi bado
kinatumika katika soko la ajira au mafunzo na mtahiniwa akathibitika kushiriki
katika kuidanganya Necta, hatua kali za kisheria zitachukuliwa,” inaonya fomu
ya maombi ya cheti.
Waliopoteza
vyeti halisi watatakiwa kutoa taarifa polisi na kutangaza gazetini, huku
waliounguliwa au vyeti vyao kuharibiwa na mchwa, mafuriko, panya au kwa namna
nyingine yoyote watatakiwa kuwasilisha vielelezo husika pamoja na barua ya Serikali
ya Mtaa wa eneo la tukio la moto au mafuriko yalipotokea.
Taarifa hiyo
ilisema kuwa, iwapo yapo mabaki ya cheti husika, watatakiwa kuyawasilisha
Necta.
Tangazo la
gazetini la upotevu wa cheti litatakiwa kuwa na taarifa muhimu kama jina la
mtahiniwa, namba ya mtihani, aina ya mtihani, mwaka wa mtihani, jina la shule
na picha ya mtahiniwa.
Baada ya
polisi kutoa hati ya upotevu wa cheti, mwombaji atatakiwa kuambatanisha picha
ndogo mbili pamoja na nakala ya kitambulisho na risiti halisi ya malipo.
Pia, katika
mwendelezo wa kujiridhisha kuwa kila mtumishi au mwanafunzi anakuwa na cheti
chake baada ya taasisi mbalimbali pamoja na idara za Serikali kuanzisha
utaratibu wa kuhakiki taarifa za kitaaluma hasa vyeti vinavyotolewa na baraza
hilo.
|
No comments:
Post a Comment