TFDA:-Kaa mbali, bidhaa hizi hatari - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Friday, April 04, 2014

TFDA:-Kaa mbali, bidhaa hizi hatari


Vinywaji baridi ambavyo havikusajiliwa na TFDA vilivyokamatwa kufuatia ukaguzi maalum katika jiji la Dar es salaam.


Maziwa ya watoto aina ya SMA 1,2 na 3, Promil Gold, S-26 Gold, Nursoy, Progress Gold, Cow &Gate, Isomil 2 na Infacare Soya , Nutrikids na Aptimil 1 yaliyokamatwa ambayo hayajasajiliwa na TFDA .


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa(TFDA) Bw.Hiiti Sillo (kulia) akitoa ufafanuzi wa maziwa yaliyokamatwa yakiwa kwenye kifungashio kisichokua na maelezo yoyote yakiuzwa kwenye maduka ya kuuzia vyakula “Supermarkets” na Mini-Supermarkets katika jiji la Dar es salaam.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa(TFDA) Bw.Hiiti Sillo akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam kuhusu ukaguzi maalum wa maduka ya kuuzia vyakula “Supermarkets” na Mini-Supermarkets katika jiji la Dar es salaam kinyume cha sheria ya Chakula , Dawa na Vipodozi sura ya 219.


Mkurugenzi wa Usalama na Chakula wa TFDA Bw. Raymond Wigenge akitoa ufafanuzi kwa waandishi kuhusu hatua zinazochukuliwa na TFDA kuhakikisha usalama wa vyakula na Dawa nchini .TFDA imekuwa ikiongeza nguvu katika kukabiliana na bidhaa zisizokidhi viwango kwa kushirikiana na mamlaka nyingine za udhibiti kwa kukagua, kukamata na kuchukua hatua za kisheria ikiwemo kuwafikisha mahakamani wanaokiuka sheria.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa(TFDA) Bw.Hiiti Sillo (kulia) akitoa ufafanuzi wa baadhi ya bidhaa zilizokamatwa katika ukaguzi maalum kwenye maduka ya kuuzia vyakula “Supermarkets” na Mini-Supermarkets katika jiji la Dar es salaam zikiuzwa kinyume cha sheria ya Chakula , Dawa na Vipodozi sura ya 219. Wengine ni Mkurugenzi wa Usalama na Chakula wa TFDA Bw. Raymond Wigenge, na Meneja wa Ukaguzi wa Chakula wa TFDA kanda ya Mashariki Bw. Emmanuel Alphonce.

Afisa Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) akiwaonesha waandishi wa habari baadhi ya bidhaa zilizokamatwa na mamlaka hiyo zikiwemo chumvi, vinywaji, maziwa ya watoto ambazo hazijasajiliwa na mamlaka hiyo kufuatia ukaguzi maalum uliofanyika katika jiji la Dar es salaam.

Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini (TFDA) imekamata na kuyaharibu makopo 591 ya maziwa ya watoto katika maduka 36 yenye thamani ya Sh. 17,625,000 ambayo hayajasajiliwa na kutokuwa na maelezo ya lugha ya Kiswahili.

Hatua hiyo imetokana na kuvunjwa kwa sheria na kanuni ya Maziwa ya Watoto ya mwaka 2013 ya TFDA ambayo inasema lugha isiyo ya Kiswahili na michoro ya picha inayomshawishi mnunuzi hairuhusiwi katika bidhaa hiyo. 

Maziwa hayo ambayo yamekutwa yakiuzwa katika maduka na mengine katika supermarket mbili za Kichina na kuwa na maelezo ya lugha ya Kichina ni aina ya SMA ( 1, 2,3), S-26 Gold, Promil Gold, Progress Gold, Cow & Gate, Infacare Soya, Isomil 2, Nutrikids, Nursory na Aptimil 1.

Mkurugenzi Mkuu TFDA, Hiiti Sillo, alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya mamlaka hiyo kufanya ukaguzi katika maduka, bakery na supermarket uliofanyika kati ya Machi 10 na 21, mwaka huu katika mkoa wa Dar es Salaam.

Alisema kuwa maziwa ya watoto yaliyosajiliwa na TFDA kisheria yanatakiwa kuwa na maelezo yenye lugha mbili ya Kiswahili na Kiingereza ili kumwezesha mtumiaji wa bidhaa hiyo kutoa kipimo cha matumizi sahihi kwa mujibu wa mtengenezaji.

Aidha, alisema ukaguzi huo uliofanyika katika supermarket 107 kwa kushirikiana na wakaguzi wa Manispaa za Ilala, Kinondoni na Temeke, umetokana na kukithiri kufunguliwa maduka hayo ikiwamo kuingizwa kwa bidhaa ambazo hazijasajiliwa, hatua ambayo ni kinyume cha sheria.

Mbali na kuharibiwa kwa maziwa hayo, pia makopo na paketi 6,090 za chumvi zenye ujazo tofauti zenye thamani ya Sh. 5,131,000 zilikamatwa katika maduka 39 kutokana na kutosajiliwa na TFDA.

Alizitaja aina ya chumvi hizo ambazo ni Ken Salt, American Garden Salt, Lo Salt, Chilly Willy Salt, Today’s Essential, Best Salt, Nezo Salt, DP, Costa Salt na kusema zinauzwa katika maduka hayo kwa kukiuka kanuni ya uwekaji wa madini joto ya mwaka 2010.

Pia, alisema bakery nne ndani ya supermarket zilikutwa hazina vibali pamoja na maduka 12 ambayo yalikutwa yakiuza vinywaji baridi vya kuongeza nguvu ambavyo havijasajiliwa na mamlaka hiyo. Vinywaji hivyo ni B52, Red Bull (silver, red, blue), Boost, Krazy, Monster, Rockstar, Climax na Atlas.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad