Matokeo Makubwa Sasa(BRN):-Watu binafsi kumiliki treni........'' - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, April 23, 2014

Matokeo Makubwa Sasa(BRN):-Watu binafsi kumiliki treni........''



Mwenyekiti wa Bodi ya TRL,Bw.Severin Kaombwe alisema mpango huo huenda ukaanza baada ya mwaka 2015 kutoka na mkakati uliopo kwenye Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).

Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) inatarajiwa kupata ushindani baada ya Serikali kuamua kuruhusu wawekezaji wa sekta binafsi kutumia Reli ya Kati.

Uamuzi huo wa Serikali huenda ukaongeza ufanisi kwa shirika hilo ambalo kwa miaka mingi limekuwa likikumbwa na matatizo ya kiufanisi.

Baada ya kuanzishwa mwaka 2007, TRL ilikumbwa na misukosuko baada ya mwekezaji Rites kutoka India kushindwa kulisimamia kikamilifu na kusababisha hasara ya mabilioni. Kabla ya TRL reli ya kati ilikuwa chini ya Shirika la Reli (TRC) ambalo nalo halikuwa na ufanisi.

Akizungumza katika ufunguzi wa warsha ya kuijengea uwezo TRL iliyofanyika Dar es Salaam jana(April 22,2014) , Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dk Shaaban Mwinjaka alisema kampuni binafsi zitaruhusiwa kuingiza treni zitakazotumia reli hiyo kwa kulipa ushuru kwa Serikali.

Kutokana na mabadiliko hayo, Dk Mwinjaka alisema Serikali imeanza kuiandaa TRL kupambana na ushindani utakaotolewa na kampuni hizo binafsi.

Katika hii warsha tunawaandaa kujua kwamba utafikia wakati wanahitaji kujitegemea. Kwa misingi hiyo basi, tumepata wataalamu kutoka ndani na nje kuweka mawazo yao pamoja kujua ni namna gani mabadiliko hayo yatafanyika,” alisema Dk Mwinjaka.

Alipoulizwa kuwa uamuzi huo utaanza kutekelezwa lini, Mwinjaka alisema baada ya TRL kujengewa uwezo wa kuwa na mabehewa, injini na watumishi wa kutosha ili kuweka uwanja mzuri wa ushindani.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Bodi ya TRL, Severin Kaombwe alisema mpango huo huenda ukaanza baada ya mwaka 2015 kutoka na mkakati uliopo kwenye Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).

Kwa sasa tumeshaagiza vichwa (injini) 21 na takriban mabehewa 200 ambayo yanatarajiwa kufika ndani ya Agosti mwaka huu,” alisema Dk Mwinjaka huku akisisitiza kwamba mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa BRN.

Alisema injini na mabehewa hayo yana uwezo wa kurekebishwa kupita kwenye reli zote; za kawaida (ya kati) na ile ya kisasa inayotarajiwa kujengwa.

Serikali imeamua kununua aina hiyo ya vifaa ili shughuli za usafirishaji wa mizigo kupitia reli ya kati ziendelee bila kuathiriwa wakati wa kujenga reli hiyo mpya na baada ya kukamilika tutarekebisha ili kupita njia mpya.”

Reli mpya ya kisasa inatarajiwa kugharimu takriban Dola za Marekani 6 bilioni (Sh9.6 trilioni) zinazofadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).

Dk Mwinjaka alisema ujenzi utaanza baada ya kukamilika hatua za kumpata mkandarasi Desemba mwaka huu, shughuli inayosimamiwa na AfDB yenyewe.

Tulishafanya upembuzi yakinifu na sasa tunasubiri kumpata mshauri elekezi anayetafutwa na AfdB, ambaye atamteua mkandarasi mwenye uwezo wa kujenga reli hiyo,” alisema.

Reli hiyo itaanzia Dar es Salaam - Isaka hadi Kigali, Rwanda; pia itaendelea kuanzia Keza wilayani Ngara hadi Gitega na Musongati, Burundi.

Mbali na nchi hizo mbili, pia Serikali mapema mwaka jana ilisaini mkataba na Serikali ya Uganda kuanza kutumia reli ya kati kusafirisha mizigo kutoka Dar es Salaam mpaka Kampala na Dk Mwinjaka alisema tayari injini tano na mabehewa 60 yameshanunuliwa kwa ajili ya mradi huo.

Mkurugenzi Mtendaji wa TRL, Kipallo Kisamfu alisema kampuni yake inajiandaa kwa mabadiliko hayo na baada ya miaka mitatu itakuwa na uwezo wa kusafirisha tani milioni tatu za mizigo kwa mwaka kutoka 200,000 za sasa.

Tumejipanga pia kuongeza rasilimali watu kwa asilimia 30 kila mwaka mpaka tutakapofikia lengo. Kwa sasa tunao wafanyakazi 2,900 na tunagemea sana Chuo cha Reli kuzalisha wataalamu hao,” alisema Kisamfu.

Awali, Kaombwe alisema kampuni hiyo itakuwa ya kibiashara zaidi na itaruhusiwa kukopa kutoka katika vyanzo mbalimbali vya fedha.

Habari Na:-Mwananchi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad