![]() |
|
Idadi kubwa
ya watu nchini ni watoto wenye umri wa chini ya miaka 15 na vijana huku mikoa
ya Simiyu, Rukwa na Geita ikitajwa kuwa zaidi ya nusu ya watu wake, ni watoto.
|
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu,
Dk Albina Chuwa alimweleza hayo Rais Jakaya Mrisho Kikwete jana Ikulu wakati
akimkabidhi vitabu na majedwali yenye matokeo na machapisho ya Sensa ya Watu na
Makazi ya Mwaka 2012.
Alisema asilimia 44 ya watu wote
hapa nchini Tanzania, ni watoto wenye umri chini ya miaka 15.
Alisema utafiti wa Mama na Mtoto wa
Mwaka 2010, unaonesha kuwa kiwango cha uzazi ni wastani wa watoto 5.4 kwa kila
mama mwenye umri wa kuzaa ambao ni miaka 15 hadi 49.
Sera ya Vijana Tanzania ya Mwaka
2007 inatambua vijana kuwa ni watu wote wenye umri wa kati ya miaka 15 na 35,
ambao kulingana na Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 ni asilimia 34.7 ya
watu wote nchini.
Kulingana na Takwimu, idadi ya watu
Tanzania imeongezeka zaidi ya mara tatu kutoka watu milioni 12.3 kwa mwaka 1967
hadi watu milioni 44.9 mwaka 2012.
Takwimu hizo zinaonesha Mkoa wa Dar
es Salaam una asilimia kubwa ya vijana wakati Mkoa wa Singida, ukiwa na
asilimia ndogo zaidi.
Kulingana na takwimu, zaidi ya nusu
ambayo ni asilimia 52.2 ya watu wote nchini, wako katika umri wa kufanya kazi
huku Dar es Salaam ikiongoza.
Mkoa wa Simiyu uko chini zaidi kwa
kuwa na asilimia 45.5 ya watu wenye uwezo wa kufanya kazi.
Katika takwimu hizo, zaidi ya nusu
ya watu katika mikoa ya Simiyu, Rukwa na Geita ni watoto wenye umri wa chini ya
miaka 15.
Takwimu zinaonesha asilimia 5.6 ya
watu nchini ni wazee na takwimu hizi zinaonesha kuwa wazee kwa asilimia kubwa
wako katika mikoa ya Kilimanjaro, Mtwara, Lindi na Pwani.
Asilimia ndogo zaidi ya wazee iko
katika mikoa ya Dar es Salaam na Mjini Magharibi.
Kwa mujibu wa Sera ya Wazee
Tanzania, mzee ni mtu mwenye umri wa miaka 60 au zaidi.
Aidha takwimu zinazidi kuonesha kuwa
asilimia ya watu wanaoishi mijini imeongezeka zaidi ya mara tano, ambapo ni
asilimia 6.4 mwaka 1967 na kufikia asilimia 29.6 kwa mwaka 2012.
Jiji la Dar es Salaam lina asilimia
10 ya watu wote Tanzania Bara wakati Mjini Magharibi ina asilimia 46 ya watu
wote wa Zanzibar.
Sensa pia imeonesha wanawake ni
wengi zaidi , kwa asilimia 51 ukilinganisha na wanaume ambao ni asilimia 49
kama ilivyo katika nchi nyingi Afrika.
Mkoa wa Manyara unaongoza kwa kuwa
na idadi kubwa ya wanaume na Njombe una idadi ndogo zaidi ya wanaume.






No comments:
Post a Comment