AJALI:-Rais Kikwete astushwa na ajali kubwa iliyotokea Jumamosi, Machi 29, 2014 na kusababisha vifo vya watu 21 na majeruhi 11 3 . - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Monday, March 31, 2014

AJALI:-Rais Kikwete astushwa na ajali kubwa iliyotokea Jumamosi, Machi 29, 2014 na kusababisha vifo vya watu 21 na majeruhi 11 3 .


Watu 21 wamefariki dunia katika ajali mbaya imetokea Wilaya ya Rufiji, mkoani Pwani ikihusisha magari 3 na wengine 11 kujeruhiwa.Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, ACP Ulrich Matei, alisema ajali hiyo imetokea katika Barabara Kuu ya Dar es Salaam-Lindi, eneo la Ikwiriri, wilayani humo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amestushwa na kuhuzunishwa na ajali kubwa iliyotokea usiku wa Jumamosi, Machi 29, 2014, katika Mkoa wa Pwani ikihusisha magari matano na kusababisha vifo vya watu 21 na majeruhi 11.

Rais Kikwete amevielezea vifo hivyo kuwa siyo vya lazima na ni upotevu wa bure wa maisha ya Watanzania.

Katika salamu za rambirambi ambazo amemtumia Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mheshimiwa Mwantumu Bakari Mahiza, Rais Kikwete amesema: “Nimeshtushwa na kusikitishwa na taarifa ya ajali iliyohusisha magari matano na iliyotokea jana usiku katika Kijiji cha Kibupa, kilichoko kati ya Ikwiriri na Kibiti, Wilaya ya Rufiji, Mkoa wa Pwani, ambako maisha ya Watanzania wenzetu 19 yamepotea na wengine 11 kujeruhiwa.”

“Kufuatia ajali hiyo, nakutumia wewe Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mheshimiwa Mwamtumu Bakari Mahiza salamu za rambirambi za dhati ya moyo wangu kuomboleza vifo vya Watanzania wenzetu hao. Nimefadhaishwa mno na ajali hiyo ambako pia wenzetu wengine 11wameumia.”

“Aidha, kupitia kwako, nawatumia ndugu, jamaa na marafiki ambao wamepoteza wapendwa wao katika ajali hiyo. Naelewa machungu yao katika kipindi hiki na niko nao katika kuomboleza upotevu huu mkubwa wa maisha ya wenzetu. Msiba wao ni msiba wangu na machungu yao ni machungu yangu. Nawaombea subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu na naungana nao kumwomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, aziweke peponi roho za marehemu.”

Rais pia amewapa pole wote walioumia katika ajali hiyo mbaya akisema: “Mkuu wa Mkoa nakuomba pia uwafikishie pole zangu nyingi wote ambao wameumia katika ajali hiyo. Nawaombea Baraka za  Mwenyezi Mungu ili wapone haraka na wapate tena nafasi ya kuendelea na shughuli za kuboresha maisha yao.”

Imetolewa na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
30 Machi,2014.

>>>Awali ajali hiyo ilihusisha magari mawili, Toyota Hiace (T 948 CUX), iliyokuwa ikitokea Ikwiriri kuelekea Rufiji ambalo lilikwenda kukwaruzana na Lori(T 132 AFJ) kwa nyumba, ambalo lilikuwa limeharibika na kusimama barbarani.

Alisema baada ya kulikwaruza roli hilo, mlango wa Hiace uling'oka na kubaki kwenye roli ambapo gari hiyo lilipoteza mwelekeo na kwenda kugongana uso kwa uso na gari nyingine aina ya Canter(T 774 CJW) na kupinduka.

"Katika ajali hii, watu 14 walifariki dunia papo hapo, wakati polisi na baadhi ya wananchi wakiendelea kuwaokoa majeruhi ili wakimbizwe hospitali, likatokea basi la kampuni ya Mining (President)( T 242 BXA), kuwakanyaga watu waliokuwa wakitoa msaada na kuwaua ndio maana idadi ya waliokufa imefikia 21.

"Basi hili lilikuwa linatoka Lindi kuelekea Dar es Salaam...polisi walifanya jitihada za kulisimamisha lakini dereva wake alikataa kusimama na kwenda kukanyaga watu lakini tayari tumemkamata, majeruhi mmoja amehamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dar es Salaam," alisema Kamanda Matei.

Kamanda Matei alisema, basi hilo linashikiliwa polisi ambapo uchunguzi ukikamilika, dereva wake atafikishwa mahakamani kujibu mashtaka.

Aliwataja waliokufa ni Sixtus Ally Mtanga(32) na Nassoro Mohamed Kajani(20) wakazi wa Ikwiriri, Juma Said Kitambulilo(30) na Salum Goma Makonde (50), Ustaadhi Kalilambwe(34) na Shafil Kip (30), Wasabi Sabil(45), Ramadhani Ally (23)wote wakazi wa Mbagala.

Shabani Bakari(30) Kondakta wa Hiace, mkazi wa Kibiti, Masud Abulal (27), mkazi wa Mkuranga, Ammi Mpemba (30)na Madadi Hassan Mangasongo (45) wakazi wa Jaribu na Japhet Ponsian (24), mkazi wa Dar es Salaam.

Pia yupo Said Ally China (21) mkazi wa Kimanzichana, mkazi wa Jaribu, Abdalahaman Yusuph Kihemke(45), mkazi wa Kongowe na Fikiri Said Sauze, mkazi wa Vikindu.

Wengine ni Nywari Mshigani mkazi wa Dar es Salaam, Hassan Wasabi (18), mkazi wa Kibiti na Seleman Mcharazi (47) mwingine aliyejulikana kwa jina moja la Mustafa, wote wakazi wa Mbagala na maiti ya mwanamke haijafahamika jina lake.

Waliojeruhiwa katika ajali hiyo ni Frank Sixmundi (31), dereva wa gari la Maliasili Kibiti ambaye alifika eneo ili kutoa msaada kwa majeruhi ambaye ameumia kichwani, Mohamed Salehe (49) na Charles Rogasani (23), wote wakazi wa Kibiti na Mohamed Mengine (42), mkazi wa Dar es Salaam.

Wengine ni Mniko Magige Mango (54) na Abdalah Issa (25) wakazi wa Mkuranga, Khalid Salum (32), mkazi wa Dar es Salaam, Ahmad Yusuph (23), mkazi wa Kigamboni na Shomari Yusuph (42), mkazi wa Mburahati. Majeruhi wamelazwa katika hospitali za Ikwiriri, Misheni ya Mchukwi na wengine hospitali ya Taifa Muhimbili.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad