VIDEO:Maelfu ya Wananchi wamzika msanii wa kizazi kipya, Albert Magwea maarufu kama Ngwear au Cowboy Mkoani Morogoro. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Friday, June 07, 2013

VIDEO:Maelfu ya Wananchi wamzika msanii wa kizazi kipya, Albert Magwea maarufu kama Ngwear au Cowboy Mkoani Morogoro.



Jeneza lenye mwili wa Albert Mangweha likishushwa kaburini.


Kaburi la Mangweha likijengwa baada ya mazishi.…ambapo Maelfu ya Wananchi wa mkoa wa Morogoro na Maeneo mengine ya jirani wamejitokeza kwa wingi kuuaga na kuuzika mwili wa aliyekuwa msanii wa kizazi kipya, Albert Magwea maarufu kama Ngwear au Cowboy.


Aidha Mazishi  ya msanii  huyo maarufu wa muziki wa kizazi kipya, Albert Mangwair, yaliyofanyika makaburi ya Kihonda-Kanisani, jana(Juni 06,2013) yaliutikisa mji wa Morogoro mbele ya Mkuu wa Mkoa huo, Joel Bendera.




Shughuli hiyo ilitanguliwa na kuaga mwili na ilifanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri kutokana na wingi wa maelfu ya watu.




Wingi wa watu ndio uliifanya Kamati ya Mazishi chini ya Adam Juma, ihamishie hafla hiyo Uwanja wa Jamhuri badala ya nyumbani kwa usalama zaidi.




Mji wa Morogoro ulianza kuzizima tangu asubuhi, baada ya kushuhudia vikundi vya watu wengi vikielekea Jamhuri wakiwa kwa miguu, pikipiki, baiskeli na wengine kwenye magari vikienda na kurudi.




Wasanii na viongozi mbalimbali, akiwamo Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’, nao walikuwapo kwenye tukio la kuaga mwili wa Ngwair na baadaye kwenye mazishi yake ambayo yalizua mkanyagano wa aina yake.




Idadi kubwa ya watu ilijitokeza katika shughuli ya kumuaga marehemu, ambapo pia ilikimbilia makaburini kwa ajili ya kushuhudia mwili wake ukiingia kaburini.




Awali, Mkuu wa Mkoa Morogoro, Joel Bendera, alifika nyumbani kwa mama wa marehemu saa nne za asubuhi na kupata fursa ya kuwapa pole wafiwa.




Akizungumza na wanafamilia na baadaye Uwanja wa Jamhuri, Bendera alisema Tanzania imepoteza msanii nyota na mwenye bahati ya kupendwa na watu wengi.




Hii ni hatari kubwa maana Ngwair ameonyesha ni kiasi gani alikuwa nyota katika tasnia ya muziki wa Hip Hop kwa umahiri wake, sambamba na kuishi na watu vizuri.




Hii leo ni historia katika mkoa wa Morogoro, hususan kwa kushuhudia watu wengi wakiwa na huzuni katika kumuaga msanii wao mpendwa kwa namna moja au nyingine, hivyo serikali itaendelea kufanyia kazi changamoto zinazowakabili vijana hawa,” alisema Bendera.




Naye Mbunge wa Mbeya Mjini kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’, alisema wasanii wamechoka kuishi kimaskini wakati watu wengi wanaheshimu kazi zao.




Inaumiza kuona tunazikwa kwa mtindo huu wakati maisha yetu ni magumu mno, hivyo hatuwezi kuona hali hii inaendelea kuota mizizi, hivyo wasanii tuendelee kuwa makini katika hili.




Matatizo yaliyompata Ngwair katika maisha yake ni sehemu ya changamoto zilizopo katika tasnia hii ya muziki wa kizazi kipya, ingawa tukifa mazishi yetu yanakuwa ya heshima mno,” alisema.




Pamoja na kukusanya watu wengi, watu wengi walionekana kwenda uwanjani kuwaona wasanii wengine, hivyo kusababisha mkanyagano kila anapoingia au kutoka msanii nyota.




Hata hivyo, matatizo yalianza kujitokeza wakati wa kuaga mwili kutokana na askari kushindwa kukabiliana na wingi wa watu katika kuwadhibiti.




M 2 The P.
Wakati wa shughuli ya kuaga, ghafla, rafiki wa Ngwair, aliyopata matatizo naye Afrika Kusini, Mgaza Pembe, M 2 The P, aliletwa uwanjani hapo kumuaga Ngwair.




Barabara zilizopitiwa na msafara wa mwili wa Ngwair, zilikuwa zimejaa watu wakiwa na nia ya kumungalia nyota wao akielekea nyumba yake ya milele baada ya kufariki Afrika Kusini, Jumanne ya wiki iliyopita.




Kufika makaburini, umati mkubwa wa watu ulikuwapo, hivyo ndugu wa marehemu kukosa muda wa kutia mchanga katika kaburi, hasa pale watu waliposhindwa kusogea.




Kaka wa marehemu, Kenneth Mangwea, aliwashukuru Watanzania kwa moyo wao wa upendo kiasi cha kushirikiana na wao kuhakikisha kuwa mwili wa Ngwair unazikwa Tanzania.




Nashukuru sana, natumia muda huu kuwatakia upendo zaidi na zaidi Watanzania wenzetu, sambamba na kumtakia mapumziko mema huko mbinguni Ngwair,” alisema Kenneth.




Mwili wa Mangwair ulizikwa majira ya saa tisa za mchana, ikiwa ni siku moja tangu aagwe kwenye Viwanja vya Leaders, jijini Dar es Salaam.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad