Matokeo ya SENSA 2012 si Wanaume kuoa wake wengi Japo wastani wa uwiano wa idadi ya watu kijinsi Tanzania Bara, ni Wanaume 95 kwa kila Wanawake 100. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, April 10, 2013

Matokeo ya SENSA 2012 si Wanaume kuoa wake wengi Japo wastani wa uwiano wa idadi ya watu kijinsi Tanzania Bara, ni Wanaume 95 kwa kila Wanawake 100.



Wataalamu na wachambuzi wa masuala ya kijinsi wameasa matokeo ya sensa ya watu na makazi yanayoonesha idadi ya wanawake ni kubwa kuliko wanaume yasitafsiriwe kwa mtazamo wa kwamba suluhu ni wanaume kuoa wake wengi.




Matokeo yaliyotangazwa na Kamishna wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012, Amina Mrisho yanaonesha wastani wa uwiano wa idadi ya watu kijinsi Tanzania Bara, ni wanaume 95 kwa kila wanawake 100.




Zanzibar ni wanaume 94 kwa kila wanawake 100 huku mikoa mingi uwiano ukiwa kati ya wanaume 92 na 95.




Mkoa wa Manyara ndio pekee una wanaume wengi kuliko wanawake kwa uwiano wa wanaume 101 kwa kila wanawake 100 huku Mkoa wa Njombe, ukiwa na wanawake wengi zaidi kwa uwiano wa wanaume 88 kwa kila wanawake 100.




Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wachambuzi wanasema dhana kwamba wanawake wanazaliwa wengi kuliko wanaume ni dhaifu badala yake, takwimu hizo zichambuliwe kitaalamu kuwezesha mipango sahihi ya kisera na kiuchumi kwenye kipengere hicho.




Wamesema tafsiri yake lazima izingatie sababu mbalimbali zikiwemo za kibaiolojia na shughuli za mwanamume ili watunga sera na wanaotoa uamuzi katika masuala ya maendeleo kuja na suluhu sahihi.




Unaweza ukachukulia mzaha kwamba wanawake ndiyo wanapaswa kusaidiwa kwa kuwaoa lakini kumbe wanaume wakawa ndiyo wanaohitaji kusaidiwa kwa kukabili mambo yanayochangia idadi yao kuwa ndogo,” alisema mwanaharakati wa masuala ya jinsia, Remmy Magesa.




Meneja wa Idara ya Takwimu za Jamii, Vifo, Uzazi na Maradhi ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Aldegunda Komba alisema kibaiolojia, uwezo wa wanaume kuishi wanapofikia utu uzima, ni mdogo kuliko wa wanawake.




Katika mafunzo yaliyoandaliwa na NBS kwa waandishi wa habari kuwaelimisha juu ya uandishi wa habari za matokeo ya sensa, Komba sanjari na Mratibu wa Sensa, Irenius Ruyobya, walikiri kuwepo watu wanaochukulia wingi wa wanawake kuwa ni tatizo ambalo suluhisho lake linapaswa kuwa ndoa za wake wengi.




Wataalamu hao walifafanua kwamba idadi ya wanawake kuzidi wanaume ni suala la kidunia siyo tu kwa Tanzania. Licha ya sababu za kibaiolojia, pia wingi wa majukumu ya kifamilia na kimaisha yakiwemo majanga, vinatajwa kuwa chanzo cha kupungua umri wa kuishi wa wanaume.




Akizungumza na mwandishi mwishoni wa wiki baada ya matokeo hayo kuzinduliwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, pia alisisitiza mantiki ya takwimu hizo akisema haimaanishi kwamba idadi ya wanawake wanaozaliwa ni wachache.




Hapa haina maana wanawake ndiyo tunazaliwa wengi, sote tunazaliwa sawa… Wanaume wengi hufariki wakifikia utu uzima kuliko wanawake,” alisema Profesa Tibaijuka.




Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba katika kuzungumzia wanawake kuwa wengi kuliko wanaume, alisema inatoa changamoto kwa Serikali kutoa nafasi sawa kwa jinsi zote.




Chuo Kikuu cha Liverpool John Moores cha Uingereza, kiliwahi kutoa matokeo ya utafiti uliofanywa na jopo la wanasayansi yaliyoonesha kwamba wanawake wana uwezo wa kuishi miaka mingi zaidi ya wanaume.




Ilibainika kwamba nguvu ya moyo wa mwanamume hupungua kwa asilimia 20 – 25 kutoka miaka 18 hadi 70, lakini nguvu ya moyo wa wanawake wenye umri wa miaka 70 haitofautiani na ya vijana wenye umri wa miaka 20.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad