Rais Dkt. Magufuli afungua rasmi Barabara ya Bariadi-Lamadi na kuwahutubia Wananchi wa Bariadi mkoani Simiyu. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, January 11, 2017

Rais Dkt. Magufuli afungua rasmi Barabara ya Bariadi-Lamadi na kuwahutubia Wananchi wa Bariadi mkoani Simiyu.

Rais Dkt. John Pombe Magufuli akiwapungia mkono wakazi wa Bariadi Leo hii January 11,2017, mara baada ya kumaliza kufungua barabara ya Bariadi-Lamadi yenye urefu wa kilometa 71.8.

Rais Dkt. John Pombe Magufuli akiweka jiwe la ufunguzi wa barabara ya Bariadi-Lamadi yenye kilometa 71.8 .

Wengine katika picha ni  Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Antony Mtaka, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano Luhaga Mpina, Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, Mwenyekiti wa CCM Simiyu Titus Kamani na Mbunge wa Bariadi Andrew Chenge.
Rais Dkt. John Pombe Magufuli akikata utepe  na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Antony Mtaka pamoja na Waziri wa Ujenzi Profesa Makame Mbarawa kuashiria ufunguzi wa barabara ya Barabara ya Bariadi-Lamadi yenye kilometa 71.8.
Rais John Pombe Magufuli, leo Januri 11, 2017 amefanya ziara na katika Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu na kufanikiwa kuzungumza na mamia ya wananchi wa wilaya hiyo katika waliojitokeza katika uwanja wa Shule ya Msingi Somanda wilayani humo.

Nimekuwekea sentensi chache ikiwa ni sehemu ya hotubaya Rais Magufuli, Bariadi leo.

“Wanaolalamika fedha hakuna ni wale waliokuwa wanafaidi fedha ambazo tumezichukuwa na kuzipeleka kwenye maendeleo ya wananchi.

“Mimi ninaopambana nao ni wale waliosababisha tukawa masikini, hao ndio nakula nao sahani moja na naomba mniunge mkono.

“Tunataka kuanzia mwaka kesho hapa Bariadi tujenge uwanja wa ndege. Wageni wakija hapa na uchumi wa Bariadi utakuwa na tutanufaika mno.

“Katika maendeleo machungu lazima yawepo. Ukitaka kufanya kazi lazima wawepo watakaoumia.
Wakazi wa mkoa wa Simiyu, nawaomba barabara hii muitunze ili iwatunze. Barabara hii nzuri isiwe chanzo cha mauaji ya Watanzania.

“Lakini muitumie barabara hii kwa ajili ya biashara, safirisheni bidhaa mbalimbali ikiwemo mazao hata Dar es Salamm mkauzie huko.

“Naomba msing’oe alama za barabara, hasa madereva wa baiskeli huwa mnangoa ‘reflector’ na kufunga kwenye baiskeli.”

“Mimi ni mgumu sana kumpongeza mtu, lakini nakupongeza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, viongozi wengine waige kutoka kwako. Mkuu wa Mkoa wa Simiyu ameanzisha programu wa Wilaya Moja, Bidhaa Moja ambapo kila wilaya itakuwa ikizalisha bidhaa yake tofauti na nyingine.

“Tumekuwa tukitegemea mvua sana, lakini ni wakati wa kulima mazao ya muda mfupi na ambayo hayahitaji maji mengi sana.

“Kuna watu bado mzee bure hajatoka kichwani mwao kila kitu wanategemea serikali, serikali yangu haitatoa kila kitu. 

“Kuna wengine Busega wamelima pembeni ya ziwa, mahindi yamekauka, yani ameshindwa hata kumwagilia, nimesema sileti chakula. Wengine wanatumia magazeti kutangaza kuna njaa ili walete mahindi kutoka Brazil wasamehewe kodi.

“Kuna mmoja kaleta mahindi tani 25,000 kutoka Brazil hayana ubora na anataka asamehewe kodi, nimesema tutakata kodi yote. Wabunge waliruhusu chakula kipelekwe Uganda lakini wao leo ndio wanalia njaa, nimesema chakula sileti, fanyeni kazi.

“Nimeweka jiwe la msingi kwenye hospitali leo hapa Simiyu nikaambiwa itatumia bilioni 46, nasema haliwezekani chini ya uongozi wangu. Mimi nitaleta TZS bilioni 10 na nataka jengo hilo la hospitali likamilike kwa hiyo fedha na si bilioni 46 mnazoniambia. Na jengo hilo likikamilika nitakuja kulizindua mimi. 
Na kama kuna kiongozi wa TBA anaweka cha juu, Waziri Mbarawa mfukuze kazi.

“Wananchi mmezoea sana kubembelezwa na kuambiwa maneno mazuri, ni wakati sasa niwaambie ukweli hata kama unauma. Jiwe nitaliita jiwe, sitaliita mchanga uliokusanyika pamoja.

“Nataka hospitali hii ikamilike kwa gharama ambazo hata ukimwambia mtoto mdogo atakuelewa na si kukushangaa. Wakala wa Barabara Tanzania (TanRoads) ni watatu kwa ubora Afrika, ya kwanza ni ya Afrika Kusini, Namibia alafu Tanzania. Mkataba wa hii barabara unataka mhandisi akishakabidhi barabara, likitokea shimo kwa miaka miwili ajaziba kwa gharama zake.

“Tumenunua ndege 6, tutanunua meli kuwa Ziwa Victoria, tunajenga reli ya kisasa ya kati, lakini wapinzani hawayaoni haya mazuri. Serikali inafanya mambo mengine makubwa. Sasa msitegemee serikali ifanye haya yote na chakula iwagawie, haiwezekani.

Mbali na hayo, Rais Magufuli amemhoji Mhandisi wa maji Busega kumtaka aseme ni lini maji yatafika mjini hapo huku akiagiza kufutwa kwa leseni ya mwekezaji wa madini Bariadi endapo ataona kuwekwa tenki la maji kutamzuia kuchimba madini.

“Maji ni yetu na madini ni yetu, haiwezekani watanzania hawa wakose maji kwasababu eti, mwekezaji atashindwa kuchimba madini. Tena ikiwezekana mwambieni huyo mwekezaji hilo tenki atujengee yeye. Tenki lijengwe juu yeye madini ayachimbe chini.

“Mimi si Rais, urais ni wenu ninyi mliosimama kwenye jua na mvua tena mkiwa na njaa mkapiga kura, sina cha kuwalipa. Inawezekana nisiwe mwanasiasa mzuri lakini siku moja mtakumbuka niliyoyafanya. Nia yangu ni nzuri mbele yenu ya mbele ya Mungu.”  Alisema Rais Magufuli.

Rais Dkt  Magufuli akamaliza kuzungumza na wananchi wa Bariadi kwa kuwataka kuiunga mkono serikali yake katika kupambana na rushwa pamoja na ufisadi sambamba na kuwasihi kufanya kazi kwa bidii kwa ajiliya maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad