SAA 72:-Mwisho wa Gwiji wa Muziki wa Dansi Tazania Maalim Gurumo…’’Mungu ailaze roho ya marehemu maali pema peponi.. Amina’’. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Tuesday, April 15, 2014

SAA 72:-Mwisho wa Gwiji wa Muziki wa Dansi Tazania Maalim Gurumo…’’Mungu ailaze roho ya marehemu maali pema peponi.. Amina’’.




Mwanamuziki Muhidini Maalim Gurumo akiwa mahututi katika hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo mwili wa gwiji huyo wa muziki wa dansi nchini unatarajiwa kuagwa rasmi leo(April 15,2014) kuanzia saa 2 asubuhi kabla ya kusafirishwa kwenda kijijini kwao Masaki kwa ajili ya maziko yatakayofanyika mchana… Awali ilipangwa marehemu Gurumo aliyefariki juzi katika hospitali ya Muhimbili azikwe jana, lakini atazikwa leo kwa kuzingatia wosia ulioachwa na kusisitizwa na gwiji huyo enzi za uhai kuwa asiharakishwe kuzikwa mapema na familia imeamua kutii wosia huo.
Mwanamuziki nguli wa muziki wa dansi nchini, Muhidini Maalim Gurumo aliyefahamika pia kama kamanda na mashabiki wa muziki wa dansi, aliyeaga dunia Jumapili iliyopita katika Hospitali ya Muhimbili jijini Dar, alikutana na mateso ya kwa saa 72 za mwisho wake baada ya kulazwa akiwa taabani kwa siku tatu.

Mtoto wa marehemu anayejulikana kwa jina la Abdalah aliliambia Uwazi  kuwa siku mauti yalipomfika baba yake katika wodi namba sita Jengo la Mwaisela, alimtembelea na kumkuta akiwa katika hali nzuri na alipopewa chakula alikula, akashiba lakini cha ajabu alisema hatakula tena.
 
Kijana huyo alisema muda mfupi baadaye, hali ya baba yake ilibadilika, akaanza kupumua kwa shida ndipo alipozidiwa na baadaye kukata roho.

Mzee Gurumo alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa mapafu kwa muda mrefu na aliwahi kulazwa katika hospitali hiyo ya Muhimbili.
 
Baadhi ya watu waliomtembelea mzee Gurumo kwa nyakati tofauti akiwa hospitalini hapo ni pamoja na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ambaye alimuombea afya njema na akaruhusiwa kurudi nyumbani.

Kifo chake kimeacha simanzi si tu kwa familia yake, bali kwa wadau wa muziki wa dansi kwani alikuwa mwalimu na kiongozi wa wanamuziki wengi ambao sasa wanatamba.

Baada ya kustaafu muziki, Mzee aliwahi kupewa zawadi ya gari na msanii wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul ‘Diamond Platnumz’ aina ya Toyota Funcargo.
 
Akizungumzia msiba huo, Kiongozi wa Bendi ya Extra Bongo, Ally Choki alisema wamempoteza mwalimu wa muziki asiyekuwa na choyo ya kuelimisha.

“Ni kama tumepoteza tochi tukiwa kwenye msitu mnene usiku wa manane,” alisema.
 
Naye msemaji wa Bendi ya Mlimani Park Ochestra (Sikinde Ngoma ya Ukae), Jimmy Chika alipozungumza na Uwazi alisema mzee Gurumo aliwahi kuja kuwatembelea na kuimba mwezi mmoja uliopita katika Ukumbi wa DDC, Kariakoo jijini Dar.
 
“Alikuja kama mara tatu hivi ukumbini, naona alikuwa kama anatuaga kwa sababu alikuwa mwanzilishi wa bendi na mbunifu wa mtindo wa Sikinde, aliubuni Septemba, 1978,” alisema Chika.

Mzee Kassim Mapili, mwanamuziki wa mkongwe, kwa upande wake alisema kifo cha Gurumo ni pengo kubwa ambalo haliwezi kuzibika na akafafanua kuwa ni mtu ambaye hakuwa mbinafsi.

Baadhi ya wanamuziki ambao amefanya nao kazi kwa karibu ambao sasa watakuwa wanamlilia mwalimu wao ni pamoja na Hassan Rehani Bitchuka, Said Mabela, Roman Mng’ande ‘Romario’ na wengine wengi.
 
Gurumo pia ameacha simanzi katika miji mbalimbali nchini kwa kuwa amewahi kutembelea kimuziki na alifanikiwa kujizolea mashabiki lukuki.
 
Hadi Uwazi  linakwenda mitamboni msiba ulikuwa nyumbani kwake Mabibo, Dar huku taratibu za mazishi zikifanyika. 


Marehemu Gurumo aliyezaliwa mwaka 1940 ameacha mjane mmoja na watoto sita, watatu wa kiume ambao ni Abdallah, Omar na Mwalimu na wa kike pia wakiwa watatu ambao ni Mariam, ambaye ndiye mtoto mkubwa wa marehemu, Mwazani na Kibibi aliye wa mwisho kuzaliwa.

Mungu ailaze roho ya marehemu maali pema peponi. Amina.

Credit:- Gazeti la Uwazi/ GPL

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad