Ajali yaua watu 13 katika ajali mbaya iliyotokea kijiji cha Ngongwa mkoani Shinyanga. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Thursday, August 29, 2013

Ajali yaua watu 13 katika ajali mbaya iliyotokea kijiji cha Ngongwa mkoani Shinyanga.

Watu kumi na tatu (13) wamefariki na wengine kumi na moja(11) kujeruhiwa katika ajali mbaya iliyotokea usiku katika kijiji cha Ngongwa mkoani Shinyanga. Ajali hiyo iliyohusisha gari aina ya Hice yenye namba za usajili T 756 CHX na gari jingine lilokuwa limeharibika T 696 AMS.
Watu 13 wamepoteza maisha papohapo akiwamo mtoto mchanga wa miezi saba, baada ya gari walilokuwa wakisafiria kugonga lori la mizigo lililokuwa limeharibika barabarani katika Kijiji cha Ngongwa, wilayani Kahama, Mkoa wa Shinyanga.

Ajali hiyo ilitokea juzi(Agost 27,2013) saa 2:30 usiku wakati gari aina ya Toyota Hiace lilipoligonga lori.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kihenya Kihenya, alisema Hiace hiyo ilikuwa ikifanya safari zake kutoka mjini Kahama kwenda mji mdogo wa Ushirombo, katika Wilaya ya Bukombe, mkoani Geita.

Kihenya alisema watu 11 akiwamo dereva ambaye pia ni mmiliki wa gari hilo, Ezekiel Werema, walifariki dunia papohapo na wengine wawili walifariki dunia wakiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama kwa matibabu.

Aliwataja waliofariki dunia na sehemu wanazotoka kwenye mabano kuwa ni Ezekiel Mniko, Peter Daud (Ushirombo), Mlekwa Maduha (Mbogwe), Kisandu Jumanne (Mwanza), David Charles (Mwanafunzi Kanembe Sekondari-Bariadi) na Levina John (Shirati).

Alisema maiti nyingine hazijatambuliwa na kwamba mpaka jana, polisi walikuwa wakihangaika kupata majina ya marehemu na sehemu wanazotoka.

Alisema hata majeruhi wa ajali hiyo, majina yao hayajafamika kutokana na wengi wao kuumia vibaya na kushindwa kuongea.
Alisema polisi wanahangaika kutafuta majina ya marehemu na majeruhi, ili ndugu na jamaa zao waweze kutaarifiwa.

Pia, Kihenya aliwashukuru wananchi wa kijiji hicho kwa ushirikiano walioonyeshwa kwa polisi baada ya ajali kutokea na kuongeza kuwa, hadi sasa baadhi ya watu tayari wamejitokeza Hospitali ya Wilaya ya Kahama kutambua maiti.

Kamanda Kihenya alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendokasi, huku akitoa wito kwa madereva kuwa makini wanapoendesha magari hasa nyakati za usiku.


Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi Hospitali ya Wilaya ya Kahama, Dk Joseph Fwoma alithibitisha kupokea maiti 11 kutoka eneo la ajali na kwamba, majeruhi wawili walifariki dunia wakipatiwa matibabu hospitalini hapo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad