Watu
13 wamepoteza maisha papohapo akiwamo mtoto mchanga wa miezi saba, baada ya
gari walilokuwa wakisafiria kugonga lori la mizigo lililokuwa limeharibika
barabarani katika Kijiji cha Ngongwa, wilayani Kahama, Mkoa wa Shinyanga.
Ajali
hiyo ilitokea juzi(Agost 27,2013) saa 2:30 usiku wakati gari aina ya Toyota
Hiace lilipoligonga lori.
Kaimu
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kihenya Kihenya, alisema Hiace hiyo
ilikuwa ikifanya safari zake kutoka mjini Kahama kwenda mji mdogo wa Ushirombo,
katika Wilaya ya Bukombe, mkoani Geita.
Kihenya
alisema watu 11 akiwamo dereva ambaye pia ni mmiliki wa gari hilo, Ezekiel
Werema, walifariki dunia papohapo na wengine wawili walifariki dunia wakiwa
katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama kwa matibabu.
Aliwataja
waliofariki dunia na sehemu wanazotoka kwenye mabano kuwa ni Ezekiel Mniko,
Peter Daud (Ushirombo), Mlekwa Maduha (Mbogwe), Kisandu Jumanne (Mwanza), David
Charles (Mwanafunzi Kanembe Sekondari-Bariadi) na Levina John (Shirati).
Alisema
maiti nyingine hazijatambuliwa na kwamba mpaka jana, polisi walikuwa
wakihangaika kupata majina ya marehemu na sehemu wanazotoka.
Alisema
hata majeruhi wa ajali hiyo, majina yao hayajafamika kutokana na wengi wao
kuumia vibaya na kushindwa kuongea.
Alisema
polisi wanahangaika kutafuta majina ya marehemu na majeruhi, ili ndugu na jamaa
zao waweze kutaarifiwa.
Pia,
Kihenya aliwashukuru wananchi wa kijiji hicho kwa ushirikiano walioonyeshwa kwa
polisi baada ya ajali kutokea na kuongeza kuwa, hadi sasa baadhi ya watu tayari
wamejitokeza Hospitali ya Wilaya ya Kahama kutambua maiti.
Kamanda
Kihenya alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendokasi, huku akitoa wito kwa
madereva kuwa makini wanapoendesha magari hasa nyakati za usiku.
Kwa
upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi Hospitali ya Wilaya ya Kahama, Dk Joseph
Fwoma alithibitisha kupokea maiti 11 kutoka eneo la ajali na kwamba, majeruhi
wawili walifariki dunia wakipatiwa matibabu hospitalini hapo.
No comments:
Post a Comment