Naibu Waziri
wa Elimu Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Kassimu Majaliwa, amesema kuanzia
sasa kazi ya kuandikisha wanafunzi kuanza madarasa ya awali na yale ya msingi,
itafanywa na watendaji wa vijiji na si walimu wakuu wa shule za msingi.
Majaliwa
aliyasema hayo juzi, wakati akizungumza na walimu wakuu wa shule za sekondari
na baadhi ya viongozi wa sekta ya elimu mkoani hapa,katika mkutano uliofanyika
kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa mjini hapa.
Alisema
watendaji wa vijiji ndio wanawafahamu zaidi watoto wanaostahili kuanza elimu ya
awali na msingi kuliko walimu wakuu wa
shule za msingi katika maeneo husika.
Alisema
kutokana na ukweli huo, kazi ya uandikishaji watoto wenye sifa ya kuanza
madarasa ya awali na yale ya msingi, ni watendaji wa vijiji na kazi
hiyo,itakuwa na ufanisi mkubwa kuliko kipindi cha miaka ya nyuma.
“Kwa hiyo,
kuanzia sasa kazi ya kuanza kuandikisha wanafunzi wa madarasa ya awali na ya
msingi, itaanza mapema mara tu shule zitakapofunguliwa Januari na hadi kufikia
Agosti ya mwaka husika, kazi hiyo itakuwa imekamilika.Kwa sasa hatutasubiri
hadi mwishoni mwa mwaka kuandikisha wanafunzi”, alifafanua Majaliwa.
Aidha, Naibu
Waziri huyo, alisema kuwa kila mtendaji wa kijiji, anapaswa kuwakilisha ripoti
ya kazi ya uandikishaji wanafunzi wa shule za awali na wale wa msingi mbele ya
Kikao cha Maendeleo ya Kata (WDC),ili kupata Baraka ya kikao hicho.
Alisema ili
kuipa umuhimu mkubwa elimu ya awali, ni lazima kuwepo na bajeti ambazo zitaonyesha
ongezeko la shule za awali.
Katika
hatuna nyingine, Naibu waziri huyo alikumbusha kuwa kila shule ya msingi, ni
lazima iwe na vyumba vya kutosha vya madarasa ya awali.
“Wanafunzi
wa shule za awali sio walundikwe tu madarasa au wawe wa kucheza tu kipindi
chote wawapo shuleni, hapana, ihakikishwe wanasoma kikamilifu ili wakianza
darasa la kwanza katika shule za msingi, wawe wameiva barabara,” alisema
Majaliwa.







No comments:
Post a Comment