Timu
ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, imewatandika wenzao wa Kenya, Harambee Stars bao 1-0 kwenye Uwanja wa
CCM Kirumba mjini Mwanza jioni hii katika mchezo wa kirafiki wa Kimataifa ulio
katika kalenda ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
Hadi
mapumziko, Taifa Stars ilikuwa mbele kwa bao 1-0 lililofungwa na beki
Aggrey Morris katika dakika ya nne, baada ya kupanda kusaidia mashambulizi.
Katika
mechi hiyo iliyochezeshwa na refa anayetambuliwa na FIFA, Oden Mbaga, Harambee
Stars, walio chini ya Kocha kutoka Ufaransa, Henri Michel walitawala dakika 10 za mwanzo,kwa kumchezesha
Staa wao anaecheza Klabu ya Ufaransa ya Auxerre, Dennis Oliech na Taifa Stars,
chini ya Kocha kutoka Denmark, Kim Poulsen, walimchezesha Staa wa TP Mazembe ya
Congo DR, Mbwana Samatta.
Baada
ya mchezo huo, kocha wa Harambee, Mfaransa Michel alionyesha kukerwa na matokeo
hayo na kusema timu yake haikucheza vizuri, wakati Polusen, amefurahia ushindi
huo akisema timu yake haijacheza kwa miezi miwili na baada ya siku mbili za
mazoezi wameifunga Kenya.
Katika
hatua Nyingine Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) limefanya mabadiliko kwa kiingilio cha juu cha mechi ya
raundi ya mwisho ya mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa
vijana wenye umri chini ya miaka 17 kati ya Tanzania (Serengeti Boys) na Congo
Brazzaville itakayochezwa Jumapili (Novemba 18 mwaka huu).
Awali
kiingilio cha juu katika mechi hiyo itakayofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni kilikuwa sh. 5,000. Lakini kwa lengo la
kuwafanya wadau wa kiingilio hicho kuchangia gharama za mechi hiyo sasa
kutakuwa na viingilio vitatu tofauti katika viti vya VIP.
Kwa
VIP A ambayo ina viti 748 kiingilio kitakuwa sh. 10,000, VIP B inayochukua
watazamaji 4,160 kiingilio ni sh. 5,000 wakati VIP C yenye viti 4,060 kiingilio
ni sh. 2,000. Kwa sehemu nyingine (viti vya rangi ya chungwa, kijani na bluu)
ambavyo jumla yake ni 48,590 kiingilio kitabaki kuwa sh. 1,000.
Timu
ya Congo Brazzaville kwa taarifa tulizopata awali kutoka Shirikisho la Mpira wa
Miguu la Congo (FCF) ilikuwa iwasili jana (Novemba 13 mwaka huu) usiku. Lakini
timu hiyo haikutokea na sasa tunatarajia itawasili leo (Novemba 14 mwaka huu)
saa 8 mchana kwa ndege ya Ethiopian Airlines. Congo itafikia Sapphire Court
Hotel.
Wakati
huo huo, Kamati ya Serengeti Boys
itakutana na waandishi wa habari kesho (Novemba 15 mwaka huu). Mkutano huo
utafanyika kuanzia saa 5 asubuhi hoteli ya JB Belmont, ukumbi wa Ngorongoro.
Boniface
Wambura
Ofisa
Habari
Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
No comments:
Post a Comment