Mungu akulaze pema penye wema Mariam Khamis....yote Mwenyezi Mungu anapanga. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, November 14, 2012

Mungu akulaze pema penye wema Mariam Khamis....yote Mwenyezi Mungu anapanga.

Mariam Khamis
Mazishi ya aliyekuwa mwimbaji mahiri wa taarabu hapa  nchini Mariam Khamis ‘Paka Mapepe’, yanatarajiwa kufanyika leo Jumatano, Magomeni Makuti wilayani Kinondoni, jijini Dar es Salaam.




Mariam (pichani) ambaye hadi anafariki alikuwa ni mwajiriwa wa TOT Taarab, alimefariki alfajiri ya kuamkia leo kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kifo chake kikitokana na matatizo ya uzazi, ingawa mtoto wake yu salama.


Kwa mujibu wa Baba Mdogo wa marehemu anayetajwa kwa jina moja la Sembuli, alisema kuwa, wamefikia uamuzi wa kumzika marehemu leo, baada ya kuombwa na Mkurugenzi wa TOT Kapten Komba kufanya hivyo ili wapate kuhudhuria mazishi ya mfanyakazi mwenzao.


Mariam Khamis alitamba sana na wimbo wa Mapaka Mapepe alouimba akiwa na Melody, kiasi cha kumpa jina hilo la utani, kabla ya kujiunga na Zanzibar Stars, kisha Five Stars na hatimae TOT.


Wimbo wake wa kwanza kurekodi na TOT ulikuwa ni ‘Sidhuriki na Lawama’ ambao unatamba sana hadi sasa anapopchukuliwa na mauti yaliyoelezwa kutokana na Kifafa cha Uzazi alichokumbana nacho baada ya kujifungua kwa operesheni kubwa.


Alijiunga na TOT Taarab mwanzoni mwa mwaka jana, akitokea katika kundi la Five Stars Modern Taarab aliloingia mwishoni mwa mwaka 2009.
Mariam Khamis aliipa kisogo Five Stars na kuhamia TOT  Taarab muda mfupi kabla ya ajali ya kundi hilo iliyosababisha vifo vya wasanii 13, akiwemo kijana mahiri Issa Kijoti mnamo mwezi Machi, mwaka jana katika eneo la Mikumi Morogoro.


Akiwa Five Stars, alitikisa kwa vibao viwili ikiwemo ‘Ndo Basi Tena’ pamoja na ‘Uzushi Haunitii Doa’ .


Historia yake kimuziki ilianzia mwaka 2003, mara baada ya kuhitimu elimu ya sekondari, ambako alipenda sana Taarab, kwa kuvutiwa na magwiji wa mipasho.


Baadhi ya magwiji hao waliokuwa wakimvutia Mariam Khamis ni pamoja na Zuhura Shaaban, ‘Malkia wa Mipasho’ , Khadija Kopa na marehemu Nasma Khamis ‘Kidogo’.


Kati ya watu waliogundua mapema kipaji chake cha uimbaji na kukifanyia kazi, ni baba yake mdogo aitwaye Kessy Abdallah ambaye alimuunganisha kwenye kundi la Segere No2, jijini Dar es Salaam, ili kujifua zaidi.



Akiwa Segere, ambalo baadhi ya vinara wake alikuwa Mussa Msuba,
alirekodi kibao kimoja kinachokwenda kwa jina la ‘Mpenzi’na kabla albamu yake haijatoka, kundi lilisambaratika.


Mwaka 2007, Mussa Mipango, kati ya wapigaji mahiri wa gitaa zito, Besi hapa nchini, aliyeko TOT Taarab hivi sasa, alimuunganishia katika kundi la Zanzibar Stars Modern Taarab ‘Watoto wa Pwani’.


Hakukaa sana Zanzibar Stars kwani mwaka huohuo, 2007 alihamia East African Melody Taarab alikorekodi kibao ‘Paka Mapepe’ kilichotokea kutikisa kiasi cha mashabiki kuamua jina hilo liwe la kwake moja kwa moja.


Mwaka 2008, alirejea Zanzibar Stars alikofikia kurekodi kibao ‘Huliwezi Bifu’, kabla ya vingine kama vile; ‘Raha ya Mapenzi’, ‘Narindima Mie’ na ‘Shoga Habari Ndo Hiyo’ .


Mara baada ya kuingia TOT  Taarab, alipewa kurekodi kibao ‘Sidhuriki na Lawama’, ambacho hata mwenyewe alikuwa akithibitisha kuwa, kilitokea kumsogeza na mashabiki wengi wa mipasho.


Kati ya watu ambao mara kwa mara alipenda kuwataja kuwa ni miongoni mwa waliochangia kumfikisha alipoishia, ni pamoja na baba na mama yake waliompa moyo tangu alipoanza kujiingiza katika muziki.


Aidha, alikuwa pia akipenda kuvishukuru vikundi vyote vya muziki wa taarab alivyopitia ikiwamo Melody na mashabiki pamoja na wapenzi wote kwa ujumla.


Paka Mapepe alizaliwa mwaka 1986, jijini Dar es Salaam na kupata elimu ya msingi katika shule ya Amana, Ilala kuanzia mwaka 1994 hadi 2000 na sekondari ya Jamhuri kati ya mwaka 2001 na 2003.


Aliolewa na mpiga gita la besi mahiri wa gitaa la Besi, Haji Kijungu, aliyejaliwa kuzaa naye mtoto mmoja aitwaye Taliq (6) pamoja na mwingine aliyezaliwa na kusababisha kifo chake.


Wasanii mbalimbali wa muziki nchini, hususani wa Taarabu, wameelezea kustushwa na kifo cha Mariam, ambapo Habari Mseto ulishuhudia waimbaji na mashabiki mbalimbali kwenye Hospitali ya Muhimbili, ulikohifadhiwa mwili wa marehemu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad