Waziri mkuu Bw Mizengo Pinda ameongoza maelfu ya wakazi wa mji wa Mpanda kuuzika mwili wa Askofu Paschal Wiliamu Kikoti wa kanisa katoliki jimbo la Mpanda. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Sunday, September 02, 2012

Waziri mkuu Bw Mizengo Pinda ameongoza maelfu ya wakazi wa mji wa Mpanda kuuzika mwili wa Askofu Paschal Wiliamu Kikoti wa kanisa katoliki jimbo la Mpanda.


Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kitoa heshima za mwisho kwa marehemu Mhashamu, Askofu Pascal William Kikoti katika ibada ya mazishi iliyofanyika kwenye kanisa kuu katoliki, jimbo la Mpanda, Septemba 1, 2012.(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).


Waziri mkuu  Mizengo Pinda amesema Serikali imefadhaishwa na msiba wa Askofu wa Kwanza wa Jimbo Katoliki la Mpanda Mhashamu Pascal William Kikoti ambao ulitokea kwa ghafla sana.


Waziri Mkuu ametoa salaam hizo leo mchana (Jumamosi, Septemba Mosi, 2012) kwenye ibada ya mazishi ya Askofu iliyofanyika kwenye Kanisa la Mt. Maria Imakulata mjini Mpanda.


Mhashamu Askofu Kikoti alifariki dunia Agosti 28, mwaka huu katika Hospitali ya Bugando, jijini Mwanza amezikwa kwenye kanisa hilo ambalo ndiyo makao makuu ya Jimbo Katoliki Mpanda.




Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akitupa mchanga kwenye kaburi la Askofu Pascal William Kikoti katika mazishi yaliyofanyika kwenye Kanisa Kuu la Katoliki jimbo la Mpanda mjini Mpanda Septemba 1, 2012. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).



Waziri Mkuu alisema: “Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wote wa Serikali kwa jumla, tumefadhaishwa sana na msiba huu mkubwa, tena uliotokea kwa ghafla. Lakini kwa kuwa haya ni mapenzi yake Mungu ambaye ndiye Muumba wetu sote tumelazimika kuipokea taarifa hii kwa majonzi makubwa.”


Alisema yeye binafsi alifarijika sana na uongozi wake, maono yake na shauku yake ya kutoa huduma za kiroho na za kijamii kwa jumla. Alisema mchango wake umegusa jamii nzima na siyo tu katika kutoa huduma za kiroho, bali pia huduma za kijamii zilizolenga kuleta maendeleo kwa wananchi katika Jimbo la Mpanda na nchini kote.


“Mhashamu Askofu Kikoti, ametutoka akiwa na umri mdogo sana wa kichungaji wa miaka 55, baada ya kulitumikia jimbo hili kwa miaka 11. Kabla ya kifo chake alikuwa na malengo mengi mazuri yakiwemo ya kufungua Seminari Ndogo ya Jimbo, kujenga Kituo cha Kichungaji na Kijamii na kupanua Shule ya Sekondari ya Mtakatifu Maria ya hapa Mpanda. Hivyo basi ni dhahiri kwamba kifo hiki ni pigo kubwa siyo kwangu, au kwa waumini wa Kanisa Katoliki, au Wanampanda tu, bali wananchi wote nchini kwa jumla,” alisema.




Mapadri wakiweka kaburini mwili wa  aliyekuwa Askofu wa jimbo  la Mpanda  Mhashamu  Pascal William Kikoti kaburini katika mazishi yaliyofanyika kwenye kanisa kuu la jimbo Katoliki la Mpada Mjini Mapanda Septemba 1, 2012.(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).


Mapema akitoa salaam za Baba Mtakatifu katika ibada hiyo ya mazishi, Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania, Mhashamu Askofu Francisco Montecillo Padilla alisema hayati Baba Askofu Kikoti hatasahaulika kwa mema aliyoyatenda Iringa akiwa Padri na hapa Mpanda akiwa Askofu.


“Nilimfahamu Askofu Kikoti Februari, mwaka huu mara baada ya kuanza kazi hapa nchini… alikuwa ni mtu wa maneno machache lakini wa vitendo zaidi. Tunashukuru kwa kuijenga Dayosisi hii mpaka sasa, kuwajali watu wake na zaidi ya yote kuwapenda,” alisema.


Aliwasihi waumini wa Jimbo Katoliki la Mpanda kuendelea kuwa na umoja hasa katika kipindi hiki cha majonzi.


Ibada hiyo iliyoongozwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, ilihudhuriwa na Maaskofu 28 kutoka majimbo mbalimbali ya Tanzania isipokuwa Askofu Renatus Msonganzila wa Musoma na Askofu Aloycius Balina wa Shinyanga ambao walitajwa kuwa ni wagonjwa.


 Maaskofu wa Mbulu na Moshi waliwakilishwa na wasaidizi wao.




Wakati huohuo, katika ibada hiyo ya mazishi, Askofu Damian Kyaruzi wa Jimbo Katoliki la Sumbawanga alitangazwa rasmi kuwa ameteuliwa na Baba Mtakatifu Benedict wa 16 kuwa Msimamizi wa Kitume wa Jimbo Katoliki la Mpanda hadi atakapotangazwa Askofu mwingine. 


Uteuzi wake ulianza  (Ijumaa, Agosti 31, 2012). 




Askofu Dk Paschal William Kikoti (55), amefariki dunia kutokana na ugonjwa wa shinikizo la damu ambalo lilipanda kufikia 240 hadi 260, hali iliyomsababishia kifo katika Hospitali ya Bugando, Mwanza. 

 Historia yake.



Askofu Kikoti alizaliwa Machi 3, 1957 huko Ihimbo, Parokia ya Nyabula, Jimbo Katoliki la Iringa.


 Alipata elimu ya msingi katika Shule ya Msingi Iringa, kisha elimu ya sekondari katika Seminari ndogo ya Mafinga na mafunzo ya falsafa katika Seminari ya Peramiho, Songea pamoja na Seminari Kuu ya Ntungamo, Bukoba.


Kwa upande wa theolojia, alisoma Seminari Kuu ya Kipalapala, Tabora na mwaka 1988 alipata daraja la upadri.


Baada ya upadrisho wake, alifanya kazi jimboni Iringa na kati ya mwaka 1989- 1990 alikwenda masomoni Rome, Italia ambako alisomea Historia ya Mababu wa Kanisa na Theolojia na kupata Udaktari wa Falsafa (PhD).


Mwaka 1997alirudi nchini na kufundisha katika Seminari ya Peramiho na Novemba 4, 2004, aliteuliwa na Baba Mtakatifu kuwa Askofu wa kwanza wa Jimbo la Mpanda na alisimikwa rasmi Januari 14, 2001 hadi umati ulipomfika.


Pia, alikuwa Mwenyekiti wa Idara ya Katekesi ya TEC tangu mwaka 2009 akisaidiwa na Katibu Mtendaji, Padri Raphael Madinda.



Napendwa kutoa pole kwa kanisa katoliki Tanzania ,Mwadhama kadinali, maaskofu na mapadri pamoja na  Wana Katavi  kwa kuondokewa na mwenzetu.MUNGU AIPE ROHO YA MAREHEMU PUMZIKO LA MILELE’’Amen.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad