Zaidi ya Raia Elfu 10 wa Kigeni waliokuwa wakiishi kinyume cha Sheria wamepokelewa nchini Rwanda,Burundi,Uganda na DRC wakitokea nchini Tanzania. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, August 21, 2013

Zaidi ya Raia Elfu 10 wa Kigeni waliokuwa wakiishi kinyume cha Sheria wamepokelewa nchini Rwanda,Burundi,Uganda na DRC wakitokea nchini Tanzania.

Eneo la Rusomo mpakani mwa Rwanda na Tanzania huku  Zaidi ya wanyarwanda Elfu Sita wamepokelewa nchini Rwanda wakitokea nchini Tanzania ambako  waliokuwa wanaishi nchini Tanzania kinyume cha sheria, na sasa serikali ya Rwanda imewapa hifadhi ya muda katika kambi iliyopo kilometa 6 kutoka mpaka wa Rwanda na Tanzania toka agizo la  Rais Jakaya Kikwete, lililowataka kurejea makwao kwa hiari yao ndani ya wiki mbili, kuanzia Julai 29, mwaka huu.







Kwa mujibu wa Afisa uhamiaji wa wilaya ya Ngara Mkoani Kagera Bw Marwa Kitang’ati amesema kuwa raia wa kigeni waliokuwa wanaishi nchini kinyume cha sheria elfu 7 na 850 wameondoka nchini kwa hiari kurejea katika nchi za Rwanda na Burudi kupitia vituo vitatu vya idara hiyo kwa Raia  elfu 4 na 748 wametumia kituo cha Rusumo kurejea nchini Rwanda huku wengine elfu 3 na 102 wakitumia vituo vya Mugoma, Murusagamba na Kabanga kurejea nchini Burundi na kwamba idadi hiyo ya wahamiaji walioondoka wilayani Ngara ni ile iliyopatikana katika vituo vilivyosajiliwa pekee na kwamba wengine wametumia njia zisizo rasmi kwa kuvuka mto Ruvubu wakitumia mitumbwi kuelekea Rwanda na Burundi.



Muonekano wa Daraja  la Rusomo mpakani mwa Rwanda na Tanzania ambalo limetumiwa na Raia wa kigeni  ambao wamekuwa wakiishi nchini kinyume cha sheria za nchi na taratibu za Idara ya Uhamiaji , wanatoka katika nchi za Rwanda, Burundi, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Serikali ya Tanzania  imetangaza rasmi kuendesha operesheni kabambe, itakayofanyika kwa kushtukiza wakati wowote kuanzia sasa, kuwaondoa kwa nguvu nchini Raia wa Kigeni wanaoishi nchini kinyume cha Sheria na waliokaidi agizo la  Rais Jakaya Kikwete, lililowataka kurejea makwao kwa hiari yao ndani ya wiki mbili, kuanzia Julai 29, mwaka huu.

Wahamiaji hao , ambao wamekuwa wakiishi nchini kinyume cha sheria za nchi na taratibu za Idara ya Uhamiaji, wanatoka katika nchi za Rwanda, Burundi, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Agizo hilo lilitolewa na Rais Kikwete Julai 29, mwaka huu, alipofanya ziara katika Mkoa wa Kagera, ambako aliwapa wiki mbili wahamiaji haramu wawe wamerudi makwao kwa hiari yao, vinginevyo wangekamatwa katika operesheni maalumu ya kijeshi baada ya muda huo kuisha.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, aliwaambia waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam jana(Agosti 20,2013) kuwa operesheni hiyo aliyoiita ya “ghafla”, itafanyika baada ya Rais Kikwete kumpa kibali cha kuiendesha.

Alisema maeneo yatakayohusika zaidi na operesheni hiyo ni ya mikoa ya Kanda ya Ziwa na kwamba, hawatakuwa na ‘msalie mtume’ kwa mgeni yeyote atakayebainika kuishi nchini isivyo halali.
  
Aliwataka viongozi wa serikali za vijiji vilivyoko katika mikoa ya kanda hiyo kufahamu kwamba, ni kosa kisheria kushirikiana na wahamiaji haramu.

Kutokana na hilo, alionya kuwa watakaobainika wakiwaficha Raia hao wasiokuwa na Kibali halali cha kuishi nchini, watakamatwa na kufikishwa mahakamani.

Awali, Waziri Nchimbi alisema baada ya agizo hilo la Rais Kikwete, mwitikio umekuwa mzuri na kwamba, hadi kufikia usiku wa Agosti 18, mwaka huu, Raia hao wasiokuwa na kibali halali cha kuishi nchini 10,672 walikuwa wameondoka nchini na mali zao.

Alisema kati ya wahamiaji hao , katika Mkoa wa Kagera, Wanyarwanda walikuwa 6,088, Warundi 4,000 na Waganda 269.

Kwa mujibu wa Waziri Nchimbi, katika Mkoa wa Kigoma, walioondoka ni 150, kati yao Warundi ni 142 na DRC ni wanane.

Alisema katika Mkoa wa Geita wahamiaji  walioondoka ni 165; kati yao Wanyarwanda ni 126 na Warundi 39.

Hata hivyo, alisema kazi ya wahamiaji hao kuondoka nchini, bado inaendelea na kuwataka wananchi hususan wa Mkoa wa Kagera kuwaacha waondoke bila kunyanyaswa, ikiwamo kupora mali zao.

Hata hivyo, alisema kati ya wahamiaji haramu walioondoka, 14 wamerudi tena nchini na kukiita kitendo hicho kuwa ni cha “kichokozi.”

Alisema Rais Kikwete alitoa agizo lile baada ya wizara kufanya utafiti na kumpa taarifa na kwamba, wahamiaji haramu wanaosumbua ni wale wanaomiliki vyeti bandia vya kuzaliwa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad