NEC yamvua rasmi uanachama Mansour huku Madiwani CCM Bukoba wakirudishwa rasmi. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Wednesday, August 28, 2013

NEC yamvua rasmi uanachama Mansour huku Madiwani CCM Bukoba wakirudishwa rasmi.

Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa imejadili na kutolea maamuzi pamoja na mambo mengine suala la Madiwani wanane waliotangazwa kufukuzwa uanachama na Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kagera.

Katika maamuzi yake, Kamati Kuu imebatilisha uamuzi uliofanywa na Halmashauri Kuu CCM ya Mkoa wa Kagera Agosti 13, 2013 wa kuwafukuza uanachama Madiwani hao. 

Hivyo Madiwani hao wanane ni wanachama halali wa CCM.

Kamati Kuu imetoa uamuzi huo, baada ya kubaini kuwa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kagera haikuzingatia Katiba ya CCM ya 1977 Toleo la 2012 Ibara ya 93 (15).

Ibara hiyo inasomeka kuwa moja ya kazi ya Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa ni:- “Kumwachisha au kumfukuza uongozi kiongozi yeyote ambaye uteuzi wake wa mwisho unafanywa na Halmashauri Kuu ya CCM ya Mkoa, isipokuwa kwa suala la kumvua uanachama au uongozi Diwani lisifanyike hadi Kamati Kuu imearifiwa na kutoa maelekezo”.


Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiongoza kikao maalum cha Kamati Kuu ya CCM, Makao Makuu ya CCM, mjini Dodoma jana, Agosti 25, 2013. Kikao hicho kilifanyika kwa ajili ya kukutana Mbunge wa Bukoba mjini Khamis Kagasheki, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Kagera, Constansia Buhiye,  Katibu wa CCM mkoa wa Kagera Abedi Mushi, Mwenyekiti na Katibu wa CCM wilaya ya Bukoba mjini na Meya wa Manispaa ya Bukoba Anatory Amani  kuhusu sakata la madiwani wa wanane wa CCM katika Manispaa ya Bukoba mjini. Kulia ni Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.

Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Kagera Constansia Muhiye na Katibu wa CCM wa mkoa huo, Abedi Mushi wakisubiri kuingia ukumbini kukutana na Kamati kuu mjini Dodoma .
Aidha, Kamati Kuu imewaonya Madiwani wa CCM wa Manispaa ya Bukoba, Mbunge wa Bukoba Mjini na Meya kwa kusababisha kukosekana kwa utulivu, mshikamano na amani katika Manispaa na Chama.

Kamati Kuu pia imeitaka Serikali kumwagiza mdhibiti na mkaguzi mkuu wa serikali(CAG) kufanya ukaguzi maalum wa haraka wa mambo yanayolalamikiwa dhidi ya Meya ili ukweli ujulikane na matokeo ya uchunguzi huo yasilishwe kwenye baraza la madiwani ili hatua stahiki zichukuliwe kwa mujibu wa sheria na taratibu zinazoongoza Serikali za Mitaa.

 Katibu wa Itikadi na
Uenezi -CCM Nape Nnauye.
Wakati tuhuma hizo dhidi ya Meya zikichunguzwa; Kamati Kuu inawataka Madiwani wa CCM kurejesha utulivu kwenye Manispaa na Chama kwa ujumla ili kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM na kuwaletea maendeleo wananchi wa Bukoba.

Katika hatua nyingine Mtikisiko mkubwa umekikumba Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya kubariki kufukuzwa uanachama kwa Mwakilishi wa Jimbo la Kiembesamaki, Mansoor Himid Yussuf.

Mbali ya uamuzi huo, CCM imefanya mabadiliko mengi katika jumuiya zake za Umoja wa Vijana (UVCCM) na Jumuiya ya Wazazi.

Uamuzi wa kufukuzwa Mansoor uanachama, umehitimisha safari ya mwanasiasa huyo mwenye ushawishi visiwani Zanzibar kupoteza rasmi uwakilishi wa jimbo.

Mansoor, amekuwa miongoni mwa Wazanzibari walio mstari wa mbele kutetea muundo wa Muungano, utakaoipa Zanzibar mamlaka kamili ya dola.

Akizungumza na waandishi wa habari jana(Agosti 27,2013), Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi Nape Nnauye alisema kikao cha NEC, kilijadili kwa kina tuhuma dhidi ya mwakilishi huyo na kutoka na uamuzi wa kumfukuza uanachama wa CCM.

Alisema NEC, ilipokea masuala mbalimbali yakiwemo maamuzi ya Kamati maalumu ya CCM Zanzibar dhidi ya Mansoor, ikiwemo kushindwa kusimamia malengo ya chama na kutekeleza masharti ya uanachama.

Tuhuma kubwa iliyowasilishwa mbele ya NEC, ni pamoja na kudaiwa kushindwa kutekeleza wajibu wa mwanachama na kukiuka maadili ya kiongozi.

Mbali na hilo, ilielezwa ameikana ilani ya CCM ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010-2015 na kukisaliti chama.

Kutokana na hali hiyo, Nape alisema baada ya kujiridhisha vya kutosha na tuhuma dhidi ya Mansoor, NEC iliridhia uamuzi wa kumfukuza uanachama.

“Yapo mambo mengi ambayo NEC imejadili katika kikao chake ikiwemo suala la Katiba Mpya, mgogoro wa umeya Bukoba ambapo hadi sasa bado haujamalizika.

Mbali na hilo, NEC imeridhia kufukuzwa kwa uanachama kwa Mansoor na kuanzia leo (jana) si kiongozi tena wa CCM,” alisema Nape.

Mwakilishi wa Jimbo la Kiembe Samaki, Mkoa wa Mjini Magharibi, Bw.Mansour Yussuf Himid na Kitendo cha kuungana na Mzee Moyo na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Seif Sharrif Hamad kupigia debe suala la Muungano wa Mkataba kati ya Tanganyika na Zanzibar kuliwakera makada wa CCM waliomchukulia kuwa anapingana na Katiba na Ilani ya CCM vilivyosimamia katika Serikali mbili.
Sakata la Mansoor la kufukuzwa kwake uanachama, lilianza katika kikao cha Kamati Maalumu iliyoketi Agosti 18, mwaka huu na kutoka na azimio la kumvua uanachama Mwakilishi huyo wa Kiembesamaki ambaye alidaiwa kukiuka maadili ya chama hicho.

Katika kikao hicho, Mansoor amekuwa akipingana na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010, inayoamini katika muundo wa Serikali mbili.

Kwa mara ya kwanza, tuhuma za Mansoor zilifikishwa katika kikao cha Kamati ya Maadili ya CCM Zanzibar, kilichoketi Agosti 16, 2013 katika Ofisi za CCM Kisiwandui ambapo wajumbe wa kamati hiyo kwa kauli moja walitoka na azimio la kumfuta uanachama mwakilishi huyo.

Dk. Shein ndiye aliyeongoza kikao cha Kamati ya Maadili, huku wajumbe wakiwa ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai, Mohamed Hija, Mbaruk Rashid Omari na Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Idd.

Kwenye kikao cha Mkoa wa Mjini Magharibi, Mansoor alitoa utetezi wake na kusema kuwa kama kufungwa afungwe, kama kunyongwa anyongwe na kama kufukuzwa afukuzwe, lakini anataka Serikali ya mkataba.

UTEUZI.

Kikao cha Halmashauri Kuu pia kimeridhia, uteuzi wa Makatibu wateule wapya wa Jumuiya za CCM, za Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Jumuia ya Wazazi na Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT).

Katika uteuzi huo mapendekezo hayo yaliyofanywa na Kamati Kuu ya CCM na kuridhiwa na NEC, kwa upande wa UVCCM ameteuliwa aliyekuwa Kaimu Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro, Sixtus Mapunda na kwa upande wa Jumuia ya Wazazi ni Mjumbe wa NEC kutoka Pemba, Seif Shabani Mohamed, huku kwa upande wa UWT akiachwa Katibu Mkuu wa sasa, Amina Makilagi.

Mapunda atachukua nafasi iliyokuwa imneshikiwa na Martine Shigela ambaye ameongoza UVCCM kwa miaka mitano sasa, na Seif Shabani Mohammed kutoka Pemba akichukua nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Hamis Suleiman Dadi ambaye pia amekuwa katika wadhifa kwa miaka mitano sasa.

Pia, NEC imeridhia mapendekezo  ya Kamati Kuu kwa ajili ya kuziba nafasi Makatibu wa CCM wa mikoa mitatu ya Morogoro, Kaskazini Pemba na Geita ambayo kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa imekuwa wazi kwa muda mrefu sasa kutrokana na sababu mbalimbali ikiwemo kifo.

Kufuatia mapendekezo hayo ya Kamati Kuu, ambayo yameridhiwa na NEC, walioteuliwa na mikoa yao ikiwa kwenye mabano ni Msaidizi Kitengo cha  Uchaguzi, CCM Ofdisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Romuli Rojas John (Morogoro), aliyekuwa Katibu Katibu wa wilaya ya Mkinga, Kassim Mabrouk Mbarak (Kaskazini Pemba) na aliyekuwa Katibu wa CCM Igunga, Mary Maziku (Geita).

Taarifa Rasmi ya CCM ya majina ya Makatibu wa Wilaya walioteuliwa na NEC

Ndugu Ashura Amanzi
Ndugu Rukia Saidi Mkindu
Ndugu Elias J. Mpanda
Ndugu Jonathan M. Mabihya
Ndugu Mulla Othman Zuberi
Ndugu Jumanne Kapinga
Ndugu Ali Haji Makame
Ndugu Jacob G. Makune
Ndugu Juma A. Mpeli
Ndugu Hawa Nanganjau
Ndugu Abdulrahman Shake
Ndugu Subira Mohamed Ameir
Ndugu Abdallah Shaban Kazwika
Ndugu Juma Bakari Nachembe
Ndugu Josephat Ndulango
Ndugu Rajab Uhonde
Ndugu Abeid Maila
Ndugu Mohamed Lawa
Ndugu Mariam Sangito Kaaya
Ndugu Bakar Lwasa Mfaume
Ndugu Julius Peter
Ndugu Jumanne Kitundu Mginga
Ndugu Mathias Nyombi
Ndugu Mohamed Hassan Moyo

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad